MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Sunday, May 31, 2009

Hamas: Hatutautambua rasmi Mkataba wa Abbas na Israel

Phalastine

Chama cha Hamas kimetangaza kwamba hakitatambua rasmi mkataba wowote utakaofikiwa kati ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina na utawala haramu wa Israel.

Hayo yamesemwa na Fauzi Barhum, Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas.

Alisisitiza kwamba, kipindi cha urais wa Mahmoud Abbas tayari kimemalizika na kwamba hana mamlaka yoyote ya kutia saini maktaba wowote na utawala haramu wa Israel.

Barhum aliongeza kwamba Abbas pia hana mamlaka yoyote ya kuitisha kura ya maoni kuhusiana na haki za Wapalestina.

Ni vyema kukumbusha hapa kwamba, Hamas iliitaja safari ya hivi karibuni ya Abbas nchini Marekani kuwa isiyo na natija na kuongeza kwamba, Rais Barack Obama wa nchi hiyo hana uwezo wowote wa kuulazimisha utawala wa Kizayuni kuondoa mzingiro wa kidhulma unaoutekelezwa dhidi ya Ukanda wa Gaza wala kuushinikiza usimamishe ujenzi haramu wa vitongoj

Sudani: Tuko tayari kwa tishio lolote dhidi yetu

Sudan

Shirika la habari la Uchina Xinhua limeripoti kuwa Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan imeulaumu vikali utawala haramu wa Israel kutokana na juhudi zake za kuchochea mgogoro na ugomvi kati ya nchi hiyo na jirani yake Chad.

Imesema kuwa utawala huo umekuwa ukiunga mkono uchukozi wa Chad dhidi ya Sudan.

Akizungumzia suala hilo, Ali Yusuf, afisa wa ngazi za juu katika wizara hiyo amesema kuwa njama za Israel kuhusiana na suala hilo ni hatari kubwa kwa usalama na uthabit wa bara la Afrika.

Hata hivyo, amesema kuwa jeshi na vyombo vya usalama vya Sudan viko tayari kukabiliana na aina yoyote ile ya tishio dhidi ya usalama wake.

Uadui wa utawala haramu wa Israel dhidi ya Sudan unatokana na msimamo wa nchi hiyo ya Kiafrika wa kuunga mkono Wapalestina wanaonyanyaswa na utawala huo wa kibaguzi na ambao wanapitia kipindi kigumu cha mateso kutokana na juhudi za kutetea haki zao za kimsingi zilizoporwa na kukanyagwa na utawala huo haramu.

Urithi mweusi wa Bushi

Kipindi cha miaka minane ya utawala wa Rais George W. Bush wa Marekani pamoja na wenzake wa mrengo wa wahafidhina mambo-leo kinaelekea ukingoni katika hali ambayo ulimwengu unaachwa na kumbukumbu chungu ya utawala na siasa zao mbovu katika Ikulu ya White House.

Kwa kuzingatia madhara ya siasa hizo ambazo zimewaletea wanadamu machungu mengi, ulimwengu kamwe hausikitishwi na kuondoka kwao madarakani bali unaridhishwa na jambo hilo ambalo bila shaka litapunguza mivutano na vita katika pembe mbalimbali za dunia.

Tarehe nne Novemba mwaka huu wa 2008, Wamarekani walishiriki katika uchaguzi muhimu ambao uliomwondoa madarakani Rais Bush na kumfungulia Barack Obama mlango wa utawala kupitia uchaguzi huo uliomshirikisha mgombea huyo wa chama cha Democrat na John McCain wa chama tawala cha Republican.

Uchaguzi huo ulifanyika baada ya kupita miezi 20 ya kampeni kali za uchaguzi ambazo ziligharimu mabilioni ya dola za Wamarekani na kushuhudia mijadala mitatu muhimu kati ya wagombea hao.

Mbali na kampeni hizo ambazo zimepelekea kuchaguliwa Barak Obama kuwa rais wa kwanza mweusi na wa 44 katika orodha ya marais wa Marekani, lakini Wamarekani na walimwengu bado wanaathirika na madhara ya siasa mbovu za ubabe, upande mmoja na za umwagaji damu za Rais Bush pamoja na watenda jinai wenzake wa mrengo wa wahafidhina mambo-leo katika Ikulu ya White House.

