MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Tuesday, February 9, 2010

CUF: ziara ya JK Dar ilikuwa kampeni

Salim Said

CHAMA cha Wananchi (CUF) kimemshukia Mwenyekiti wa Chama Cha Mapnduzi (CCM) Rais Jakaya Kikwete kwamba, ziara yake jijini Dar es Salaam ililenga kujipigia kampeni na kwamba ni matumizi mabaya ya madaraka ya umma.

Rais Kikwete alifanya ziara ya siku tatu jijini hapa, ambapo wachambuzi wa mambo wameihusisha na kampeni zake za kuelekea uchaguzi mkuu wa 2010 huku akitarajiwa kuwa mgombea wa urais kupitia CCM.

Mkurugenzi wa Siasa wa CUF Mbarallah Maharagande, alisema CUF inasikitishwa na matumizi mabaya ya madaraka yaliyofanywa na Rais katika ziara zake zilizofanyika wiki iliyopita.

Maharagande alisema mwenyekiti huyo wa CCM alitumia ziara hiyo ya kichama kutoa ahadi mbali mbali za kiserikali huku baadhi ya wakati akitoa kauli za kutishia kuwawajibisha watendaji wa Serikali, ili kujisafishia njia.

“Katika ziara hiyo, pamoja na kuongozana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam William Lukuvi, ambapo si sahihi kabisa katika ziara za kichama lakini, Kikwete alitumia ziara hiyo ya kichama kutoa ahadi mbalimbali za kiserikali, huku akitoa kauli za kutishia kuwawajibisha watendaji wa Serikali, ili kujisafishia njia,” alisema Maharagande.

Alisema CUF inalaani vikali ziara hiyo ambayo alidai ni matumizi mabaya ya madaraka, kwa kutumia nafasi ambazo ni za kuchaguliwa kwa kura za wananchi wenye itikadi tofauti na wasio na itikadi kwa maslahi ya CCM.

“CUF tunawaomba watanzania kuwa makini na viongozi wa Serikali ambao ni wasanii hususan katika kipindi hiki cha uchaguzi ambapo, hujitokeza kwa ahadi zisizotekelezeka ambazo, ni kiini macho kwa nia ya kuwalaghai watananzania,” alisema Maharagande.

Wakati huohuo Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mahusiano ya Umma wa CUF, Ashura Mustafa alisema kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari jana kwamba, chama chake hakikushangazwa na matokeo mabovu ya kidato cha nne katika shule za sekondari za Kata mkoani Dar es Salaam.

“Haya ni matokeo ya mipango na sera mbovu za CCM na serikali yake kwa kurejesha tena mfumo wa ualimu pasipo na elimu (UPE) katika ngazi ya Sekondari,” alisema katika taarifa yake.

Alisema pamoja na wadau wengi wa elimu nchini, kupigia kelele kuhusu madhara ya shule za sekondari za kata, lakini serikali ya CCM imekaidi na kudai kuwa ni mchakato bila ya kujua kuwa wanafunzi wa shule hizo hawasimami kusoma wanaenda sambamba na shule nyingine zenye ubora wa waalimu na vifaa vya kisasa.

“Pia wanaotunga mitihani hawajali kuwa shule za kata ziko katika mchakato na hazina maabara, maktaba na zina waalimu waliopata mafunzo ya wiki tatu na pia hawakufanya vizuri katika mitihani yao ya kumaliza kidato cha sita,” alisema Mustafa.

“CUF inaitaka serikali ya CCM kuacha kuwahadaa watanzania katika sekta ya elimu ili, kutimiza malengo yao ya kupigiwa kura katika chaguzi mbalimbali kwa kuwajengea shule za kata ambazo, hazina mwelekeo wa kutoa elimu bora kwa watoto masikini wa kitanzania,” alisema.

Fataki atinga bungeni

Salim Said

MBUNGE wa Sumbawanga (CCM), Paul Kimiti jana alizua kicheko kwa wabunge wenzake baada ya kuitaka serikali kuliangalia upya jina la watu wanaowapachika mimba wanafunzi la Fataki, kwa madai kuwa jina hilo ni la babu yake.

