MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Monday, October 25, 2010

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Maryam Mwafisi akizindua semina katika Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Kuchoto ni Mkurugenzi wa TEWW Lambertha Mahai na kulia ni Mkurugenzi wa Elimu ya Watu Wazima Salum Mnjagila. Picha na Salim Said
Mkurugenzi wa TEWW Lambertha Mahai na kulia ni Maryam Mwafisi. Picha na Salim Said
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Maryam Mwafisi akizindua semina katika Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Kuchoto ni Mkurugenzi wa TEWW Lambertha Mahai na kulia ni Mkurugenzi wa Elimu ya Watu Wazima Salum Mnjagila. Picha na Salim Said

Sunday, October 24, 2010

HESLB, yachakachua majina ya waombaji wapya wa mikopo

* BAADHI WADAI HAWAONI MAJINA YAO, VYUO VYAO

Salim Said

HOFU na wasiwasi umetanda miongoni mwa wanafunzi wa vyuo mbalimbali nchini, baada ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Tanzania (HESLB), kutangaza orodha ya majina ya vyuo na waombaji waliofanikiwa kupata mikopo, huku majina ya baadhi ya vyuo na waombaji kutoonekana katika orodha hiyo.

Hofu hiyo imekuja kufuatia HESLB kutangaza majina ya baadhi ya vyuo na baadhi ya waombaji waliofanikiwa kupata mkopo huo, huku vyuo vingine na majina ya baadhi ya waombaji kutoonekana.

Taarifa iliyochapishwa katika mtandao wa bodi hiyo, inasema waombaji na vyuo ambavyo majina yao hayapo katika orodha hiyo ya kwanza wanashauriwa kuwa wavumilivu, kwa kuwa kuna orodha nyingine ya majina ya vyuo na waombaji yanayotarajiwa kuchapishwa siku chache zijazo baada ya kumalizika kwa mchakato wa kupanga mikopo hiyo.

Taarifa kutoka ndani ya HESLB waombaji hao wamegawanywa katika makundi mbalimbali na kwamba kundi lililochapishwa katika mtandao wake ni la waombaji 25,000 pekee kati ya zaidi ya 30,000 wanaotarajiwa kupata mkopo huo.

Kutokana na taarifa hiyo, zaidi ya waombaji 5,000 wa mikopo hiyo hawajatangazwa majina yao katika orodha hiyo ya kwanza, iliyopo katika mtandao wa HESLB, huku wakiwa na hofu kuwa ndio wamekosa mkopo.

Baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakipiga simu mara kwa mara katika chumba cha habari cha gazeti hili, wakilalamikia kutoona majina yao katika orodha hiyo iliyochapishwa katika mtandao wa HESLB.

Wakizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam jana, baadhi ya waombaji ambayo majina yao na au ya vyuo vyao hayapo katika orodha hiyo, walisema hadi sasa wako njia panda.

“Kwa kweli sijajua kama nitasoma au sitasoma kwa sababu nilitegemea mkopo wa bodi ya mikopo ya serikali lakini nashangaa jina langu halipo katika orodha iliyowekwa katika mtandao wa bodi hiyo,”alisema Juma Omar ambaye ni mmoja kati ya walioomba mkopo.

Lakini Mkurugenzi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HESLB, Cosmas Mwaisobwa aliwatoa wasiwasi wanafunzi hao kwa kuwaeleza kuwa, majina ya vyuo na waombaji waliyochapishwa katika mtandao wa bodi hiyo ni baadhi tu na kwamba mchakato wa kuchanganua majina hayo bado unaendelea.

“Majina yaliyochapishwa ni baadhi tu ya vyuo na wale walioomba mkopo, mchakato unaendelea na mengine yatachapishwa hivi karibuni,”alisema Mwaisobwa.

Alifafanua kuwa, katika awamu hiyo ya kwanza zaidi ya majina ya waombaji 25,000 yamechapishwa na kwamba mengine yapo katika hatua za mwisho kuchapishwa.

Hata hivyo, Mwaisobwa alisema hakuweza kutaja idadi kamili ya jumla ya watu walioomba mkopo na waliofanikiwa mkopo kw mwaka huu wa masomo wa 2010/11.

“Unajua sina idadi kamili kwa sasa kwa sababu nipo nyumbani lakini nipigie kesho nikiwa ofisini itakupatia idadi kamili,”alisema.

Mkurugenzi huyo wa Habari alilaumu tabia ya baadhi ya waombaji wa mikopo ambao hawajaona majina yao katika orodha ya ‘Means Test’ ya bodi hiyo kutumia njia ya kupiga simu katika vyombo vya habari na kulalamika wakati sio chombo kinachoweza kutatua tatizo lao.

“Mimi nipo ofisini wazi kabisa kila siku, waje pale kama wana tatizo lolote. Sio kuanza kupiga simu katika vyombo vya habari, vitakusaidiaje kwani wao ndio wanatoa mkopo au wanafanya ‘Means Test,” alihoji Mwaisobwa.

Kwa mujibu wa majina yaliyochapishwa katika mtandao wa HESLB, kiwango cha mkopo kinatofautiana kwa wale waliofaulu kinatofautiana kutoka mwombaji mmoja hadi mwengine.

