MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Wednesday, October 7, 2009

Lipumba:Kikwete anapaswa kubeba msalaba wa Richmond

Salim Said, Mtwara
MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba, amesema Rais Kikwete Jakaya Kikwete, anapaswa kubeba msalaba kuhusu Kampuni feki ya Richmond, iliyopewa zabuni ya mradi wa kufua umeme wa dharura.

Profesa Lipumba aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia katika uzinduzi wa operesheni zinduka katika Kanda ya Kusini, iliyofanyika katika Uwanja wa Mashujaa mjini Mtwara,

Alisema Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri, hawezi kukwepa lawama kuhusu zabuni hiyo, iliyoisababishia kashfa serikali yake.

Alisema, maamuzi ya kusainiwa kwa mkataba wa zabuni ya kufua umeme wa dharura kwa Kampuni ya Richmond yalifanywa na Kikwete na kwamba kwa msingi huo, yeye ni mtuhumiwa namba moja katika suala hilo.

“Mtuhumiwa na mshitakiwa namba moja wa kashfa ya Richmond ni Rais Kikwete kwa sababu maamuzi ya kuingia zabuni hiyo yalifanywa na yeye,” alisema Profesa Lipumba.

“Kwa sababu hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kutengua au kubariki maamuzi ya baraza la mawaziri, isipokuwa rais, yeye ndiye mhusika nambari moja na anayepaswa kubeba msalaba wa Richmond," alisisitiza kiongozi huyo wa CUF.

Profesa Lipumba alielezea kusikitishwa kwake juu hatua ya Katibu Mkuu Kiongozi (Luhanjo), ya kuwasaliti na kuwafanya Watanzania kuwa ni watu wasio na akili hasa baada ya kujitokeza na kudai kuwa Rais Kikwete, hahusiki na Richmond.

“Luhanjo anayajua yote kuanzia mchakato hadi kusainiwa kwa zabuni ya kufua umeme wa dharura kwa kampuni ya mkobani ambayo haina hata uwezo wa kuunganisha waya kwenye nyumba. Leo anawadanganya Watanzania,"alisema Profesa Lipumba.

Alidai kuwa hatua hiyo inadhihirisha kuwa CCM wote ni mafisadi na ndiyo maana wameamua kuficha ufisadi na kuwasaliti Watanzania, waliowaweka madarakani.

“Ndugu zangu kiongozi aliyeingia madarakani kwa ufisadi hawezi kupambana na ufisadi hata kidogo. Rais Kikwete si mpambanaji wa ufisadi,” alisema Lipumba.

Alielezea kushangazwa kwake na kauli za baadhi ya viongozi wa CCM kwamba ufisadi umekithiri lakini bila kumhusisha Rais Kikwete ambaye alidai kuwa naye anayendesha ufisadi.

“Kama kweli ni wazalendo na wana nia ya dhati ya kupambana wamtaje, Rais Kikwete na wawambie Watanzania wasimchaguwe katika uchaguzi wa mwaka 2010," alisisitiza.

Alisema Tanzania ina uongozi dhaifu wa rais Kikwete na kwamba hata wanamtandao walimkubali kwa tamaa ya kupata madaraka tu.

Chadema wataka ufisadi wa UBT uanikwe

Salim Said
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeitaka serikali kuianika hadharani ripoti ya Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu ufisadi ndani ya stendi ya kuu ya mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani ya Ubungo (UBT) pamoja na kuiwajibisha familia ya Kingunge Ngombale Mwiru inayodaiwa kuendesha ufisadi katika stendi hiyo.

Miezi michache iliyopita Waziri Mkuu Mizengo Pinda alifanya ziara ya kikazi jijini la Dar es Salaam na kugundua harufu ya ufisadi UBT ambapo alimuagiza CAG kufanya ukaguzi katika stendi hiyo.

Akifungua mkutano mkuu wa jimbo la Ubungo (Chadema) katika ukumbi wa mikutano wa Urafiki Dar es Salaam jana, mkurugenzi wa mambo ya nje na uhusiano wa kimataifa wa Chadema John Mnyika, alisema ana taarifa za uhakika kwamba CAG amemaliza kazi yake na kugundua ufisadi wa mamilioni ya fedha.