Kimiti ambaye ni mmoja kati ya wabunge waliokaa bungeni kwa muda mrefu na mwenye umri mkubwa, alitangaza kuachana na ubunge katika Uchaguzi Mkuu wa ubunge, urais na madiwani unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Kimiti alimuomba Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwantumu Mahiza kuliangalia upya jina hilo kwa sababu huwa anaumia akisikia wanaitwa watu wanaowapachika mimba wanafunzi kwa kuwa ni jina la babu yake.

“Mheshimiwa Spika naomba serikali iliangalie upya jina la Fataki kwa watu hao kwa sababu ni jina la babu yangu,” alisema Kimiti bila ya kufafanua.

Kimiti hakufafanua iwapo babu yake anatumia jina hilo kama la utani au iwapo ni jina lake halisi alilopewa na wazazi wake.

Baada ya mbunge Kimiti kutoa hoja hiyo, Spika wa Bunge Samuel Sitta alihoji kwa utani iwapo babu yake alikuwa Fataki kweli au la.

“Lakini Mheshimiwa Kimiti hakutufafanulia iwapo babu yake alikuwa Fataki kweli au vipi,” alisema Spika Sitta huku wabunge wengine wakiangua kicheko.

Akijibu suala hilo, Mahiza alisema wizara yake itawatafutia jina jingine waharibifu hao ili kuepukana na kumkwaza mbunge Kimiti.

“Mheshimiwa Spika tutawatafutia jina jingine mafataki wa elimu nchini,” alijibu kwa ufupi Mahiza.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), Ananilea Nkya alikiri kuwa jina hilo linaweza kuleta maumivu makali ikiwa ni jina halisi la mtu fulani katika jamii.

“Kwa kweli ikiwa ni jina halisi la mtu ni kweli linaweza kuleta maumivu makali, lakini hii ni changamoto kubwa katika sanaa zetu kuangalia kwanza kama majina tunayoyatumia hayataumiza baadhi ya watu,” alisema Nkya.

“Kwa kweli hata kama ni baba yangu au baba yako ndugu mwandishi usingefurahi kutokana na maana ya jina lile, ungejisikia vibaya hata mimi pia kama ni baba yangu ningejisikia vibaya.”

Hata hivyo, Nkya alisema ni vigumu kwa sasa kulifuta jina hilo katika nyoyo za watu kwa kuwa limeleta athari kubwa na kwamba lina maslahi ya umma.

“Kwa vile jina hili lina maslahi ya umma na limeleta athari sana katika sekta ya elimu, mheshimiwa Kimiti angejaribu kumuelewesha babu yake aone kama vile yeye ni msanii anatumia jina hilo, lakini sio sifa yake kwa sababu kitaaluma na kimaadili huwezi kumnusuru mtu mmoja kwa kuwaumiza wengi,” alisema Nkya.

Fataki ni tangazo lililobuniwa na wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, kitengo cha kuzuia Ukimwi.

Membe: Ama zao ama zetu waliohusika rada

Salim Said

SAKATA la kashfa ya ununuzi wa rada ya kijeshi nchini, limeingia katika sura mpya baada ya serikali kuahidi lazima iwashughulikie watuhumiwa wote waliohusika katika kashfa hiyo, ili kulinda heshma ya nchi katika sura ya kimataifa.

Hivi karibuni kampuni ya BAE Systems inayodaiwa kumlipa dalali zaidi ya Sh12 bilioni kwa kufanikisha kwake serikali ya Tanzania kununua rada ya kijeshi ya Plessey Commander Fighter Control System kwa Sh 40 bilioni, imekiri makosa na kuahidi kurudisha fedha kwa serikali ya Tanzania.

Wiki iliyopita BAE System ilikiri kufanya makosa kwa kulipa rushwa katika mkataba wa kuiuzia serikali ya Tanzania rada hiyo ya kijeshi, chini ya Sheria ya Mikataba ya Makampuni ya mwaka 1985.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Shirika la Utangazaji Tanzania(TBC), mjini Dodoma jana Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alisema lazima serikali isafishe wale wote waliohusika na kashfa hiyo kwa kulinda heshma ya nchi.

Alisema kashfa ya sakata la rada imefikia katika ukingo wake, baada ya BAE System kukiri makosa na kukubali kujisafisha kutokana na makosa hayo.

“BAE imejisafisha, imekiri makosa na imekubali kujisafisha na ule ndio uaminifu, wanakwenda wanafanya uchunguzi, wanagundua udhaifu, wanakiri makosa na wanajisafisha,” alisema Membe.

