MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Wednesday, June 24, 2009

Profesa Lipumba aiponda bajeti ya 2009/10




Salim Said
JUNI 18 mwaka huu Watanzania wameshuhudia wabunge wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wakiipitisha kwa kishindo bajeti ya serikali ya Sh9.5 trilioni kwa mwaka 2009/10, baada ya wabunge 221 wa chama hicho kuipigia kura za ndio.

Katika kazi ya kupitisha bajeti hiyo, jumla ya wabunge 33 wa kambi ya upinzani kati ya wabunge wote 318 wa bunge la Tanzania, waliipinga bila ya mafanikio kwa kupiga kura za sio, kutokana na idadi yao kuzidiwa na wale wa CCM waliopiga kura za ndio.

Bajeti hiyo ambayo awali ilipata upinzania mkubwa kwa wabunge wa CCM kabla ya kufika bungeni, lakini kilichotokea ni kwa ujasiri wa wabunge hao haukuthubutu kujitokeza bungeni jambo ambalo baadhi ya wachambuzi wamesema ni unafiki.

Wadau mbalimbali wa masuala ya kiuchumi nchini waliipokea kwa mitazamo tofauti bajeti hiyo na kutoa maoni yao wakiamini kuwa serikali huenda ikayatumia katika kuirekebisha bajeti hiyo.
Mchambuzi nguli, wa masuala ya kiuchumi nchini Profesa Ibrahim Lipumba anaiponda bajeti hiyo kwa madai kuwa, ni tegemezi na haiwezi kumfikisha popote mtanzania wa kawaida.

Anasema, bajeti hiyo haikuzingatia misingi muhimu ya bajeti na hivyo haiwezi kuitwa bajeti bora na iliyokamilika.

Anasema bajeti hiyo, ina upungufu mwingi na haiwezi kabisa kupambana na matatizo ya umasikini yanayomkabili Mtanzania wa kawaida, kwa sababu haikuzingatia misingi muhimu ya bajeti.

“Bajeti hii bado ni tegemezi iliyojaa kasoro na wala hawiezi kumfikisha popote mtanzania wa kawaida katika kumuondeshea matatizo ya umasikini wa kipato,” anasema Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) anasema, bajeti iliyokamilika inapaswa kujumuisha mapato yote na matumizi ya serikali bila ya kujali taratibu maalum za kuendesha baadhi ya miradi au programu.

“Kwa ujumla mapato na matmizi yote lazima yapangwe na kuainishwa katika bajeti bila ya kujali chanzo cha mapato, hii itabainisha iwapo kuna uhusiano wa karibu kati ya mapato na wanaonufaika na matumizi ya mapato hayo, kwa sababu hoja ya mapato husika kulipia matumizi ya huduma inakubalika,” anasema Profesa Lipumba.

Anasema, utayarishaji wa bajeti lazima uzingatie malengo ya uchumi mpana, ukuaji wa pato la taifa, mfumko wa bei, akiba ya fedha za kigeni na thamani ya sarafu ya nchi husika.

“Bajeti bora lazima matumizi yake yagawiwe kulingana na malengo ya sera ya maendeleo ya taifa kwa sababu jambo linaloathiri sera, utayarishaji na utekelezaji wa bajeti ni uanzishwaji wa sera na utamkaji wa ahadi zisizoendana na vipaumbele vilivyotumika kuandaa bajeti,” anasema Profesa Lipumba.

Anafafanua kwamba, pia bajeti lazima ilenge kujenga mazingira mazuri ya utekelezaji mzuri wa bajeti ya serikali.

Anasema, kwa kuwa bajeti ni kioo cha sera za serikali, ni lazima iwe na uhusiano wa karibu na sera hizo ili kuratibu vizuri uanzishwaji wa sera na kushirikisha umma katika utungaji wake.

Anasema, bajeti lazima iweze kupitia na kutathmini mafanikio na mapungufu ya sera za maendeleo ya taifa na kuchambua kwa kina mahitaji ya fedha na rasilimali nyingine za taifa, ili kuhakikisha bajeti inashika hatamu katika mapato na matumizi ya serikali.

