MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Monday, July 20, 2009

ZEC: Wawakilishi walitafsiri vibaya Katiba ya Zanzibar

Salim Said
TUME ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imesema, baraza la Wawakilishi la Zanzibar limetafsiri vibaya Katiba ya Zanzibar katika kutunga sheria namba 7 ya uchaguzi ya mwaka 1984 toleo la mwaka 2004.

Sheria hiyo ambayo imetungwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 toleo la 2003, inapingana na sheria ya Uchguzi ya Zanzibar ya mwaka 2004 katika kufafanua sifa za mzanzibari anayepaswa kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura.
Tatizo hilo limesababisha mkanganyiko mkubwa katika zoezi zima la uandaaji na uboreshaji wa daftari la kudumu la wapikura, ikiwa ni pamoja na baadhi ya wazanzibari kukosa haki zao za kupigakura katika chaguzi mbalimbali visiwani humo.

Akizungumza na waandishi wa habari nje ya kituo namba moja cha uandikishaji wa daftari hilo jimbo la Konde kisiwani Pemba, Mkuugenzi wa ZEC Salim Kassim, alisema licha ya kuwa katiba ya Zanzibar iko juu lakini mzanzibari anaweza kukosa haki ya kupiga kura kutokana na sheria ya uchaguzi.

“Sheria au katiba inaweza kumnyima mtu haki ya kupiga kura bila kujali kwa ni ipi iliyo juu au hdhi zaidi kati ya hivyo,” alisema Kassim.

Alisema, tatizo hilo limesababishwa na Baraza la Wawakilishi kuitafsiri vibaya katiba ya Zanzibar wakati wa kutunga sheria namba 7 ya uchguzi.

“Ni kweli baraza la wawakilishi limetafsiri vibaya katiba ya Zanzibar na ndio maana kuna malalamiko ya hapa na pale katika zoezi hili, lakini hebu jaalia kama vifungu vyote vya sheria vingekwa vimekosewa tungefanyaje kazi? Kwa hiyo tunafanya tu licha ya kuwa kuna hizo kasoro katika tafsiri” alisema Kassim huku akionesha kitabu cha sheria hiyo.

Baaadhi ya wananchi visiwani humo wamekuwa wakilalamika kunyimwa haki zao za kuandikishwa katika daftari hilo kwa kukosa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

Lakini Kifungu namba 7 (1) cha Katiba ya Zanzibar kinasema, kila mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka 18 anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi wa Zanzibar na kwamba haki hiyo itatumiwa kwa kufuata masharti ya kifungu cha pili cha kifungu hiki pamoja na masharti mingine ya katiba hii na ya sheria ya uchaguzi inayotumika Zanzibar.

Kwa mujibu wa katiba hiyo hiyo kifungu kidogo cha pili, baraza la wawakilishi laweza kutunga sheria na kuweka masharti ya kumzuia mzanzibari asitumie haki ya kupiga kura kutoka na oyote kati ya sababu zifuatazo.

“Kuwa na uraia wa uraia nchi mbili, kuwa na ugonjwa uliothibitishwa na mahakama kuu, kutiwa hatiani na kuendelea kutumikia adhabu kwa kosa la jinai isipokua aliewekwa rumande anaweza kuandikshwa,” inaeleza katiba hiyo na kuongeza.

“Kukosa au kushindwa kuthibitisha au kutoa kitambulisho cha umri, uraia au uandikishwaji kama mpiga kura.”

Hata hivyo baadhi ya wananchi wameilalamikia sheria kumzuia mtu kuandikishwa kwa sababu ya kukosa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi wakati katiba ikitak kitambulisho cha uraia.

Wakati katiba ikieleza hayo, sheria namba 7 ya Uchaguzi inapingana na katiba kwa kusema, hakuna mtu ataeandikishwa kuwa mpiga kura ila awe ametimiza masharti ya uandikishaji kama yalivoelezwa katika kifungu cha 7(2) cha katiba, ameonesha kitambulisho cha uzanzibari na kwamba hakuna mtu atakaeandikishwa kuwa mpiga kura katika zaidi ya jimbo au eneo moja la uchaguzi.

Kassim alisema, hawapokei vyeti vya kuzaliwa kama kigezo cha mtu kuandikishwa kwa sababu hata hicho kitambulisho cha ukaazi hakitolewi bila ya kuonesha cheti cha kuzaliwa.

Hata hivyo baadhi ya watu walithibitisha kupata vitambulisho vya ukazi bila ya vyeti vya kuzaliwa na wengine kuonesha vyeti vya kuzaliwa na kunyimwa vitambulisho vya ukaazi.

Aidha, Kassim alisema kati ya wapigakura 8947 walioandikishwa katika Jimbo la Konde mwaka 2005 hadi sasa awamu ya kwanza inaisha wameandikisha watu 582 ambao ni pungufu ya watu 3000.

Kwa mujibu wa Kassim awamu za uboreshaji wa daftari hilo zilipangwa kuwa tatu, lakini kwa sasa zitafanyika mbili tu kwa sababu moja imekufa kutokana na uchaguzi mdogo wa Magogoni uliofanyika mwezi uliopita.