“Nina taarifa za uhakika kwamba CAG amemaliza kazi yake na amegundua ufisadi wa mamilioni, kwa hivyo tunawataka wananchi wa jimbo la Ubunge tushirikiane kuibana serikali kuianika hadharani ripoti yake,” alisema Mnyika na kuongeza:

“Si hilo tu bali serikali iiwajibishe kwa kuifikisha mahakamani familia ya mzee Kingunge ambayo ndiyo inahusika na wizi huu wa mamilioni ya fedha ambao unawakosesha huduma nyingi wananchi wa Ubungo na halmashauri nzima ya Kinondoni”.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu jana, CAG Ludovick Utouh alithibitisha kukamilika kwa uchunguzi huo na kwamba ripoti yake imekamilika.

“Ni kweli ripoti ya uchunguzi wa ufisadi ndani ya stendi ya mabasi Ubungo imekamilika na nimeshaipeleka kunakohusika kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda,” alisema Utouh.

Alipoulizwa iwapo kuna ufisadi wowote aliougundua katika uchunguzi huo alijibu.

“Ahh hilo siwezi kuzungumzia si kazi yangu mimi kazi yangu niliambiwa nichunguze tu, mwenyewe Waziri Mkuu ndio mwenye haki ya kuzungumzia matokeo ya uchunguzi huo,” alisema.

Mnyika alisema mwaka 2005 aliwaeleza wananchi wa Ubungo kuwa familia hiyo ya Mbunge wa kuteuliwa na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (NEC) kuwa inafanya ufisadi mkubwa katika mkataba wa ukusanyaji mapato UBT lakini serikali ilipinga.

Kambi ya Upinzani Z'Bar yawapongeza waliokwamisha' Uandikishaji wapigakura

Salim Said
KAMBI ya upinzani kwenye Baraza la Wawakilishi imewapongeza wananchi wa jimbo la Ole kwa ujasiri wao katika kutetea haki zao uliosababisha zoezi la uandikishaji wapiga kura kwenye daftari la kudumu, kusitishwa.

Kambi hiyo inayoundwa na wajumbe wa CUF, imesema wananchi wa Ole ndio walioichachafya ZEC na kusababisha usitishwaji wa zoezi la uandikishaji.

Kambi hiyo pia imeilaumu Serikali ya Muungano na ile ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), ikidai zilihusika kuhujumu haki za kiraia na wananchi kisiwani Pemba.

Msimamo huo umo kwenye taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana baada ya kumalizika kwa kikao cha pamoja cha wawakilishi wote wa CUF kilichofanyika juzi kwenye jimbo la Wawi wilayani Chake Chake, Pemba.

Katika taarifa hiyo iliyotolewa na mwenyekiti wa kambi hiyo, Abubakar Khamis Bakar, wawakilishi wanawaunga mkono wananchi wa jimbo la Ole kwa ukakamavu na ujasiri wa kuhakikisha kwamba haki yao ya kuwa wapigakura inapatikana.

“Msimamo wa kambi ya upinzani ndani ya Baraza la Wawakilishi ni kuwaunga mkono wananchi wote waliosimama kidete kutetea haki zao, hasa wale wa jimbo la Ole,” inaeleza taarifa hiyo ya Khamis ambaye pia ni mwakilishi wa jimbo la Mgogoni.

Siku chache zilizopita, maelfu ya wananchi katika shehia za Kiuyu Minungwini, Mjini Kiuyu, Mchangamdogo, Shumba ya Vyamboni na Sizini walijikusanya kwenye vituo vya uandikishaji wakiitaka ZEC iwaandikishe watu wote wenye sifa ya kuwa wapiga kura, vinginevyo tume hiyo isiandikishe mtu hata mmoja.

Wananchi hao hawakuwa na vitambulisho vya ukaazi wa Zanzibar, ambavyo ZEC inavitambua kama kielelezo pekee cha kumuwezesha mtu kuandikishwa kuwa mpigakura.

Wananchi hao, waliokuwa wakiimba nyimbo za kuhamasishana, walidai kwamba kuandikishwa kuwa wapigakura ni haki yao ya kikatiba, msimamo ambao umeungwa mkono na watunga sheria wa Baraza la Wawakilishi kutoka kambi ya Upinzani.

“Madai ya wananchi ni halali kisheria. ZEC inajaribu kutumia sheria Namba 12 ya 2002 ambayo katika kifungu chake cha kwanza (b) inazungumzia kuwa moja ya sifa za kutoweza kujiandikisha ni kutokuwa na kitambulisho cha Uzanzibari. Lakini kifungu (a) kinasema kuwa mtu anaweza kuandikishwa ikiwa ametimiza masharti ya kifungu cha 7 (2) cha Katiba ya Zanzibar, ambacho kabisa hakiweki kitambulisho cha ukaazi kwa kigezo cha kujiandikisha,” alisema Khamis.