“Maandalizi ya bajeti lazima yazingatie hali halisi ya uchumi ili kuweza kukadiria kwa usahihi mapato na kuyatambua matumizi yake yote ya lazima,” anafafanua Profesa Lipumba.

Anasema, bajeti ya mwaka huu ni ya kisanii kwa sababu haikuzingatia sera za maendeleo ya taifa ikiwamo ya Mkakati wa Kukuza na Kupunguza Umasikini (Mkukuta), Dira ya Maendeleo ya 2025, Ilani ya CCM na Mpango Maalum wa Kurahisisha Maendeleo (Tiger Plan 2020).

Anasema, mpango wa kunusuru uchumi wa nchi umetengewa sh1.7 trilioni na rais Jakaya Kikwete, ambaye amesema fedha hizo zimeingizwa katika bajeti ya serikali, lakini bajeti haijaainisha waziwazi mpango huo na matumizi ya fedha hizo.

Anailaumu serikali, kwa kukusudia kukopa kiasi hicho cha sh1.7 trilioni kwa riba kubwa ili kukopesha kwa wafanyabiashara kwa riba ndogo.

“Hivi wewe unakopa fedha kwa riba ya asilimia 11 au zaidi, halafu unamkopesha mfanyabiashara kwa riba ya asilimia 2, hizo ni akili kweli? Tutasema wewe uko makini kweli au una lengo zuri kwa wananchi wako,” anahoji profesa Lipumba.

Anasema, kwa mujibu wa utafiti wa Shirika la Fedha Duniani (IMF) umebaini kuwa mabenki ya kigeni yaliyopo nchini yanakula njama ya kuhakikisha kuwa yanapata faida kubwa na kwa haraka ili kununua amana za serikali.

“Benki Kuu ya Tanzania (BoT) haina mamlaka ya kupanga riba kwa wateja wa benki za biashara. Tusipokuwa makini mikopo ya serikali itawanufaisha wenye mabenki na kuwadidimiza wafanyabiashara wetu wadogo na wa kati,” anatoa angalizo.

Anasema, benki zinawalipa riba ndogo wanaoweka akiba zao kwa wastani wa asilimia 2.7 wakati yanatoa mikopo kwa riba ya wastani wa asilimia 16.1 huku kukikosekana benki inayofanya jitihada za kutosha kutoa motisha na kukusanya akiba za watanzania.

“Serikali imeweka mikakati na mfumo gani wa kiutawala ili kuhakikisha Benki ya Rasilimali (TIB) haitoi mikopo kisiasa na fedha za walipa kodi zilizoweka kama mitaji katika benki hiyo hazipotei,” anahoji Profesa Lipumba.

Anasema, ili kunusuru hilo, utawala wa benki hiyo unahitaji kuimarishwa, kwa kuteua watendaji makini na Bodi ya Wakurugenzi iteuliwe bila ya kujali hisia za kichama ili iwe na mamlaka ya kusimamia watendaji wake na kutotoa mikopo kisiasa na kifisadi.

Profesa Lipumba anasema, kaulimbiu ya ‘Kilimo Kwanza’ ni msemo wa kisiasa na kwamba imepita mingi lakini katika utendaji hakuna mabadiliko kwa kuwa mgao wa fedha katika sekta hiyo hauna tofauti na ule wa mwaka jana katika bajeti.

“Bajeti ya mwaka jana ilitenga sh513 bilioni sawa na asilimia 7.1 na hii ya mwaka huu imetenga sh666 bilioni sawa na asilimia 7.0 ya bajeti yote. Je tofauti iko wapi, ni usanii tu wa kisiasa katika utendaji,” anasema Profesa Lipumba.

“Mara Kilimo Kwanza, Kilimo ni Uti wa Mgongo, Siasa ni Kilimo, Utu ni Kilimo yote ni misamiati tu ya kuwababaisha watanzania.”