Tarrifa hiyo inaonyesha kuwa, wapo watakaopata mkopo wa asilimia 100 kwa daraja ‘A’ hadi wale wataopata mkopo wa asilimia 10 daraja ‘J’hadi asilimia 0 daraja ‘K’.

Kwa mujibu wa kalenda za vyuo vingi nchini, wanafunzi wanatakiwa kurudi vyuoni kuendelea au kuanza masomo kuazia Novemba 1 mwaka huu, ambapo kufika kwao vyuoni kunategemea sana kufanikiwa au kutangazwa kwa majina yao kwamba yamefanikiwa kupata mkopo.

Utaratibu wa kusoma elimu ya juu kwa njia ya fedha za mkopo kutoka serikalini, ulianza miaka mitano iliyopita baada ya serikali kufuta sera yake ya kutoa elimu ya juu bure sambamba na kuanzisha chombo cha kusimamia utaratibu wa kutoa na kurudisha mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu.

Lakini mfumo huo umekuwa ukikabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na malalamiko, migomo na aminoamano yasiyokwisha kutoka kwa wanafunzi wa taasisi mbalimbali za elimu ya juu, kuhusu mfumo mzima wa utoaji wa mikopo hiyo.

Orodha ya vyuo vilivyofanikiwa ni pamoja na Chuo Kikuu cha Bugando, Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es Salaam na Dodoma (CBE), Community Development Training Institute, College of Engineering and Technology, Chuo cha Elimu Zanzibar, Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), Institute of Accountancy Arusha, Taaisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Taasisi ya Usimamizi wa Fedha (IMF) na Institute of Medicine and Technology University.

Vyengine ni Institute of Rural Development Planning, Taasisi ya Ustawi wa Jamii, chuo kikuu cha Makumira, Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Mbeya, chuo kikuu kishiriki cha Elimu Mkwawa, Moshi University College of Cooperatives and Business Studies, Chuo kikuu cha Mount Meru, chuo kikuu cha Tiba Muhimbili, chuo kikuu cha Waislaam Morogoro, chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Mwenge University College of Education na chuo kikuu cha Mzumbe.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo vyuo vingine ni National Institute of Transport, Ruaha University College, School of Journalism and Mass Communication, Sebastian Kolowa University College, St. Augustine University Tanzania matawi ya Mtwara na Mwanza, St. John’s University of Tanzania kampasi ya Dar es Salaam na Dodoma.

Vingine ni St. Joseph College of Engineering, Chuo Kikuu cha Serikali ya Zanzibar (Suza), Stephano Mosha Memorial University, chuo kikuu cha kilimo cha Sokoine (SUA), Tanzania Institute of Accountancy, Teofilo Kisanji University, chuo kikuu cha Tumaini Dar es Salaam, Iringa na KCMC, chuo kikuu cha Arusha, chuo kikuu cha Dar es Salaam na chuo kikuu cha Dodoma.

Friday, October 22, 2010

ANASWA KWA USHIRIKINA, ADAI KUTUMWA NA MFANYABIASHARA MASHUHRI JIJINI, soma habari kamili chini.....

Shamsa akisikiliza kwa makini maelezo ya mzee Athumani
Mzee Athumani akikabidhiwa kwa polisi wa kituo kidogo cha Gogoni Kiluvya
Mzee Athumani akigoma kutoa panga alililotumia kuchimba chini wakati akifukia vitu vyake


Mzee Athumani akinasihi Shamsa ili akubali kuyamaliza hapo hapo na wasiyafikishe polisi

Picha mbalimbali za tukio hilo

Athuman akionyesha sehemu aliyofukia vitu hivyo
Shamsa akimhoji Athumani kuhusu vitu vya ajabu ajabu ndani ya mfuko mweusi kama unavyoonekana

Anaswa akifukia herizi, ngozi ya kondoo nyumbani kwa mtu




*MWENYEWE ADAI KUTUMWA NA MFANYABIASHARA MASHUHURI JIJINI DAR ES SALAAM

Salim Said

KATIKA hali isiyo ya kawaida mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Athuman Said (53) amekamatwa akifukia vitu vinavyosadikiwa kuwa vya kishirikina huku akiwa na silaha za jadi katika nyumba ya Mkazi wa Kiluvya Gogoni Jijini Dar es Salaam, Shamsa Salum na kudai ametumwa na mfanyabiashara mashuhuri Abdallah Maliki.

Uchunguzi wa Mwandishi umebaini kuwa, Maliki ni mmiliki wa kampuni ya maji safi ya Cool Blue na Matofali ya Tembo zote za jijini Dar es Salaam.

Tukio hilo la aina yake lilitokea juzi saa 4:00 usiku, baada ya mtu huyo aliyedai kuwa ni mkazi wa Kigamboni jijini hapa, kuamua kufunga safari hiyo hadi Kiluvya kutekeleza kazi ya mfanyabiashara huyo ambaye Mwandishi amebaini kuwa ni shemeji wa Shamsa.