Bila shaka machungu yanayowasibu walimwengu hivi sasa kutokana na siasa hizo yataendelea kushuhudiwa kwa miaka mingi ijayo.

Katika mazungumzo yake ya hivi karibuni alipokutana na shakhsia kadhaa wa kisiasa na kidini mjini Tehran, Ayatullah Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran alisisitiza kwamba ukweli mchungu unaoshuhudiwa hii leo katika pembe mbalimbali za dunia, vikiwemo vita, majanga ya njaa na ukiukwaji wa haki za binadamuu, yote hayo yanatokana na dhulma ikiwemo ya uchu wa madaraka na tamaa ya watawala.

Kwa msingi huo alisema, katika kila juhudi zinazofanywa kwa lengo la kutatua matatizo yanayoukabili ulimwengu, nara za uadilifu na mapambano dhidi ya dhulma zinapasa kuchukuliwa kuwa muhimili na nguzo muhimu.

Alisema kuwa mazungumzo na kubadilishana mawazo ni jambo zuri na la dharura na kusisitiza kuwa, jambo hilo lina nafasi muhimu katika kuleta maelewano kati ya mataifa na serikali mbalimbali. Ameongeza kwamba licha ya hayo, lakini jambo hilo pekee halitoshi kufutilia mbali sifa mbaya za madola ya kibabe na dhalimu ulimwengu wala kutatua masaibu yanayoikumba jamii ya mwanadamu, bali mambo mengine yanapasa kutiliwa maanani kuhusiana na suala hilo.

Ayatullah Khamenei aliongeza kwamba, uonevu na dhulma ndicho chanzo cha historia ya masaibu na matatizo yanayoikumba jamii ya mwanadamu. Huku akiashiria mauaji ya kinyama ambayo yamekuwa yakifanywa na Marekani pamoja pamoja na nchi nyingine za Magharibi dhidi ya watu wa Iraq, Afghanistan na Palestina, Ayatullah Khamanei aliuliza swali hili kuwa je, mauaji hayo yanatokea kutokana na kutokuwepo maelewano na kutofahamiana vyema pande mbili hizi au yanatokana na tamaa, ubabe na dhulma ya madola makubwa? Hata kama migogoro inayoendelea nchini Afghnaistan, Iraq, Palestina na mzozo wa nyuklia wa Korea Kaskazini na ule unaogharimu fedha nyingi wa Iran, mpango uliofeli eti wa Mashariki ya Kati Kuu na mivutano iliyopo kati ya Marekani na China na vilevile Russia inaweza kuchukuliwa kuwa miongoni mwa mifano ya wazi ya kufeli kwa siasa mbovu za Marekani ulimwenguni, lakini rais huyo anayeondoka madarakani anakabiliwa na matatizo mengine chungu nzima ndani ya Marekani yenyewe.


Mfano wa wazi zaidi wa matatizo hayo yanayowakabili Wamarekani hivi sasa kutokana na siasa mbovu za rais wao, ni mgogoro wa kifedha unaoendelea hivi sasa nchini humo.

Si tu kwamba mgogoro huo umewakumba Wamarekani peke yao bali na ulimwengu mzima kwa ujumla, kutokana na kuwa mifumo ya kiuchumi ya nchi nyingi ulimwenguni inafungamana na mfumo wa kifedha na kiuchumi wa Marekani. Uchumi wa nchi hiyo ndio mkubwa zaidi duniani.

Kufeli kwa siasa za Bush ndani na nje ya mipaka ya nchi hiyo hakujafumbiwa macho na Wamarekani bali siasa hizo mbovu na za kupenda vita, na hasa kuhusiana na Iraq na Afghanistan, zimekabiliwa na radiamali kali ya Wamarekani wa kawaida na vilevile wasomi na wanafikra wa masuala ya kisiasa wa nchi hiyo.

Katika maafikiano yasiyo ya kawaida ya kimitazamo, mara hii wasomi wengi wa Marekani wamekubaliana kwamba urithi wa pekee ulioachwa na Bush na wahafidhina wenzake mambo-leo, ambao wameeneza siasa za uchokozi, uharibifu, vita na umwagaji damu kote ulimwenguni unaoana kikamilifu na maana ya ibara 'urithi mweusi.'