Anasema, ili kuhakikisha umasikini unapungua vijijini kilimo kinapaswa kukuwa kwa wastani wa asilimia 6 hadi 8, kwa mwaka katika kipindi cha mpito kwani wakulima wadogo ndiyo tegemeo la kilimo cha Tanzania, lakini hawajasaidiwa vya kutosha kuboresha kilimo chao.

Anaitaka serikali kufuta misamaha ya kodi kwa viongozi wa juu wa serikali na wabunge na kuhakikisha kuwa wanalipa kodi ili kuondoa matabaka kati yao na wanaowaongoza.

“Mapato mingi ya serikali yanapotea kupitia misamaha holela ya kodi. Viongozi wana misamaha mingi ya kodi ikiwa ni pamoja nay a kuingiza vitu vyao binafsi nchini,” anasema Profesa Lipumba.

Kwa upande wake Msomi wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam Dk. Benson Bana anatofautiana na Profesa Lipumba kuhusu bajeti hiyo akisema kwamba, ni nzuri na imezingatia vipaumbele muhimu kwa maisha ya Mtanzania.

“Profesa Lipumba, ni mchumi nguli, tunamuamini na tunamuheshimu kweli, lakini profesa huyu ni mwanasiasa, hivyo nilitegemea ataipinga, na kama angeipongeza au kuikubali ningemshangaa sana, hasa ukizingatia nafasi yake,” anasema Dk. Bana.

Anasema, “Namuheshimu sana lakini naweza kumkosoa Profesa kwa hili, bajeti yetu imezingatia sana misingi ya bajeti ina uhusiano na sera zote za maendeleo ya taifa na imeainisha mapato na matumizi ya serikali kwa mwaka wa bajeti, kwa sababu hata mimi nimechambua.”

Anasema bajeti kwa kawaida inatenga fungu maalum kwa ajili ya vipaumbele vyake kwa kuzingatia umuhimu, mahitaji na uwezo wa mapato ya taifa na sio kupanga bajeti kubwa hadi kuvuka kiwango cha mapato yako, itakuwa haitekelezeki.

Lakini Dk Bana anasema, bajeti hiyo imeandaliwa na wataalamu wa fedha na uchumi nchini ambao ni wanafunzi wa Profesa Lipumba.

CUF yaanza kuweweseka kwa Lwakatare

Salim Said
SIKU chache baada ya Willfred Lwakatare kuvua nyadhifa zake zote na kurudi jimboni kwake, CUF imeanza kudhibiti nyendo zake baada ya kumzuia kufanya mikutano ya hadhara.


Mkurugenzi wa habari na uenezi wa CUF, Ashura Mustafa aliiambia Mwananchi jana kuwa chama hicho kimesambaza barua katika wilaya na matawi yake yote nchini kuwaagiza watendaji wake wamdhibiti Lwakatare ili asifanye mikutano kwa mgongo wa chama.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Lwakatare, ambaye amekuwa akiripotiwa kuhutubia mikutano ya hadhara akiuliza watu ahamie chama gani, haruhusiwi kufanya mkutano wowote isipokuwa kwa idhini ya makao makuu.

Nafasi ya Lwakatare, ambaye aliondolewa katika kutetea nafasi yake ya naibu katibu mkuu baada ya kuuishikilia kwa karibu miaka 10, ilichukuliwa na Joram Bashange. Kwa upande wa Zanzibar, nafasi hiyo inashikiliwa na Juma Duni Haji.

Kitendo hicho kilimfanya aandike barua ya kujivua nyadhifa zote kwenye chama hicho na kubaki na mwanachama wa kawaida.

Jana Ashura aliliambia gazeti hili kuwa pamoja na chama kusambaza barua hizo za kumzuia Lwakatare kufanya mikutano, pia kinakusudia kutoa tamko zito dhidi ya mbunge huyo wa zamani wa Bukoba Mjini.