Muhene Said Rashid ni Katibu wa Uchaguzi wa Chama cha Wananchi (CUF) anathibitisha kupokea malamiko ya watu 508 walionyimwa kuandikishwa kwa sababu ya kukosa kitambulisho cha ukaazi.

“Leo ikiwa ni siku ya mwisho katika shehia hizi sita tayari tumepokea malalamiko ya watu 508 kutoandikishw kwa sababu hawana vitambulisho vya uzanzibari mkaazi,” alisema Rashid na kuongeza.

“Cha ajabu kuna mkanganyiko mkubwa kati ya sheria ya uchaguzi na katiba ya Zanzibar . Sheria inapingana na katiba ya Zanzibar jambo ambalo linasababisha wananchi wengi kukosa haki zao za msingi.”

Zoezi hili limekamilika jana katika shehia sita za jimbo la Konde wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba na leo linaendelea katika shehia nyengine za jimbo la Mgogoni kisiwani hapa.

Hofu yatanda kisiwani Pemba

Salim Said, aliyekuwa Pemba
MWELEKEO wa hali ya kisiasa katika kisiwa cha Pemba ni mbaya kufuatia kuanza kwa awamu ya kwanza ya zoezi la uboreshaji wa Dafati la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK) Julai 6 mwaka huu katika Wilaya ya Micheweni kwa kuwaacha bila ya kuwaandikisha baadhi ya wakazi wa kisiwa hicho kwa kutokuwa na vitambulisho vya ukazi.

Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi kwa wiki nzima iliyopita umeonyesha kuwa wananchi kisiwani humo hususan katika mkoa wa Kaskazini karibu obo yao wamekataliwa kujiandikisha hali inayowasababishia hofu kubwa ya kunyimwa haki yao ya kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa 2010.

Awamu ya kwanza ya uboreshaji wa DKWK kisiwani humo imeanza vibaya kufuatia maelfu ya wananchi kukataliwa kusajiliwa katika daftari hilo, huku awamu ya pili na ya mwisho kabla ya uchaguzi mkuu ikitarajiwa kuanza Januari 2010.

Mwanachi ilishuhudia maelfu ya watu waliokataliwa kusajiliwa katika DKWK kwenye vituo 12 vya uboreshaji wa daftari hilo katika majimbo ya Konde na Mgogoni Wilaya ya Micheweni kisiwani humo.

Abdallah Haji ni Wakala wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) katika kituo cha Mgogoni alisema, zoezi hilo ni gumu na kwamba hali ni mbaya sana kwa sababu maelfu ya wananchi wenye sifa wanakataliwa kujiandikisha katika DKWK kila siku.

Hali hiyo ya watu wengi kukataliwa, imesababisha watu kujikusanya katika vikundi vidogovidogo kujadili hatma yao, jambo linalosababisha hofu ya kutokea vurugu na hivyo kuwafanya askari wa vikosi vya kutuliza ghasia (FFU) kuzunguka zunguka kwenye magari yao (Defender) na kupeperusha bendera nyekundu kuashiria hali ya hatari.

Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Mwananchi umegundua kuwa, kituo kimoja cha kujiandikisha kisiwani hapa hulindwa na kati ya askari 10 hadi 15 wenye silaha na wachache wasio na silaha ambao hukaa sehemu za wazi na wengine kujificha kwenye vichaka vilivyozunguka kituo husika.

Askari hao ni pamoja na FFU, usalama wa raia, askari wa usalama barabarani na vikosi mbalimbali vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (KVZ) maafisa wa usalama wa taifa.

Utafiti unaonesha kwa, vyombo vya dola hufanya kazi ambazo sio zao ikiwa ni pamoja kuwaondosha watu katika mistari kwa madai hawana Zan ID au kadi ya mpigakura ya 2005, kuwakataza masheha wa Shehia kuzungumza na waandishi wa habari na kukaa na silaha ndani au mita chache kutoka katika kituo cha uandikishaji.

“Cha ajabu ni kwamba, mwandishi wa habari haruhusiwi kuingia katika kituo, pia hatakiwi kuhojiana na wananchi bila ya kuwa na kitambulisho cha ZEC au akae mita 200 kutoka kituoni, lakini kwa nini askari mwenye silaha anaingia kituoni. Hii ni demokrasia,” alihoji Mwandishi mmoja.

Alisema, lengo la ZEC kuweka masharti hayo ni katika kubana uhuru wa habari, ili yale waliyoyapanga kuyafanya yafanikiwe vizuri, huku wananchi, mashirika ya haki za binadamu na mashirika ya kimataifa yasipate taarifa yoyote.

Salim Hamad Mwijaa ni Afisa wa Usalama wa Taifa kutoka Wilaya ya Michweni, aliomba msaada kutoka kwa mabosi wake baada ya waandishi wa habari kuanza kuchukua malalamiko kutoka kwa wananchi katika kituo cha Mgogoni.

“Naona bosi hapatikani kwenye simu zake zote mbili, naomba msaada wenu kwa sababu hapa kuna watu hawana vitambulisho vya ZEC na wanachukua maelezo kwa wananchi hali imebadilika na imekuwa ya vurugu. Naomba msaada haraka,” alisema Mwijaa.