Kwa mujibu wa mtu huyo aliyekuwa amevaa bagalashia alidai kuwa alitumwa na Maliki kwa ajili ya kwenda kuomba dua katika eneo hilo ili kumaliza mgogoro katika yake shemeji yake (Shamsa) uliodumu kwa miaka kadhaa.

Said alimwambia mwandishi wa habari hili katika eneo la tukio kuwa, yeye ni mfanyabiashara wa magari kati ya Tanzania na Arabuni, lakini pia huwa anafanya shughuli hizo za kuombea watu dua.

Mtu huyo alikuwa na tasbihi, kitabu chenye maandishi ya lugha ya kiarabu, herizi ambayo alidai kuwa ina ngozi ya kondoo ndani yake na silaha ya jadi aina ya panga, kwa ajili ya kuchimbia chini ya mlango wa nyumba hiyo ili kufukia herizi hiyo.

“Mimi nimeletwa kwa gari na mfanyabiashara huyo hadi hapo kituo cha Gogoni na kuniacha ili nije kumfanyia kazi yake, mimi na Maliki ni marafiki wa muda mrefu,” alisema Said.

Alisema lengo kuu la yeye kwenda hapo lilikuwa ni kumuomba Mungu ili kasi au kumaliza kabisa mgogoro kati ya mfanyabiashara huyo na shemeji yake Shamsa.

Mwandishi alibaini kuwa, kwa miaka kadhaa mfanyabiashara huyo na Shamsa wana mgogoro wa kugombania mali za urithi, baada ya mume wa Shamsa ambaye ni ndugu na mfanyabiashara huyo kufariki dunia.

Utafiti umebaini kuwa mfanyabiashara huyo alishafanya majaribio kadhaa ya kumtoa kwa nguvu Shamsa katika nyumba na eneo ambalo alikuwa akiishi na marehemu mumewe, ambalo analishikilia hadi sasa.

Baaadhi ya majaribio hayo ni pamoja na kutumia vikao vya familia, kwenda mahakamani, kutoa vitisho na kutumia kampuni za udalali kwenda kumtoa kwa nguvu mwanamke huyo katika nyumba.

Lakini majaribio hayo yalishindwa baada ya Mahakama ya Nyumba Wilaya ya Kinondoni kuhukumu Shamsa arudishwe katika nyumba hiyo siku mbili tu baada ya kuhamishwa kwa nguvu na shemeji yake huyo.

Hata hivyo kijana huyo alifikishwa katika kituo Kidogo cha polisi Kiluvya Gogoni saa 5:00 usiku na baadaye kuhamishiwa kituo cha polisi cha Mbezi, ambapo siku yapili alitoka kwa dhamana ya watoto wake.

Wakati huo huo Shamsa alijeruhiwa kwa panga katika mkono wake wakati wa purukushani za kumkamata mtu huyo anayesadikiwa ni mganga wa kienyeji aliyedai kutumwa na mfanyabiashara huyo kusuluhisha mgogoro kwa njia hizo.

Shamsa alidai kuwa, mfanyabiashara huyo ana njama za kumdhuru na kutaka kumuua na kwamba hana amani katika maisha yake kwa kuwa shemeji yake huyo amekuwa akifanya majaribio mbalimbali ya kumdhuru na hilo la kumtuma mganga wa kienyeji ni moja kati ya hayo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni Elias Kalinga alisema hajapata taarifa ya tukio hilo kwa kuwa yeye huzungumzia taarifa za matukio yanayokuwa katika rekodi na kufikishwa mezani kwake.

“Lakini ngoja nitafutilia tukio hilo, nipigie muda mwengine labda nitakuwa nimepata taarifa zake,”aliahidi Kalinga.

Baada ya kupata taarifa za kunasuka kwa jaribio hilo na kwamba taarifa ziko kwa waandishi wa gazeti hili, siku ya pili Mfanyabiashara huyo alimtumia shemeji yake (jina linahifadhiwa) kumtafuta mwandishi ili kuiua habari hiyo kwa madai kuwa, kama itachapishwa itamchafulia jina lake kwa kuwa yeye ni mtu mashuhuri jijini hapa.

“Mimi nimetumwa na (mfanyabiashara huyo) yupo nje ya nchi, lakini tunawasiliana kwa simu nimeomba namba yako kwa mtu mmoja ndio nikapata,” alisema na kuongeza:

“Uhusiano wetu mimi na mfanyabiashara huyo ni kwamba, yeye ana kaka yake baba na mama mmoja anaitwa Salum Mwanamboka ambaye amemuoa dada yangu, kwa hiyo mfanyabiashara huyo ni kama shemeji yangu.”

Hata hivyo mtu huyo kabla ya kukutana na Mwandishi wa habari hii alituma ujumbe mfupi wa maneno uliosomeka, “Kuna ‘issue’ ya huyo mama (Shamsa) juzi aliwachukua waandishi kutoka huko kwa ajili ya kumdhalilisha shemeji yake (mfanyabiashara huyo), ambaye wana ugomvi mahakamani. Tafadhali izuiye.”

Juhudi za kumpata Maliki kujibu tuhuma hizo hazikufanikiwa kwa kuwa simu zake zote za mkononi hazipatikani kila alipopigiwa.