“Mle mnatajwa kitambulisho cha umri au uraia au uandikishwaji kuwa mpigakura. Kwa hivyo, hati yoyote ile ambayo ingeliweza kuthibitisha moja kati ya hayo ingetosha kumpatia mtu haki yake ya kupiga kura. ZEC inapolazimisha kuwa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi tu ndicho kitumike inakwenda kinyume na katiba na hilo wananchi wanalielewa.”

Khamis alisema hiyo ndiyo sababu iliyowasukuma wananchi kusema kama ni kuandikishwa, waandikishwe wote kwa mujibu wa katiba au asiandikishwe hata mmoja, kutokana na kuhisi kuwa serikali haina nia ya kuwaandikisha.

Alisema kambi yake inasimama pamoja na wakaazi wote wa jimbo la Ole na kuwataka wananchi wa maeneo mengine ya Zanzibar kuiga mfano wa wenzao kama serikali haitafanya marekebisho ambayo aliyataja kuwa ni kuondoa sherti la kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi au kuwapa Wazanzibari wote wenye sifa vitambulisho hivyo kabla ya kuanza tena zoezi hilo.

“Hapa ni moja kati ya mawili: aidha serikali iiagize ZEC kufuata ule uamuzi wa makamishna wa tume hiyo kwamba kithibitisho chochote cha ukaazi na uzawa kitumike kumruhusu mtu kuandikishwa au isitishe zoezi la uandikishaji mpaka kila mtu mwenye sifa awe amepata kitambulisho chake cha ukaazi. Hakuna njia ya mkato katika hili,” alisema Said Ali ambaye ni msemaji wa upinzani kuhusu fedha na uchumi kwenye Baraza la Wawakilishi.

Said alisema ukweli ni kuwa serikali imekuwa ikitumia hila, udanganyifu na ghilba nyingi ili kuhakikisha kuwa wakazi wengi wa kisiwa cha Pemba, ambacho ni ngome ya upinzani dhidi ya serikali, hawaandikishwi kuwa wapigakura, na hivyo kupunguza nguvu za upinzani nchini.

Said alionyesha barua zilizoandikwa mwezi Juni na Julai mwaka huu kwa hati za mkono kutoka kwa Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha kwenda kwa watendaji, akijnga hoja kuwa kiongozi huyo alishatoa agizo kwa watendaji wa chini yake kuhakikisha kuwa kila mtu anapatiwa kitambulisho.

Hata hivyo, masheha ambao ndio watendaji wa chini wa serikali wanasema kwamba hawajapewa fomu zinazowawezesha watu kupata vitambulisho hivyo.

Hivi karibuni kuliripotiwa kwamba masheha wa maeneo kadhaa kisiwani Pemba wamekuwa wakikataa kuwapatia wananchi fomu za kudai vitambulisho vya Uzanzibari Mkaazi kwa madai kwamba watu hao hawana vyeti vya kuzaliwa.

Lakini hata watu hao walipokwenda mahakamani kudai hati za viapo ili kupata vyeti hivyo, nako walikataliwa kupewa hati hizo.

Katika kile kinachoonekana kama ni kuwepo kwa usumbufu wa makusudi kwa wananchi, masheha wamekuwa wakikataa hata kutoa fomu za kuwasaidia wakazi wao kutoa taarifa za kupotelewa kwa mali zao katika vituo vya polisi.

Mfumo wa utawala wa Zanzibar unawapa masheha, ambao ni ngazi ya chini kabisa ya utawala, madaraka makubwa ya kuamua hatima ya wakaazi wa maeneo yao katika masuala mbalimbali yakiwemo haki za kiraia kama uchaguzi.

Wakilishi hao pia walilaani vikali vitendo walivyoviita vya kuingilia mamlaka za taasisi huru vinavyofanywa na mkuu wa mkoa wa Kaskazini Pemba , Dadi Faki Dadi.

Baadhi ya vitendo hivyo ni pamoja na, kufanya kikao cha pamoja kati ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa na mahakimu wa mkoa wake na kuwakataza mahakimu hao wasitoe hati za viapo kwa watu wanaokwenda kuomba hati hizo kwa ajili ya kuthibitisha uzawa wao.

Hamad amvaa JK

Salim Said na Levina Chengula
KATIBU mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad ameihusisha Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vurugu zinazoendelea Zanzibar katika zoezi la kuboresha daftari la kudumu la wapigakura, akidai ni mpango wa kumuandalia mgombea urais wa CCM visiwani humo mazingira ya ushindi mkubwa katika uchaguzi wa mwakani.