Baada ya muda mfupi lilitokea gari la polisi (Defender) likiwa na askari wa FFU waliobeba silaha za moto na kupeperusha bendera nyekundu lakini bila ya hata kusimama na kufanya chochote lilizunguka katika uwanja wa kituo hicho na kurudia lilikotoka.

Aidha, Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi (Zan ID), kadi ya mpiga kura katika uchaguzi uliopita vinatumika kuwakwamisha wananchi kuandikishwa katika daftari hilo.

Pia Masheha wamekuwa wakitumika kukwamisha zoezi la uboreshajiwa Daftari hilo kwa kutotoa fomu za kuombea Zan ID na barua za wananchi kupotelewa na mali zao ili kwenda polisi kwa msaada zaidi.

Mashehao ambao ni watendaji wa chini katika mtiririko wa uongozi wa SMZ huteuliwa na kuapishwa na Wakuu wa Mikoa, huamua kufunga ofisi zao bila ya kuweka msaidizi wanapotumiwa na ZEC kwa uwakala.

Khatib Hassan (27) mkaazi wa Wingwi Mjananza aliesema, kila anapofika kwa Sheha kutaka huduma huambiwa yuko katika uboreshaji wa DKWK na akimfuata jioni hujibiwa na Sheha huyo kwamba bendera imeshushwa na muda wa kazi umeisha.

“Mchana haonekani anakuwa ni mfanyakazi wa tume, lakini ukimfuata jioni anasema, bendera imeshushwa na muda wake wa kufanya kazi umeisha hivya mpaka siku ya pili na siku ya pili ukienda majibu ni hay ohayo,” alisema Hassan.

Sambamba na hilo la kufungwa kwa ofisi nyingi za Masheha, pia wapo baadhi ya Masheha wanaowatangazia wananchi kuwa serikali imesitisha utoaji wa fomu za kuombea Zan ID na hata Vitambulisho vyenyewe vya Mzanzibari Mkaazi hadi hapo awamu ya kwanza ya zoezi hilo itakapomalizika.

Hata hivyo Mkurugenzi wa ZEC Salim Kassim na Mkurugenzi wa Idara ya Zan ID Mohammed Ame walikataa malalamiko hayo lakini Ame alisema atafuatilia ili kujua ukweli wa hali hiyo.

Maafisa Usalama wawatimua wananchi katika vituo vya uandikishaji

Salim Said, Pemba
ZOEZI la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika Jimbo la Mgogoni Wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba limeingia dosari katika siku yake ya kwanza, baada ya maamia ya wananchi kutimuliwa katika baadhi ya vituo vya uandikishaji na maafisa Usalama na hivyo kukosa kujiandikisha.

Wananchi hao kutoka vituo vya Kinyasini, Finya na Wingwi Mapofu waliofika katika vituo hivyo na kupanga foleni mapema jana asubuhi, walijikuta wakitimuliwa vituoni na maafisa hao kwa kuwa hawana vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi (Zan Id).

Maafisa hao waliwambia wananchi hao kwamba hawapaswi kuonekana katika vituo hivyo kwa sababu hawana Zan ID.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa hasira huku wakionekana kuchoka nje ya baadhi ya vituo, baadhi ya wananchi walisema maofisa wa usalama waliokuwa wamekaa karibu na maeneo hayo waliwataka waondoke mara moja vituoni hapo.

Katika kituo cha Wingwi Mapofu walionekana maofisa wa usalama waliokuwa wamekaa katika baraza za jengo la kituo hcho wakitoa maelekezo kwa watendaji wa tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).

“Ukifika pale kituoni unaambiwa uondoke na maafisa usalama kwa sababu huna Zan ID, hii ni haki kweli? Mimi nina cheti cha kuzaliwa, kipande cha kupigia ktika uchaguzi mkuu wa 2005, na uchaguzi mdogo wa mwaka 2003 (kura za maruhani),” alisema Khatib Hassan (27).

Hassan alilalamika kuwa, anapokwenda kwa Sheha ambaye anapaswa kutoa fomu za kuombea Zan ID anaambiwa aende Wilayani na akifika Wilayani hutakiwa kurudi kwa sheha.

”Ukieda kwa Sheha anakwambia nenda Wilayani na ukienda Wilayani unaambiwa nenda kwa Sheha. Wametufanya kama mpira wa kona Sheha apiga chenga wilaya yafunga goli. Wanatunyima haki zetu hivi hivi,” alilalamika Hassan.

Naye Mbarouk Rubea (48) alisema, ana sifa zote za kuandikishwa kuwa mpigakura kwa mujibu wa katiba ya zanzibar lakini hadi sasa anahangaishwa hajapata kitambulisho na hatimaye amenyimwa kujiandikisha katika daftari hilo.

Akiwa amesawajika na mtoto mgongoni Rehema Khamis (32) alisema, ameanza kukata tamaa ya kupiga kura katika uchaguzi ujao kwa sababu hajapatiwa kitambulisho hadi licha ya kuwa ameshalipa sh 500 za Zan ID.