Huku akisema kuwa mshindi wa uchaguzi wa Marekani hatapata fursa nzuri ya kutulia na kupumzika, Chas Freeman, mkuu wa kamati ya Marekani inayoshughulikia masuala ya Mashariki ya Kati anaamini kuwa, ili kubadili sura mbaya na nyeusi ya Marekani iliyoharibika duniani kutokana na siasa mbovu za Rais Bush, rais wa baadaye wa Marekani atahitaji kufanya jitihada maradufu ili kupunguza chuki na hasira iliyoenea duniani dhidi ya nchi hiyo kutokana na siasa mbovu za Bush.

Kwa mujibu wa Freeman, rais wa baadaye wa Marekani anapasa kufungua ukurasa mpya katika siasa za nje za Marekani kwa ajili ya kuwakinaisha walimwengu kwamba serikali mpya ya nchi hiyo inaheshimu sheria za kimataifa na kwamba iko tayari kurekebisha siasa nyeusi na mbovu zilizotekelezwa na Bush kuhusiana na kashfa za jela za Abu Ghuraib na Guantanamo na vilevile kurekebisha siasa hizo zilizotumika na serikali inayoondoka madarakani kwa shabaha ya kumwaga damu za watu wasio na hatia katika nchi za Iraq na Afghanistan.

Katika ripoti ya hivi karibuni kwenye mtandao wake, harakati inayopinga vita ya Anti-War iliashiria rekodi mbovu ya siasa za uingiliaji na uchokozi za serikali ya Bush dhidi ya nchi nyingine na kusema kuwa rais huyo ndiye aliyetengwa na kuchukiwa zaidi katika historia ya marais wa Marekani. Laurence Wool, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sheria cha Massachusetts nchini Marekani pia anasema kuwa Bush na serikali yake wanapasa kufikishwa mbele ya vyombo vya mahakama kuhusiana na jinai walizofanya na kuchukuliwa hatua za kisheria hata kama itakuwa na maana ya kupewa adhabu ya kifo kama watapatikana kuwa na hatia.

Francis Fukoyama, mwananadharia wa Marekani na ambaye hivi karibuni alijitenga na mrengo wa Wazayuni na Wakristo wenye misimamo ya kupindukia nchini humo pia hivi karibuni aliandika kitabu ambapo alisema kuwa, udiplomasia wa kikaoboy wa Marekani ulikuwa unaelekea ukingoni na kuituhumu serikali ya Bush kwamba imetumia vibaya madaraka.

Joseph Nay, mkuu wa zamani wa Halmashauri ya Habari za Kitaifa ya Marekani vilevile hivi karibuni aliwalinganisha marais wa Marekani na kusema kuwa Bush ndiye rais mbaya na anayechukiwa zaidi katika historia ya marais wa Marekani katika kipindi cha karne mmoja iliyopita. Amesema, katika kipindi cha utawala wake, serikali ya Bush imekuwa ikitajwa ulimwenguni kuwa serikali inayochukiwa ziadi na mataifa.

Paul Findlay, mbunge wa zamani wa Marekani katika Congress ya nchi hiyo kwa tiketi ya chama cha Republican aliandika makala ya kielimu katika gazeti la Lebanon la Daily Star ambapo alisema kwamba, serikali ya Bush ilifanya makosa makubwa na ya kipumbavu ambayo yamehatarisha usalama wa Marekani.

Seneta Joe Biden, Makamu wa Rais wa baadaye katika serikali ya Obama alisema katika mjadala wake wa televisheni wa hivi karibuni na Sara Palin ambaye alikuwa mgombea mwenza wa John McCain kwamba, hali mbaya inayotawala hivi sasa nchini Marekani inatokana na siasa mbovu za Bush.

Akizungumza hivi karibuni na televisheni ya CNN, Nancy Pelosi Spika wa Congress ya Marekani alimwita Bush kuwa msindwa mkuu na halisi wa siasa zake na kuongeza kuwa amepoteza shakhsia na itibari yake mbele ya Wamarekani, yakiwemo masuala yanayohusiana na uchumi, vita na nishati.

Katika kampeni zake za uchaguzi kabla ya kushindwa na mwenzake, Barrack Obama katika kinyang'anyiro cha kuwania urais wa Marekani, Seneta Hillary Clinton aliashiria kufeli kwa siasa za Bush katika kipindi cha miaka minane ya utawala wake nchini Marekani na kusema kuwa hatua za lazima zilipasa kuchukuliwa ili kukomesha siasa zake za kikaoboy na hivyo kupunguza madhara ya siasa hizo kwa taifa la Marekani.