CUF imekuwa mpinzani mkubwa wa chama hicho tawala visiwani humo tangu kuruhusiwa kwa vyama vingi, kiasi cha kufanya matokeo ya uchaguzi wa rais wa visiwa hivyo kujawa na utata na mshindi, ambaye amekuwa akitokea CCM, kushinda kwa tofauti ndogo ya kura.

Lakini CUF imeeleza kuwa Serikali ya Muundano sasa inafanya njama ili mgombea wa chama hicho tawala aibuke na ushindi mkubwa zaidi ili kukimaliza nguvu chama hicho cha upinzani.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Hamad alisema serikali ya Muungano inabariki vurugu hizo ili itekeleze nia yake ya kumuwezesha mgombea wake wa kiti cha urais wa visiwa hivyo kupata asilimia 70 ya kura katika uchaguzi mkuu ujao.

“...Lakini kipindi hiki tumepata taarifa za uhakika kutoka vyanzo vya kuaminika kwamba mikakati miovu ya kulivuruga daftari la wapiga kura Zanzibar inaendeshwa na kusimamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya viongozi wakuu wa Serikali hiyo na vyombo vilivyo chini yake,“ alisema Hamad.

“Taarifa hizo zinaonyesha kwamba ni kutokana na mikakati hiyo hata maagizo yaliyotolewa hadharani na viongozi wa Zanzibar, akiwemo Rais Amani Karume kwamba Wazanzibari wote wenye sifa za kupatiwa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi wapatiwe vitambulisho hivyo na kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, hayakutekelezwa na vyombo vinavyoshughulikia suala hilo, yaani wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, Idara ya Usajili wa Wazanzibari Wakaazi na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC),“ alisema.

“Matukio yote yanayotokea kisiwani Pemba na Unguja ni mkakati uliopangwa ili kumhakikishia ushindi wa asilimia 70 mtu wao ambaye wameshamuandaa.”


Kwa mujibu wa Hamad, ambaye alikuwa waziri kiongozi wa Zanzibar, serikali ya Muungano imeagiza kukiukwa maelekezo ya taratibu za zoezi hilo ili kupunguza kwa madri itakavyowezekana idadi ya Wazanzibari wenye na pia kuwaingiza wengine wasio Wazanzibari.

Alisema hayo yanafanyika ili CCM ijihakikishie ushindi mkubwa katika uchaguzi wa mwakani visiwani humo na kwamba matokeo yameshapangwa.

Alisema kwa upande wa Zanzibar mkakati huo unaungwa mkono na kuratibiwa na baadhi ya viongozi wa SMZ wenye malengo ya kugombea urais, ambao wamepewa tamaa na viongozi wa Serikali ya Muungano kwamba wana nafasi nzuri ya kupitishwa na Halmashauri Kuu ya CCM.

“Tunazo taarifa za kutosha za hata wakuu wa mikoa na wilaya wa Zanzibar waliyoandaliwa kutekeleza mkakati huu muovu kufikia hatua ya kudharau hata maagizo ya SMZ kwa madai kwamba wanachokifanya kimeagizwa na Serikali kuu ya Muungano,” alisema Hamad.

Kwa mujibu wa Hamad, hadi sasa mkakati huo umefanikisha kuwakata zaidi ya watu 11,000 katika majimbo matatu ya Konde, Mgogoni na Micheweni Kisiwani Pemba na wengine 6,000 katika Jimbo la Magogoni, Unguja.

“Hali hii inatisha na iwapo itakamilishwa katika majimbo yote 50 ya Zanzibar kwa wastani wa kukatwa watu 3,500 kwa kila jimbo, itasababisha Wazanzibari wasiopungua 175,000 kunyimwa haki ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa 2010,” alisema.

“Huu ni uhalifu na uporaji mkubwa wa haki ya Wazanzibari ya kuchagua na kuwaweka madarakani viongozi wanaowataka, uliopangwa kutekelezwa na viongozi wa juu wa Muungano. Lakini uhalifu na uporaji huu hauwezi kukubalika hata kidogo kwa Wazanzibari.”
Zanzibar ina takriban watu milioni moja.


Alisema kuhusika kwa Serikali ya Muungano katika mkakati huo kunathibitishwa na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyoitoa bungeni mjini Dodoma kwamba uandikishaji wa wapiga kura Zanzibar ni halali na unafanywa kwa mujibu wa sheria licha ya wakazi wengi kunyimwa haki zao.