”Hivi sasa nakaribia kulia mana nimeacha kwenda kuvuna mpunga wangu nikaamua kuja huku lakini nahangaishwa tu na mtoto mgongoni. Nanyimwa haki yangu na maofisa wa usalama wanatufukuza hapa,” alisema Rehema.

Hata hivyo, maofisa wa usalama waliokuwa vituoni hapo na kutuhumiwa kuwatimuwa wananchi wasiokuwa na Zan ID walikataa kuzungumza na waandishi wa habari na kuwapiga marufuku watendaji wa tume kufanya hivyo.

Sheha wa Shehia ya Mjananza Hamad Said, ambaye pia ni wakala wa ZEC alikatazwa na maafisa wa Usalama kuzungumza na waandishi wa habari waliofika kituoni hapo.

Waandishi waliwaomba mmoja wa askari wa usalama wa raia waliokuwapo kituoni hapo kumuita sheha huyo ili kuzungumza naye, lakini alipotoka na kusalamiana na waandishi ghafla aliitwa na maofisa wa usalama na kuagizwa kutozungumza na waandishi hao.

”Nimekatazwa na wale pale nisiongee na ninyi,” alisema Said huku akiwaandalia maofisa hao na kuingia katika kituo cha uandikishaji.

Aidha katika vituo hivyo, vilikuwa na ulinzi mkali wa dola wakiwamo askari polisi wa usalama wa raia, askari wa kutuliza ghasia wenye silaha (FFU), askari wa vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanibar (SMZ) na usalama wa taifa.

Mwananchi ilibaini kuwa, wananchi wengi kisiwani Pemba hawana Zan ID hususan wale waliotimiza miak 18 na wale waliokuwa nje ya zanzibar kwa muda kidogo.

Hiyo ni kutokana na sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar kuagiza kwamba mtu yeyote hapaswi kupewa kitambulisho cha ukaazi bila ya kufikia umri wa miaka 18.

Aidha, Mwananchi ilishuhudia mamia ya wananchi wakiondoka katika vituo huku wakilalamikia maafisa wa tume ya uchaguzi, serikali na Chama cha Mapinduzi kwa kuwanyima haki zao.

”Hivi kwani hawa watu wa tume ya uchaguzi wamekuja kufanya nini hapa, mana kama ni kuandikisha hawatuandikishi,” alihoji bwana mmoja kwa hasira.

Katika vituo vitatu ambavyo waandishi walitembelea, waligundua mamia ya wananchi kunyimwa haki hiyo kwa kukosa Zan ID huku wakiwa wamekaa katika vikundi vidogo vidogo ili kujadiliana.

Mwnyekiti wa Halmshauri ya Wilaya ya Micheweni Abdallah Ali Said alithibitisha kupokea malalamiko hayo katika siku ya kwanza ya zoezi hilo kwenye jimbo la Mgogoni kisiwani hapa.

Masheha wakwamisha daftari la wapigakura

Salim Said, Pemba
MASHEHA wa Shehia za Wilaya ya Micheweni mkoa wa Kaskazini Pemba wameshutumiwa kukwamisha awamu ya kwanza ya zoezi zima la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura katika wilaya hiyo, kwa kuwanyima wananchi huduma katika ofisi zao.

Masheha ambao pia ni mawakala wa ZEC ni watendaji wa serikali katika ngazi ya Shehia ambayo ndio ngazi za chini kiutawala katika Serikali ya Zanzibar (SMZ) kwa kawaida huteuliwa na kuapishwa Wakuu wa Mikoa pindi wanapoteuliwa na rais baada kuingia madarakani.

Aidha malalamiko dhidi ya Masheha yalijitokeza katika vituo vyote sita vya vya jimbo la Mgogoni na baadhi ya shehia za jmbo la Konde Wilaya ya Micheweni kisiwani hapa.

Malalamiko hayo, ni ya kutowapatia wananchi fomu za kupatia vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi (Zan ID), fomu za uthibitisho wa kukataliwa kuandikishwa katika daftari hilo (2KK) na barua za kuthibitisha kupotelewa na vitambulisho vyao.

Kwa mujibu wa sheria ya Zanzibar mtu yeyote anayepotelewa na mali yake hupaswa kuripoti Polisi ambapo Polisi huwa haitoi barua hadi mlalamikaji huyo anapopata barua ya Sheha kuthibitisha kuwa aliyepotelewa ni mkaazi wa eneo lake.

Wakizungumza na Waandishi nje ya vituo tofauti vya kuandikishia wapiga kura, baadhi ya wananchi walisema Masheha ndio kikwazo kikubwa cha zoezi hilo .

Said Salim (22) wa Shehia ya Mgogoni alisema, tangu mwaka 2005 amekuwa akienda kwa Sheha kuomba fomu ya kombea Zan ID lakini hadi hii leo hajapata fomu hiyo.

“Mwaka 2005 nilienda kwa Sheha kuomba fomu akaniambia sipati, nikakaa mwaka jana nilienda tena akaniambia sipati, nikampelekea na hata cheti cha kuzaliwa lakini hadi hivi sasa ninavyozungumza sijapatiwa fomu hiyo,” alisema Salim na kuongeza.