Bush ambaye alijiita kuwa Kaoboy alipoingia madarakani nchini Marekani, amepitisha miaka hiyo mieusi kwa kutekeleza siasa hatari za umwagaji damu katika maeneo mengi ya dunia. Ubovu wa siasa hizo ulianza kuonekana wazi pale alipoanza kupinga wazi, na kwa mshangao wa wengi katika upeo wa kimataifa, juhudi za kimataifa za kulinda mazingira na kukabiliana na uchafuzi wa hali ya hewa duniani.

Kwa kisingizio cha kulinda viwanda vya Marekani, Bush alipinga vikali na akakataa kutia saini mkataba wa kulinda mazingira wa Kyoto Japan. Kwa mujibu wa wataalamu wa mambo, hatua hiyo imeongeza matatizo ya mazingira pamoja na kiwango cha joto duniani. Kipindi hiki cheusi cha utawala wa Bush ambacho kinamalizika kwa mgogoro wa fedha na uchumi, kinaelekea ukingoni katika hali ambayo walimwengu wanatamani kimalizike haraka ili waweze kupumzika kutokana na matatizo pamoja na mikasa kilichoandamana nayo.

Kipindi hicho mbali na kuandamana na mikasa mikubwa ikiwemo ya fedha na uchumi pamoja na uharibifu wa mazingira, kimekuwa na machungu mengine mengi ambayo yalisababishwa na siasa mbovu za Bush, vikiwemo vita vya Afghanistan ambavyo vilitekelezwa dhidi ya makundi ya Taliban na al-Qaida kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. Ni wazi kuwa vita hivyo havikuwa na natija nyingine isipokuwa kuwafaidi magaidi na kuwaletea machungu zaidi wananchi wa Afghanistan.

Hii leo, licha ya kuwepo kwa wingi askari-jeshi wa Shirika la Kujihami la Nchi za Magharibi Nato, katika ardhi ya Afghanistan na kwa uongozi wa Marekani, matatizo ya Waafghani yamekithiri na ulanguzi wa madawa ya kulevya umeongezeka maradufu. Si tu kwamba wafuasi wa makundi ya Taliban na al-Qaida wanajiimarisha zaidi, bali kwa mshangao na aibu kubwa, watawala wa kisiasa na kijeshi wa Marekani hivi sasa wanadai kwamba makundi hayo yanayochukuliwa kuwa ni ya kigaidi hayawezi kutokomezwa kwa njia za kijeshi bali, yanapaswa kushirikishwa katika mazungumzo ya amani na pia katika uendeshaji wa serikali kwa kupewa nyadhifa muhimu za wizara katika serikali hiyo!

Matamshi ya hivi karibuni ya Robert Gates, Waziri wa Ulinzi na vilevile, Condoleezza Rice, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani juu ya ulazima wa kushirikishwa serikalini makundi ya Taliban na al-Qaida na ushauri wao kwa serikali ya Hamid Karzai kuwa anapasa kuanzisha mazungumzo na makundi hayo ya kigaidi, ni ishara na tathmini kwamba njia za kijeshi dhidi ya makundi hayo hazina tena athari na kwamba njia bora ni kufanywa mazungumzo na magaidi. Kufeli kwa nadharia ya Marekani ya kutekeleza vita kwa ajili ya kuzuia mashambulio, nadharia ambayo ilitumiwa na serikali ya Bush kwa lengo la kuanzisha vita dhidi ya Iraq na kupitia propaganda chafu na kubwa za mtambo wa propaganda wa vyombo vya habari vya Marekani, hii leo ni jambo ambalo liko wazi kwa kila mtu kulishuhudia duniani.

Hadi leo Wamarekani wameshindwa kuthibitisha madai yao kwamba Iraq ilikuwa na mpango wa kutengeneza silaha za maangamizi ya umati za nyuklia na kemikali na vilevile kwamba ilikuwa na uhusiano wa moja kwa moja na mtandao wa al-Qaida, visingizio viwili vilivyotumiwa na serikali ya Bush kuanzisha hujuma kali ya kijeshi dhidi ya nchi hiyo. Kisingizio kingine kilichotolewa dhidi ya serikali ya Dikteta Saddam Hussein ni kuwa ilihusika kwa njia moja au nyingine katika mashambulio ya Septemba 11 katika miji ya New York na Washington.