Alisema anachofanya Lwakatare si kuimarisha chama kama alivyodai kwenye barua yake kwa mwenyekiti alipotaka kujiuluzu bali kukivuruga katika kipindi hiki cha kukaribia chaguzi za kitaifa.

“Ni kweli tumewaandikia wenyeviti wa chama katika kata na wilaya zote Tanzania Bara na hasa Kanda ya Ziwa kuwataka kuwataka wamzuie Lwakatare kufanya mikutano ya kukivuruga chama kwa kuwalisha sumu wa wananchi akitumia jina la CUF,” alisema Mustafa.

“Tumewaagiza kama atataka kufanya mkutano wowote kwa jina la CUF asiruhusiwe, badala yake waripoti makao makuu, halafu tutaangalia lengo la mkutano huo. Tukijiridhika tunaweza kuruhusu lakini bila hivyo asifanye.”

Alisema Lwakatare sasa hana mamlaka kikatiba kufanya mkutano wowote kwa jina la CUF kwa sababu si kiongozi tena wa chama bali mwanachama wa kawaida.

“Kwa vile ameamua kujivua nyadhifa zake zote ndani ya chama na chama kimeridhia, hana tena mamlaka ya kuitisha mikutano ya wanachama; uwe wa hadhara au wa ndani,” alisema Mustafa.

Mwishoni mwa wiki iliyopita mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alimsihi Lwakatare kutoharibu chama baada ya kujiengua katika nyadhifa zake.

Habari za ndani zinasema kuwa tayari viongozi wakuu wa chama hicho- Prof Lipumba, katibu mkuu Seif Sharif Hamad na makamu mwenyekiti Machano Khamis- wamekutana kujadili namna ya kukihami chama na kile kilichoelezwa kuwa mkakati wa Lwakatare kutaka kukichafua.

Inadaiwa kuwa katika kikao hicho, Machano, ambaye alifanya ziara fupi Kanda ya Ziwa baada ya Lwakatare kujiuzulu, alieleza mambo aliyoyaona wilayani Bukoba kuhusu maendeleo ya chama chao.

Akizungumzia uamuzi huo wa CYF, Lwakatare aliiambia Mwananchi kuwa hana taarifa ya agizo hilo kwa kuwa anaamini halijafika wilayani kwake Bukoba mjini.

“Huku hili agizo au barua halijafika na ikifika tutaijadili kuona kitu gani cha kufanya kuweza kufanya kazi yangu ya kuimarisha chama,” alisema Lwakatare jana.

“Mimi bado ni mwanachama wa CUF na nilisema kwamba uamuzi wa kujiunga na chama chochote upo mikononi mwa familia yangu, wananchi na viongozi wangu wa CUF,” alisema Lwakatare alipozungumza kwa njia ya simu akiwa Bukoba.

'Kutogusa Meremeta ni kukiuka utawala bora'

Salim Said
UAMUZI wa Serikali kuzuia kujadiliwa kwa kampuni ya Meremeta Gold Mine umeelezwa kuwa ni ukiukwaji wa misingi ya utawala bora, wanaharakati na wanasiasa wameeleza.


Kwa mara nyingine, serikali juzi ililieleza Bunge kuwa masuala yanayohusu kampuni ya Meremeta hayawezi kujadiliwa kwenye chombo hicho cha wawakilishi wa wananchi kwa kuwa yanahusu usalama wa nchi na Jeshi la Wananchi (JWTZ).

Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Jeremiah Sumari alitoa tamko hilo akirejea kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyoitoa Bungeni mwaka jana kuwa suala hilo haliwezi kujadiliwa na kuwataka Wabunge waheshimu kauli hiyo ya mtendaji mkuu wa serikali.

Katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, ambaye aliuliza swali la msingi, alipotaka kueleza kuwa anachohoji ni wizi, spika wa Bunge, Samuel Sitta alimkatisha na kumwambia kuwa walishakubaliana katika kikao cha kamati ya maadili ya viongozi kuwa suala la Meremeta lisijadiliwe hadharani kwa sababu za kiusalama.