“Sisi tunaenda vituoni tunakataliwa kujiandikisha lakini hatuwezi kwenda mahakamani kwa sababu hatuna ushahidi na ili tuwe na ushahidi ni lazima tupate fomu za 2KK ambazo masheha wamegoma kabisa kutupatia. Huu ni mkakati.”

Khatib Haasan (27), wa kituo cha Wingwi Mapofu alisema wamekuwa wakizungushwa kati ya ofisi ya sheha na Ofisi ya Vitambulisho wakati wa kutafuta fomu za kuombea Zan ID.

”Mimi nina cheti cha kuzaliwa, kipande cha kupigia ktika uchaguzi mkuu wa 2005, na uchaguzi mdogo wa mwaka 2003 lakini hadi sasa sijapewa Zan ID licha ya kufanya juhudi kubwa kukitafuta,” alisema Hassan.

Baadhi ya Masheha walioingizwa moja kwa moja katika tuhuma hizo ni Omar Khamis Faki (Kifundi), Said Hamad Ali (Mjananza), Mohammed Omar (Konde) na Said Hamad Khamis (Mgogoni).

Lakini waandishi wa habari walishindwa kuzungumza na masheha hao kutokana na Maafisa wa Usalama wa Taifa kuwakataza watendaji hao wa SMZ kuzungumza na mwandishi yeyote.

“Mimi nimekatazwa na mabosi wangu kuzungumza chochote na mtu nisiyemjua,” alisema Khamis ambaye ni Sheha wa Mgogoni baada ya kuashiriwa kuingia ndani ya kituo na Afisa wa Usalama aliyekuwapo.

Kwa mujibu wa wananchi wanapofika kwa Sheha ofisi huwa imefungwa wakati wa mchana na wakienda jioni au usiku huwajubu kuwa bendera imeshushwa kwenye mlingoti na muda wa kazi umeisha.

Mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Salim Hamad Mwijaa alisema kuwa yeye ni Afisa wa Usalama wa Taifa kutoka ofisa ya Wilaya ya Micheweni alimkataza sheha wa Mgogoni kuzungumza na waandishi.

“Haloo, mbona namba ya bosi siipati? Maana hapa kumekuja watu hawana vitambulisho vya tume na wanachukua maelezo kutoka kwa wananchi hapa. Tunaomba msaada wenu,” alisikika Afisa huyo wa usalama akiongea kwa nji ya simu.

Aidha baada ya muda mfupi sana lilitokea Gari la Polisi aina ya Difender huku likipeperusha bendera nyekundu juu na askari wa kutuliza ghasia wenye silaha na kuzunguka katika uwanja wa mpira wa kituo cha Mgogoni na kurudi lilikotokea.

Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Salim Kassim alithibitisha kupokea malalamiko ya Masheha kutotoa barua na fomu hizo na kuongeza kwamba jambo hilo linakoroga kazi ya uboreshaji wa daftari hilo katika awamu ya kwanza.

”Masheha wantukoroga hasa sheha wa Kifundi kwa sababu hawatoi fomu za Zan ID na barua za kwa wananchi waliopotelewa na vitambulisho vyao,” alisema Kassim na kuahidi kulifuatilia tatizo hilo.

Kassim pia alisema, jambo hilo la kufuatilia ukorofi wa masheha ni msaada wao wanaoutoa kwa wananchi hao kwa sababu ZEC wala yeye hatoi vitambulisho vya ukaazi.

”Sisi ni msaada tu huu lakini ZEC wala mimi sitoi Zan ID wanaohusika ni serikali yaani ofisi ya vitambulisho,” alisema Kassim.

Baadhi ya Wananchi walijaza fomu za vitambulisho na kulipia ada ya sh500 na kupatiwa stakabadhi zao lakini hadi sasa hawajapatiwa vitambulisho hivyo kwa sababu tofauti zinazotolewa na ofisi ya Zan ID wilaya ya Micheweni.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Abdallah Ali Said alithibitisha kuwepo kwa hali hiyo ambapo pia aliwaonesha waandishi wa habari stakabadhi kadhaa za watu waliolipa mwaka 2005 na 2006 lakini hadi sasa hawajapatiwa Zan ID.

“Unaona hawa ni watu 10 katika Shehia ya Wingwi Mjananza wamelipia ada ya Zan ID tangu mwaka 2005 na 2006 lakini hadi hii leo hawajapatiwa vitambulisho. Wanazungushwa tu wakienda wialyani wanarudishwa kwa sheha na sheha hatoi vitambulisho. Nimejaribu kuwasiliana na Mkuu wa Mkoa na Kaskazini na Mkuu wa Wilaya ya Micheweni lakini hakuna jibu,” alisema Said.

Hata hivyo, Mkuu wa Idara ya Vitambulisho wilaya ya Micheweni Hamad Shamata alikataa kujibu tuhuma hizo kwa madai kwamba kuna maelekezo maalumu waliyopewa.

“Aaah.. sisi tuna maelekezo maalumu tuliyopewa naa... naa….,” alisita kidogo na kuongeza: ” Kama ninyi ni waandishi mtafuteni Mkurugenzi wa Idara ya Zan ID.”