“Inasikitisha zaidi kuona kwamba Serikali ya Muungano sasa imejiingiza kichwa kichwa katika kuvuruga daftari la wapigakura kwa malengo ya kulinda maslahi yake maovu visiwani na dhidi ya demokrasia,” alifafanua Hamad.

Alikumbusha kauli ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa bungeni Disemba 30 mwaka 2005 kwamba anasononeshwa na mpasuko wa kisiasa Zanzibar na kuahidi kuupatia ufumbuzi wa kudumu mpasuko huo haraka, akisema hakuwa na nia hiyo.

“Hatukujua kwamba dhamira yake halisi ya kuupatia ufumbuzi mpasuko huo ni kuvuruga daftari la wapigakura na uchaguzi ili chama na mgombea wake wa urais Zanzibar aonekane anakubalika,” alisema Hamad.

Alisema tayari wameshawaeleza Wazanzibari kutokubali kunyimwa haki zao na kuwataka wasimame kidete kudai haki zao kwa njia za amani bila ya kufanya vurugu.

“Hivi sasa sio Pemba tu, hata Unguja jana (juzi) nasikia wamewafungia ndani wafanyakazi wa Idara ya Uandikishaji Vitambulisho vya Ukaazi. Lakini kwa nini serikali iwafikishe hapo wananchi; kwa nini chaguzi zisiwe huru na haki; kwa nini tusiandae mkakati wa kufanya chaguzi huru na haki,” alihoji Hamad.

Hamad aliziomba kumuiya ya kimataifa kuingilia kati mikakati hiyo kwa lengo la kuinusuru Zanzibar na Tanzania kwa ujumla dhidi ya hatari ya kutokea janga alilodai linaandaliwa na serikali ya Rais Kikwete.

Hivi karibuni kumetokea matukio yanayoashiria machafuko ya kisiasa Zanzibar baada ya kuanza kwa awamu ya kwanza ya uboreshaji wa daftari la wapigakura ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi mkuu wa 2010.

Baadhi ya matukio hayo ni kumwagiwa tindikali kwa sheha wa Ole, Mussa Ali; kukataliwa baadhi ya wananchi kujiandikisha katika daftari; kususiwa kwa daftari; nyumba za viongozi kulipuliwa kwa mabomu na kukamatwa kwa watu wakihusishwa na vurugu zilizosababisha Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kusitisha kazi hiyo kwa muda usiojulikana.

Unguja waja juu kudai Zan ID

Salim Said
ZAIDI ya watu 300 kisiwani Unguja jana walikusanyika kwenye ofisi ya Idara ya Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi (Zan ID) na kuwafungia ndani wafanyakazi wa idara hiyo wilayani Kaskazini ‘A’ wakidai kuwa wamenyimwa vitambulisho.


Wananchi hao walianza kumiminika kwenye ofisi hiyo iliyo eneo la Gamba majira ya saa 1:00 asubuhi na baadaye kuchukua uamuzi wa kufunga ofisi baada ya kubaini kuwa wengi matatizo yao yanafanana.

Wakizungumza na Mwananchi jana kwenye eneo hilo, baadhi ya wananchi hao walisema wamechoshwa na usumbufu ambao wanaupata kutoka kwa ofisi hiyo serikali katika kudai haki zao.

Mmoja wa wananchi hao Faki Ali alisema, amejaza fomu kutoka kwa Sheha na kuirudisha katika ofisi ya Zan ID na kupatiwa stakabadhi lakini amekuwa akizungushwa kwa zaidi ya miezi miwili sasa.

“Tumechoka kabisa kuacha kazi zetu kila siku kwa kufuatilia kitambulisho halafu hatupewi, tumekamilisha taratibu zote lakini wanatuzungusha tu kila siku,” alisema Ali na kuongeza:

“Sisi tumekaa zaidi ya vijana 300 nje ya ofisi za wilaya za vitambulisho hata hawatujali wanachotuonesha ni dharau tu tukaamua tuwafungie ndani wafanyakazi wao”.

Alisema kejeli na dharau za wafanyakazi wa ofisi ya vitambulisho zimechupa mipaka na kuhoji kuwa hawajui kiburi hicho wanakitoa wapi.

Naye Juma Khamis Ngwali alisema, waliamua kuwafungia ndani wafanyakazi hao majira ya adhuhuri baada ya kukaa nje ya ofisi hiyo kwa muda mrefu bila ya kuhudumiwa.