Jana mratibu wa masuala ya utawala bora wa Mtandao wa Mashirika ya Wanaharakati (FemAct) ambao unaunganisha taasisi 50, Buberwa Kaiza alisema jana kuwa kitendo hicho kinajenga taswira kuwa dola inashabikia ufisadi.


Alisema katika nchi yoyote inayofuata misingi ya utawala bora, hakuna jambo linalopaswa kuendeshwa kwa usiri hasa jambo hilo linapohusu wizi wa mali ya umma na kwamba kuzuia Meremeta kujadiliwa hadharani ni kukiuka kanuni hizo.

“Katika utawala bora hakuna siri na matumizi ya fedha za umma yanapaswa kuwekwa hadharani,” alisema Kaiza.

Alisema ni jambo la kushangaza kuona bunge ambalo ni sehemu pekee ya haki ya kuzungumza na kujadili masuala ya maendeleo ya nchi, hasa matumizi ya fedha za umma linazuiwa kujadili kampuni hiyo ya Meremeta kwa kigezo cha ulinzi na usalama wa taifa.

Kaiza, ambaye pia ni mkurugenzi mtendaji wa shirika la Fordia, alisema: "Hii ni ishara ya nchi kutekwa na mafisadi kwa sababu serikali imeamua kuwatetea kwa nguvu zote watu wachache ambao wanatuhumiwa kwa matumizi mabaya ya fedha za umma."

Kauli ya Buberwa iliungwa na mkono na katibu mkuu wa chama cha NCCR- Mageuzi, Samwel Ruhuza aliyetaka kampuni hiyo ijadiliwe kwa sababu imetuhumiwa kwa ufisadi ambao hauna uhusiano na usalama wa taifa.

Ruhuza alisema licha ya kuwa suala la Meremeta linahusisha usalama wa taifa, serikali inatakiwa kutambua kuwa kampuni hiyo inahusika na ubadhilifu wa fedha za walipakodi.

“Hivi mfanyakazi wa usalama wa taifa akiiba hataulizwa wala kushtakiwa," alihoji Ruhuza
"Suala la msingi hapa ni ubadhilifu... hayo ya usalama yasijadiliwe, lakini hili la ubadhilifu lazima liongelewe.”


Kwa mujibu wa Ruhuza, inaeleweka kuwa fedha nyingi za walipakodi zilitolewa na kupelekwa Meremeta, hivyo serikali haina sababu za kuzuia suala hilo kujadiliwa hadharani kwa kuwa linawahusu wananchi.

“Mimi sina haki ya kujua kama jirani yangu anamiliki bunduki au la lakini ikitokea mtoto wangu amekutwa ameuawa nje ya nyumba ya jirani yangu, hapo lazima niulize ili nipate ufafanuzi na maelezo sahihi juu ya kifo hicho sasa suala hili ndio mfano halisi wa hii kampuni ya Meremeta.”

Kauli hiyo ya serikali imekuja wakati Bunge likiwa limemuagiza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali (CAG), kuikagua Meremeta pamoja na Mwananchi, ambayo imeelezwa kuwa iko katika mchakato wa kufilisiwa na kwamba itajadiliwa baada ya kumalizika kwa zoezi hilo.

Inadaiwa kuwa wanahisa wa Meremeta, ambayo ilipewa kiasi cha Sh155 bilioni na Benki Kuu (BoT) katika mazingira yanayoonyesha kuwepo kwa ufisadinatuhumiwa, ni kampuni ya Trienex ya Afrika Kusini ambayo inamiliki asilimia 50 na Hazina (50%).

Wanahisa wengine wa kampuni hiyo inayodaiwa kuwa ilianzishwa jijini London, ni London Law Secretary Services. Ilidaiwa Bungeni kuwa kampuni ya Tangold ndiyo iliyorithi mali za Meremeta baada ya kampuni hiyo kuwa mufilisi.