Hata hivyo juhudi za kumpata Mkurugenzi wa Idara ya Zan ID Zanzibar Mohammed Ame hazikufanikiwa baada ya simu yake ya mkononi kutokuwa hewani kila alipopigiwa.

Zaidi ya watu 2500 wamekataliwa kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura katika Jimbo la Konde na Mgogoni wilaya ya Micheweni kisiwani hapa kwa sababu ya kukosa Zan ID. Zoezi hili linaingia katika siku ya tatu leo katika Jimbo la Mgogoni baada ya kukamilika katika jimbo la Konde hapo juzi.

Hali tete kisiwani Pemba

Salim Said, Pemba
ZOEZI la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura katika Wilaya ya Micheweni limezidi kuzorota katika siku yake ya tisa jana, baada ya baadhi ya wananchi kukataliwa kuandikishwa katika daftari hilo licha ya kuonesha kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi (Zan ID).
Wananchi hao ambao wengi wao wana Zan ID lakini hawana kadi ya mpiga kura ya mwaka 2005 wameonekana katika vituo mbalimbali vya uandikishaji wa daftari hilo kisiwani Pemba .

Awali kikwazo kikubwa cha wananchi wengi ilikuwa ni Zan ID lakini, jana watu wengi walishindwa kupata kuandikishwa katika daftari hilo kwa sababu ya kupoteza kadi ya mpiga kura ya mwaka 2005.

Wakizungumza na waandishi wa habari nje ya vituo mbalimbali vya uandikishaji wananchi hao walisema, imeonekana wazi kuwa kuna mkakati maalum wa kuwanyima haki yao ya kupiga kura.
Salim Khalfan Said (23) mkaazi wa Finya jimbo la Mgogoni alisema, licha ya kuwa na Zan ID lakini amenyimwa kuandikishwa katika daftari hilo .

“Mimi ninayo Zan ID lakini nimekataliwa kujiandikisha kwa sababu sina kadi ya mpiga kura ya mwaka 2005, na hata jina langu hawakutaka kuliangalia katika daftari kwa sababu naamini limo labda walitoe hivi sasa,” alisema Said na kuongeza:

”Mimi kadi yangu ya mpigakura imepotea lakini mwaka 2005 nilipiga kura hapa hadi chumba nilichopigia kura nakikumbuka nilimpigia babu yangu kwanza halafu nikapiga na mimi, leo wanasema sionekani kwenye daftari.”

Said alionesha kitambulisho chake cha Mzanzibari Mkaazi (Zan ID) ambacho kilionesha kuwa kinapitiwa na muda wake miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tume ya uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Salim Kassim alisema, ili mtu aweze kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapigakura ni lazima awe na Zan ID.

“Huwezi kuwa na simu bila ya kuwa na kadi ya simu (line) hivyo huwezi pia kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapigakura kama huna Zan ID,” alisema Kassim.

Kassim alikanusha taarifa za kuwa kuna baadhi ya wananchi wanaandikishwa katika daftari hilo kwa sababu ni wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) bila ya kuonesha Zan ID kama kigezo kikubwa cha ZEC.

“Habari hizo si za kweli, na naweza kusimama mahali popote kuyasema haya, lakini kama umemuona mtu aliyeandikishwa bila ya Zan ID na kutumia kigezo cha itikadi ya chama chake basi niletee stakabadhi yake,” alisema Kassim na kusisitiza:

“Hizo habari ni za uongo, uzushi na za kupotosha, na nakuomba usiandike habari hizo, hao ni waongo na ukiandika nakwambia nitakushtaki.”

Wakati Kassim akisisitiza hayo Mwananchi ilishuhudia kijana Salim Khalfani (23) akikataliwa kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura katika kituo cha Finya jimbo la Mgogoni licha ya kuonesha Zan ID.

Wakati kijana huyo akikataliwa kuingia katika daftari hilo, kijana mwengine Assaa Ismail Nassor (25) mkaazi wa Mtemani Wingwi alisema, yeye amekataliwa kuingia katika daftari hilo kwa sababu ni mwanacham wa Chama cha Wananchi (CUF), wakati mdogo wake ambaye ni mwanachama wa CCM alikubaliwa bila ya kuwa na Zan ID.

“Mimi nimekataliwa kuingia katika daftari la kudumu la wapiga kura na ninayo kadi ya mwaka 2005, lakini mdogo wangu amekubaliwa wakati hana chochote. Sijui hata kama umri wa miaka 18 ametimiza, lakini kwa sababu yeye ni CCM lakini amekubaliwa,” alisema Nassor.

Aidha Mwananchi ilishuhudia mamia ya wananchi wakiwa wamekaa nje ya vituo katika vikundi vidogo vidogo wakijadiliana baada ya kukataliwa kuingia katika daftari hilo .

Wakati huohuo baadhi ya wazee wamelalamika kuwa kigezo cha kuonesha cheti cha kuzaliwa ili upate Zan ID si sahihi kwa sababu kimelenga kuwakatisha tamaa.