“Kama huna kitambulisho cha mzanzibari mkaazi tume haikusajili ndani ya daftari la kupiga kura, huku tumefuata taratibu zote hadi mahakama imetoa hati watu wapewe vitambulisho lakini wanatuzungusha tu,” alisema Ngwali.

Alisema walikaa nje ya ofisi hiyo ya Idara ya Vitambulisho ya Wilaya ya Kaskazini A Uguja kwa zaidi ya saa nane bila ya hata kuulizwa.

Mkurugenzi wa Idara ya Vitambulisho Zanzibar Mohammed Ame alithibitisha kutokea kwa tukio hilo jana ambazo alizipata kutoka kwa Mkuu wa Ofisi ya Wilaya ya kaskazini A.

“Nikweli nimezipata taarifa hizo kupitia kwa ‘incharge’ msimamizi wa ofisi kwamba kuna vijana wamejikusanya wengine wakiwa hawana vyeti vya kuzaliwa na wengine hawana barua za sheha lakini wanalazimisha wapewe vitambulisho,” alisema Ame.

Hivi karibuni matukio ya vurugu yamekuwa yakitokea Zanzibar kufuatia kuanza kwa awamu ya kwanza ya uboreshaji wa daftari la wapigakura ikiwa ni pamoja na Sheha wa Shehia ya Ole Mussa Ali alimwagiwa tindikali usoni tukio ambalo lilipelekea kukamatwa kwa Katibu wa Tawi la Kianga la CUF Ali Mussa Salim.

Juzi ZEC iliahirisha zoezi la uandikishaji wa wapigakura kisiwani Pemba baada ya wananchi kugoma kwenda vituo kujiandikisha kwa sababu kila anayekwenda anakataliwa kwa sababu ya kukosa Zan ID.

Hatua hiyo ilisababisha askari wa Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (KVZ) kufyatua risasi hewani na kuongeza vurugu huku vijana wawili wakikamatwa na kuwekwa ndani.

Dk Mwinyi: Tupo tayari kusaidia ulinzi Pemba

Mohamed Ghassan, Pemba na Salim Said
WAZIRI wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dk Husein Mwinyi amesema Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) halitakiwi kufanya shughuli zozote za ulinzi katika maeneo ya vituo vya uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura hadi hapo mamlaka za kiraia zitakapoliomba rasmi kufanya kazi hiyo.

Dk Hussein Mwinyi ametoa kauli hiyo katika uwanja wa ndege wa Karume kisiwani Pemba muda mfupi baada ya kuwasili na ujumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanya ziara ya siku moja kisiwani Pemba.

"Sisi kama wasimamizi wa JWTZ, kwa kawaida mpaka mamlaka za kiraia zitakapotuomba rasmi msaada wetu kama utahitajika ndipo huwa tunafanya kazi hiyo, lakini kwa sasa tumekuja kwa safari ya kawada tu kutembelea vikosi vya Jeshi," alisema Dk Hussein Mwinyi.

Dk Mwinyi alisema wao kama viongozi wa Wizara zilizo chini ya kamati hiyo ya bunge ya ulinzi na usalama wanatakiwa kuwa pamoja na kamati hiyo katika maeneo yote wanayotembelea na kukagua vikosi vya JWTZ, Jeshi la Polisi, Uhamiaji pamoja na kuangalia majukumu ya ulinzi na usalama katika kisiwa cha Pemba.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati hiyo Wilson Masilingi alisema kamati yake imesikitishwa na matukio yaliyojitokeza katika zoezi la uandikishaji ikiwemo kumwagiwa tindikali mmoja wa viongozi (Sheha) hali ambayo ni tishio la uvunjifu wa amani.

Alisema kamati hiyo inawaomba Wazanzibari upande wa Pemba watoe ushirikiano kwa Serikali hasa baada ya kufanya mazngumzo na Rais Aman Abeid Karume ambaye aliihakikishia kamati hiyo kuwa kila mtu atapata haki ya kuandikishwa ili aweze kupiga kura.

Miongoni mwa wajumbe wa kamati hiyo waliowasili jana Pemba ni Jackson Makweta, Athuman Ngwilizi, Masoud Abdllah Salim, Feteh Mgeni, Beutrice Shelukindo, Khalifa Suleiman, Saleh Farah na John Shibuda.