Membe alifafanua kuwa baada ya BAE System kukubali kujisafisha kwa kuirudishia Tanzania "chenji" yake, kazi kubwa iliyobaki ni kwa serikali kuhakikisha inawashughulikia wahusika.

Alisema, “…..lakini la pili ambalo sihitaji ushauri wala utaalamu kulisemea, ni kwamba safari hii ya sakata la rada imefikia ukingoni, wenzetu wameshajisafisha na sisi hatuna budi kujisafisha katika sura ya dunia,”.

“Kwa hiyo sasa shughuli ni kwetu sisi, mimi nina uhakika kabisa zile nchi zilizoguswa na kashfa hii zitachukuliwa kutoka pale, ili zisafishwe na sisi Watanzania sasa lazima tujiweke sawa tujisafishe katika sura ya kimataifa, yaani katika ngazi ya kimataifa ya nchi zinazoheshimika katika utawala bora,” alisisitiza Membe.

Membe alifafanua kuwa, “Lazima tulifikishe suala hili katika hitimisho lake, yani lazima tujisafishe, tukae vizuri ili tuonekane kwamba mashimo yote ya rushwa yamefukiwa na kama kuna mtu yeyote amehusika katika kashfa hii, hiki ndicho kipindi ambacho, utawala bora wa Tanzania unatakiwa kuimarishwa.”

Membe alisistiza kuwa suala la rada nchini halitopita hivihivi bila ya kuchukuliwa hatua za kisheria ili Tanzania ijionyeshe katika sura ya dunia kwamba inawajibika.

“Suala hili halitoisha hivihivi kwa sababu tumesemwa sana na lazima tujionyeshe katika serikali za dunia na katika uhusiano wa kimataifa kwamba na sisi tuko ‘responsive’ (tunawajibika) kwa maana tunajibu mapigo,” alisema Membe na kusisitiza;

“Kama hili limetokea na tumepata ushahidi, lazima tusafishane humu ndani kwa heshima ya nchi,”.

Juzi Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utawala Bora, Sofia Simba alinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa hadi sasa hakuna taarifa rasmi ambayo serikali imepokea kuhusu sakata la kashfa ya rada, isipokuwa wamekuwa wakisoma katika magazeti na katika mitandao ya kimataifa.

Hata hivyo, aliahidi kuwa, watakaohusika katika kashfa hiyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Katika moja ya ziara zake nchini Uingereza, Rais Jakaya Kikwete aliambia Serikali ya Wingereza kwamba kama kuna fedha imezidi katika ununuzi wa rada anaomba chenji yao.

Membe alisema jana kuwa, hatimaye sasa chenji hiyo inarudi na kwa maana hiyo Tanzania imeula kwa kurudishiwa fedha hiyo takribani paundi 28 milioni kwani miradi mingi itafanikiwa.

“Tanzania tumeula na tunasema Alhamdulillaahi, nilisema na narudia tena kwa vile tunarudishiwa chenji yetu tumeula, miradi yetu itakwenda vizuri, kilimo kwanza kitakwenda vizuri, elimu yetu itakwenda vizuri na masuala mengine yatakwenda vizuri,” alisema Membe.

Wanaotuhumiwa na kashfa ya rada ni Mwanasheria Mkuu wa wakati huo Andrew Chenge, Gavana wa Benki Kuu Tanzania (BoT), Dk Idrisa Rashid na dalali mwenye asili ya Asia, Saileth Vithlani.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba ambaye ni mtu alioongoza wanaharakati katika kufichua sakata la ununuzi wa rada na ndege ya rais tangu wakati wa rais Mkapa, alisema anashangazwa na kigugumizi cha serikali kuchangamkia fedha hizo.

“Nastaajabu sana ufisadi ndani ya nchi hii, nyinyi mmetapeliwa na taarifa zimo katika vyombo vya habari vya uhakika, lakini waziri anaulizwa anasema serikali haijapata taarifa rasmi, si ufuatilie,” alihoji Lipumba.

Alisema kigugumizi cha serikali kwenda kudai fedha hizo kinakuwapo kwa sababu, waliohusika na kashfa hiyo wapo madarakani na hivyo wanaogopa kuwajibika.