Juma Kombo Ali (56) alisema, “ikiwa mzee kama mimi unanidai kitambulisho wakati barua ya sheha ninayo, unakusudia nini kama si kunikwamisha ili nikate tamaa.”

”Huyo sheha mwenyewe wala baba yake hana cheti cha kuzaliwa kwa sababu vyeti hasa vimeanza baada ya Mapinduzi, lakini cha ajabu wanadai vyeti hivyo,” aliongeza Ali.

Alisema, zaidi ya watu 2000 hawajaandikishwa kwa sababu hawana Zan ID na kuhoji kwamba watapiga wapi kura za kumchagua rais wa Muungano na Wabunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
”Je hawa watapiga wapi kura za Muungano, maana si watanzania hawa wala si wazanzibari, basi tunaiomba serikali iwatafutie nchi iwapeleke kama ni Kenya, Uganda au Marekani kwa Obama huko watapewa haki zao,” alisema.

Awamu hii ya kwanza ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura katika majimbo ya wilaya ya Micheweni inaendelea huku kukiwa na malalamiko mengi kuhusu watendaji na Mawakala wa ZEC ambao ni pamoja na Masheha.

Masheikh waionya serikali

Salim Said
SIKU moja baada ya serikali kuutua mzigo wa mahakama ya Kadhi kwa Waislaam, viongozi wa dini ya hiyo wamepinga vikali uamuzi huo na kusema kama serikali inaona gharama kutumia fedha kudumisha amani iliyopo, itakuja kutumia fedha hizo kuitafuta amani hiyo baada ya kutoweka.

Akizungumza Bungeni juzi Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema, waislaam ruksa kuanzisha mahalama ya Kadhi lakini kwa sharti iwe nje ya dola na Katiba ya nchi.

Wakizungumza mara baada ya Swala ya Ijumaa katika Msikiti wa Kituo cha Kiislaam (TIC) Magomeni jijini Dar es Salaam jana Masheikh mbalimbali walisema hawakubaliani na kauli hiyo ya Waziri Mkuu kwa sababu bado haijawatendea haki waislaam nchini.

Amir wa Shura ya Maimamu Tanzania Sheikh Mussa Kundecha alisema, kauli ya Waziri Mkuu ni ya kisiasa na kwamba kama serikali inaona gharama ndogo kwa kutumia fedha kulinda na kudumisha amani ya nchi, itakuja kutumia gharama kubwa zaidi kuitafuta baada ya kutoweka.

“Kauli hii bado haijawapatia waislaam majibu sahihi ya hoja yao na ni yakisiasa zaidi, mambo ya kuwambia waislaam haya fanyeni nje ya dola na katiba hatukubaliani nayo. Lakini kwa nini serikali inaona tabu kutumia gharama kudumisha amani? Matokeo yake itakuja kutumia fedha nyingi kutafuta amani baada ya kutoweka,” alisema sheikh Kundecha.

Alisema, msimamo wa waislaam ni kwamba Mahakama ya Kadhi lazima iwepo na ipewe hadhi ya kisheria na kikatiba ikiwa ni pamoja na kusimamiwa na kugharamiwa serikali ya Tanzania.

“Mahakama ya kadhi lazima iwepo na lazima igharamiwe na serikali na ipewe hadhi ya kikatiba na kisheria nchini. Kuinyima hadhi ya kikatiba na kisheria ni sawa na kuikataa,” alisema Sheilh Kundecha na kusisitiza:

“Mambo ya kusema serikali haipingi mahakama ya kadhi lakini iundwe nje ya dola, ni kama mambo mengi ambayo serikali inajidai imeyakubali lakini haijayakubali yakiwamo ya mirathi, talaka na ndoa za kiislaam.”

Alizungumza huku akitoa mifano Sheikh Kundecha alisema, siku zote yanapokuja mambo yanayowahusu waislaam, serikali hufanya ujanja ujanja na ubabaishaji kwa lengo la kuwanyima haki zao.

“Serikali inawajibika kugharamia mahaka ya kadhi kama inavyowajibika kugharamia taasisi za madhehebu au dini nyingine nchini kwa sababu jambo hili linawahusu walipa kodi ya Tanzania na wala si wa nje ya nchi,” alisema.

Alihoji kuwa, kodi za nchi hii zinalipwa na watanzania wote wakiwamo waislaam, wakristo na dini nyingine lakini kwa upande mmoja taasisi zao zigharamiwe na serikali halafu upande mwengine ukataliwe.

“Serikali katika tangazo la wazi kabisa imetangaza kulipa mishahara ya hospitali inayomilikiwa na taasisi ya dini ya CCBRT na imeipandisha hadi kuwa ya mkoa. Si hilo tu bali imetenga eneo na kuahidi kugharamia ujenzi ili kuipanua, kwa nini waislaamu wasigharamiwe vya kwao,” alihoji sheikh Kundecha.

“Kuna memorandum of understanding na ubalozi wa Holy Sea wala si wa Vatican, vyote hivi vinagharamiwa na serikali. Wakrsto wana vingapi vinagharamiwa na serikali? Halafu inaonekana upande mmoja unafanya kazi zaidi kuliko mwengine kumbe wanagharamiwa,” aliongeza.