Taarifa za kuwasili kwa kamati hiyo ya bunge zilipokelewa kwa hisia tofauti huku wananchi wengi wakiamini kuwa ziara hiyo ililenga suala zima la uandikishaji hasa baada ya tukio la askari wa vikosi vya SMZ kufyatua risasi katika kituo cha Mchanga mdogo muda mfupi baada ya tume ya uchaguzi kufunga vituo vya uandikishaji.

Wakati huo huo Mbunge wa viti maalum jimbo la Wete (CUF) Riziki Omar Juma alisema, wananchi walijitokeza kwa wingi katika vituo vya kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura jana, lakini walikuta vituo hivyo vikiwa vimefungwa.

Alisema Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ilisimamisha zoezi hilo juzi baada ya kutokea kwa vurugu baina ya wananchi na vyombo vya dola.

Alifafanua kuwa, ZEC haikuwatangazia wananchi kwamba zoezi hilo limesitishwa na hivyo kusababisha wananchi hao kujitokeza kwa wingi katika vituo vya kujiandikishia.

“Sisi tulifika vituoni majira ya saa 3:00 asubuhi na kuwakuta wananchi wengi vituoni, lakini tuliwaomba wananchi watawanyike na kwenda kufanya shughuli zao kwa sababu ZEC imesitisha uandikishaji,” alisema Juma ambaye pia ni Katibu wa CUF wilaya ya Wete.

Katika hatua nyingine Mbunge Juma alisema, vijana Ali Bakari Hassan na Khamis Ali Ali walioshambuliwa na askari wa Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) walifikishwa mahakamani jana wakikabiliwa na makosa ya Uzembe, Ukorofi na kuzuiya gari la msafara wa askari waliokuwa wakienda kumpeleka Sheha.

“Hata hivyo kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 11 mwaka huu na washitakiwa wamerudishwa rumande baada ya kukataliwa kupewa dhamana,” alisema Juma.

Aliiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kuhakikisha kwamba wanatumia nafasi hiyo ya kusitishwa kwa zoezi la uandikishaji kuwapatia wananchi haki yao, ambayo wananyimwa kutokana na kisingizio cha kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi (Zan ID).

“Haki tunanyimwa kwa kisingizio cha Zan ID na chanzo cha kupatia kitambulisho hicho ni masheha ambao ni kikwazo kikubwa, wanaweka vipingamizi vya kila namna ilimradi kuwakwamisha na kuwakatisha tamaa wananchi,” alisema Juma.

Vurugu zaibuka uandikishaji daftari wasimama Pemba


Mohamed Ghasan, Pemba na Salim Said


KWA mara ya kwanza tangu kuanza kwa zoezi la kurekebisha Daftari la wapiga kura, Pemba, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) imelazimika kufunga vituo vya uandikishaji kufuatia vurugu zilizoibuka baina ya maafisa wake na wananchi walioshiniza kuwa watu wote waandishwe.

Mwenyekiti wa ZEC, Khatibu Mwinchande, alisema wamefunga vituo vyote vitatu vya uandikishaji katika jimbo hilo la Ole na kusisitiza kuwa endapo hali hiyo itajitokeza tena leo, watashauriana kwa pamoja kabla ya kuamua kuhamisha zoezi hilo katika jimbo la Mtambwe.

Hivi karibuni Sheha wa Shehia ya Ole Mussa Ali alimwagiwa tindikali na kusababishwa kukamatwa kwa Katibu wa Tawi la Kianga la Chama cha Wananchi (CUF), Ali Mussa Salim.

Hatua hiyo imekuja katika siku ya kwanza ya uandikishaji katika Jimbo la Ole lililopo Wilaya ya Wete kisiwani Pemba ambapo maelfu ya wananchi waliojitokeza kuandikishwa walionekana kutoridhika na maelezo ya waandikishaji wa tume ya uchaguzi waliotaka kila mmoja kuwa na kitambulisho cha ukaazi.

Katika kituo cha Minungwini, wananchi wakiwemo wenye vitambulisho waligoma na kupinga kuandikishwa kwa mtu yoyote kwa madai kuwa kufanya hivyo ni kuwanyima haki wasioukuwa na vitambulisho.

"Hapa haandikishwi mtu, kama mnataka mtuandike wote, hii ni haki ya kila mwananchi, msitufanyie ubaguzi, kama hamuwezi ondokeni, lakini msimamo wetu ndio huu, sisi tuna vyeti vya kuzaliwa ambavyo tulivitumia tulipoandikishwa 2005," alisema mmoja wa wananchi hao huku akishangiliwa na wenzake.