Alisema, msimamo wa waislaam mahakama ya kadhi iwepo na serikali isimamie na kugharamia ila uteuzi wa kadhi na utendaji wa mahaka hiyo liwe jukumu la waislaam.

Naye Imamu wa Msikiti wa Riyaadha wa Mjini Arusha sheikh Shaaban Juma alisema, serikali ya Tanzania ni serikali ya amani hivyo inapaswa kuhakikisha kuwa amani hiyo inaendelea kwa kuwapa waislaam haki yao.

“Tangu rais wa kwanza, wa pili, wa tatu na huyu wa nne tunadai mahakama ya kadhi hatujaipata, hivyo tukinyimwa tutakasirika sisi na tukikasirika amani itatoweka,” alisema sheikh Juma na kuhoji:

“Hivi hii serikali ya amani imeichoka hii amani? Kutunyima mahakama ya kadhi kwa kutumia lugha za ubabaishaji kama hii ya Pinda ni sawa kutudhulumu, ukiibiwa fedha umedhulumiwa na ukinyimwa haki yako ya kidini pia umedhulumiwa na Allah awalaani wote wanaoendesha dhulma hii,” aliongeza sheikh Juma huku waislaam wakimjibu, “aammiiin.”

Kwa upande wake sheikh Hussein Hashim kutoka Tanga alisema, kauli ya Pinda ni ya ubabaishaji lakini waislaam hawatokubali tena kubabaishwa.

“Mahakama ya kadhi lazima iwepo na tena iwe chini ya dola,” alisema sheikh Hashim huku akinukuu baadhi ya aya za Kur-an na Hadithi za Mtume Muhammad (S.A.W) kukazia hoja yake.
Mwisho.

Mbunge: ZEC yaanza kutupunguzia kura zetu za urais Pemba

Salim Said, aliyekuwa Pemba
MBUNGE viti maalum Wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba (CUF), Mgeni Jadi Kadika amesema, vikwazo wanavyowekewa wananchi katika shughuli ya kuboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura (DKW) kisiwani hapa ni mkakati wa ZEC wa kupunguza kura za wapinzani katika uchaguzi mkuu wa 2010.


Shughuli hiyo, ilianza Julai 6, mwaka huu katika awamu ya kwanza na watu 7,000 wamekatalwia kujisajili katika daftari hilo.

Akizungumza na Mwananchi kisiwani hapa mwishoni mwa wiki, Kadika alisema baada ya Chama cha Mapinduzi (CCM) visiwani Zanzibar kuona kuwa hawana ubavu wa kuchukua Jimbo la Pemba, wameamua kupunguza kura za urais za mgombea wa Chama cha upinzani.

“Jimbo la Pemba, CCM hawapati, lakini wanachofanya sasa ni kupanga mikakati mbalimbali kwa kuunda utatu usio mtakatifu ambao ni wa ZEC, Idara ya Zan ID na Masheha ili kutupunguzia kura zetu za urais.

“Maana kama utawahesabu wanachama wa CCM katika majimbo ya Wilaya yangu, basi utapata 500 tena ukijumlisha mpaka watoto wanaonyonya ndio wanafikia idadi hiyo,” alisema.

Akitoa mfano, alisema Jimbo la Mgogoni kisiwani hapa, Kadika alisema katika uchaguzi wa mwaka 2005 idadi ya wananchi walioandikishwa walikuwa zaidi ya 7,000, lakini baada ya kumalizika kwa shughuli ya kuboresha DKW katika jimbo hilo, ni watu 4,300 tu waliosajiliwa.

“Kwa hiyo hapa utaona kuna zaidi ya kura zetu 3,000 zimekatwa katika jimbo moja tu, wakati sisi tulikuwa na matarajio ya kuongezeka kwa watu hadi kufikia 9,000 au 10,000. Hivi tuseme sisi huku kwetu hatuongezeki tunapungua tu tena kwa kasi yote hiyo.


“Wakishafanikiwa hapa, basi wataruhusu mawakala hadi kwenye vyumba vyao vya kulala, lakini wanajua kuwa wameshajihakikishia ushindi kwa njia hiyo. Halafu utasikia uchaguzi ulikuwa huru na haki, hakuna nguvu iliyotumika kumbe mchezo ulishachezwa zamani.” alisema.

Mkurugenzi wa Idara ya Zan ID Zanzibar Mohammed Ame alisema kazi ya kutoa vitambulisho vya Zan ID, halijasitishwa na kwamba hajapata malalamiko yoyote kuhusu shughuli hiyo.

“Hatujasitisha utoaji wa Zan ID, tunaendelea kutoa kila siku na watu wote wenye sifa na vigezo vya kupata basi wanapewa. Sijapata malalamiko yoyote kutoka kisiwani Pemba, lakini kama kuna hali hiyo basi nitafuatilia,” alisema Ame.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa ZEC Salim Kassim alisema, kasoro zinazojitokeza katika uboreshaji wa DKW kisiwani Pemba hazitaathiri uchaguzi mkuu wa 2010 na kwamba utakuwa huru na wa haki.