Viongozi wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa Kaskazini Pemba, Dadi Faki Dadi na Mkuu wa Wilaya ya Wete, Omar Ali walijaribu kila njia kuwashawishi waliokuwa na vitambulisho vya ukaazi wajiandikishe, lakini juhudi zao ziligonga mwamba kutokana na msimamo mkali waliouonesha.

Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wananchi hao kumpatia hati za kuzaliwa walizokuwa nazo, lakini bila ya kutegemea alikataliwa huku akitupiwa maneno makali yakiwemo ya kutomwamini.

Kufuatia hali hiyo, ilibidi kuimarishwa kwa ulinzi katika katika kituo hicho na Jeshi la Polisi lilituma magari mawili yaliyobeba askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), JKU, Mafunzo na Valentia wote wakiwa na silaha za moto.

Wakati wananchi hao wakiendelea na msimamo wao wa kutotaka kuandikishwa, Mkuu wa Mkoa alilazimika kuzungumza na Mwakilishi wa Jimbo la Ole, Hamad Masoud akimtaka kuzungumza na wananchi ili waondoke katika eneo hilo, ombi ambalo Mwakilishi alilikataa kwa madai kuwa sio kazi yake.

"Mimi sio kazi yangu kuwaondoa, unataka niwaondoe kwa mamlaka gani ya sheria, siwezi, wewe ndiye mkuu wa mkoa uko na mkuu wa wilaya na hawa ni wananchi unajuaje kama ni wafuasi wangu, kwani hakuna wanachama wa CCM, ndipo uniambie kuwa wote hawa ni CUF?" alihoji mwakilishi huyo.

Baada ya muda mfupi walitokea viongozi wa Zec wakiongozwa na Mwenyekiti Mwinchande alikifuatana na makamishna wake ambao walifanya mazungumzo na waandikishaji na baadae mwakilishi wa jimbo hilo kuhusiana na suala hilo.

Majadiliano hayo yaliyochukua zaidi ya nusu saa huku wakibishana kisheria kuhusu uwezo wa mwakilishi kuwaondoa wananchi katika eneo hilo na kuwataka kuandikishwa wenye sifa. Hata hivyo mwakilishi huyo alishikilia msimamo wake kuwa hiyo si kazi yake bali inapaswa kufanywa na tume ya uchaguzi.

Utaratibu unaotumiwa na tume ya uchaguzi ni kuandikisha wapiga kura wapya kwa muda wa siku mbili wakati wale waliondkishwa mwaka 2005 utaratibu wao huchukua muda wa siku tano.

Awali akizungumza na Mwananchi mwakilishi wa jimbo hilo alisema, zoezi hilo limesimama katika vituo vya Kambini na Kiuyu Minungwini, Mjini Kiuyu tangu vituo vilipofunguliwa leo (jana) asubuhi kwa sababu wananchi wamekataa kwa kuwa wenzao wamezuiwa.

“Kila kituo kimesimama kwa sababu kila anayeingia kituoni anakataliwa kwa sababu hana kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi (Zan ID) au kadi ya kupigia katika uchaguzi wa 2005. kwa hiyo wananchi wote wameamua kwa umoja wao kugomea zoezi hadi hapo wenzao wote wenye sifa watakapoandikishwa,” alisema Masoud.

Alisema Sheha wa Kambini, Ali Said Ali amekuwa akiwambia wananchi kuwa yeye si sheha kila wanapomfuata ofisini kwake kutaka fomu za kutafutia vitambulisho vua ukazi (Zanzibar ID).

“Pia wananchi baada ya kumuona katika kituo cha uboreshaji wa daftari la wapigakura wamemkataa sheha wao kwa sababu kila siku huwambia yeye si sheha, sasa wanashangaa kumuona kitioni,” alisema Masoud.

“Kwa kweli hali ni mbaya, mbaya, mbaya kupita maelezo, dhuluma tunayofanyiwa Wapemba imepita mipaka. Walipitisha sheria yao ya uchaguzi na ya vitambulisho, lakini wanashindwa kuidhibiti na kuisimamia ili wananchi wapate haki zao. Sasa katiba ya Zanzibar imekuwa haina tena maana mbele ya sheria,” alisema Hamad.

Alisema wako tayari kuuawa tena au kupigwa risasi na mabomu kwa mara ya pili lakini hawatakubali kudhulumiwa haki zao za kupiga kura.

Awamu ya kwanza ya uboreshaji wa daftari la kudumula wapiga kura kisiwani humo lilianza Julai 6, mwaka huu na awamu ya pili na ya mwisho inatarajiwa kuanza Januari mwakani.