Hii leo Wamarekani wameshindwa kabisa kurudisha amani na utulivu nchini Iraq na ili kuondokana na jinamizi linalowaandama kutokana na siasa zao bovu katika nchi hiyo, wanajaribu kuepuka mashinikizo yanayotolewa dhidi yao kimataifa na ndani ya Marekani yenyewe kuhusiana na jambo hilo kwa kujaribu kuwatupia wengine lawama za machafuko yanayoendelea nchini humo.

Wanajaribu kupunguza mashinikizo hayo kwa kudai kwamba nchi jirani ndizo zinazochochea machafuko katika ardhi ya Iraq au kuwashinikiza viongozi wa Iraq watie saini mkataba wa amani na serikali ya Washington ili jambo hilo liwape mwanya wa kupumua, wakidhani kwamba kuendelea kubaki kwao nchini Iraq kwa muda zaidi huenda kukawapa fursa ya kutatua matatizo ya usalama ya nchi hiyo na wakati huohuo kuwapa fursa ya kupora utajiri wa Iraq na kutekeleza malengo yao mengine haramu nchini humo.

Ni wazi kuwa hii leo siasa za upande mmoja za Marekani zimefeli kabisa na wala serikali ya Marekani haiwezi kudai kwamba Iraq ni nchi yenye uthabiti na iliyosimama kwenye misingi ya demokrasia ya kuagizwa kutoka nje. Hatua ya watawala wa nchi hiyo ya kuomba msaada wa mashirika na jumuiya za kimataifa ziingilie kati baada ya kushindwa siasa zake za upande mmoja, ni dalili ya wazi inayothibitisha kwamba jumuiya hizo sio ubao wa sataranji unaotumiwa daima na watawala wa Marekani kama muhuri wa kupitisha na kuunga mkono siasa zao za kibabe na kijuba duniani.

Mfano mwingine wa wazi wa watawala wa Marekani kutumia nguvu zao za kijeshi kama wenzo wa kufikia malengo yao haramu duniani ni mashinikizo yao dhidi ya Ethiopia kwa lengo la kupelekwa askari jeshi wake katika ardhi ya Somalia mwaka 2006. Jambo hilo kwa hakika halijakuwa na natija nyingine isipokuwa mauaji, wizi, uporaji na utumiaji mabavu dhidi ya raia wasio na hatia. Mkono mbovu wa watawala hao wapenda vita pia unaonekana wazi katika mauaji na machafuko yanayoendelea hivi sasa katika mpaka wa Pakistan na jirani yake Afghanistan, nchi ambayo imekuwa ikihesabiwa kuwa mshirika wa kwanza wa Washington katika vita vinavyodaiwa kuwa ni vya kupambana na ugaidi wa kimataifa.

Hii ni katika hali ambayo mzozo ambao unachukuliwa kuwa mkubwa zaidi katika Mashariki ya Kati, yaani suala la Palestina, ni nembo ya faili jeusi la serikali mbalimbali za Marekani na hasa utawala wa miaka minane wa Bush. Faili hilo limefumbiwa macho na kunyamaziwa kimya na Wamarekani kana kwamba halina umuhimu wowote kwao.

Miaka minane ya Bush imepita bila ya kutekelezwa ahadi za uongo za utawala huo za kusaidia kuunda serikali ya taifa huru la Palestina. Badala yake utawala huo umekuwa ukiunga mkono waziwazi jinai zinazotekelezwa na utawala haramu wa Israel dhidi ya Wapalestina wasio na hatia wala ulinzi. Kwa masikitiko makubwa, uungaji mkono na himaya ya serikali ya Washington kwa jinai za utawala huo zimeupelekea kumea pembe na kupata kiburi zaidi cha kuendelea kutekeleza jinai zake hizo dhidi ya watoto, wanawake, wazee na vijana wa Kipalestina huku ulimwengu mzima ukiwa umenyamaza kimya na kutochukua hatua yoyote ya maana kwa ajili ya kukabiliana na jinai za utawala huo.

Kufanywa mazungumzo yasiyo na natija, uungaji mkono mkubwa na usio na masharti wa serikali ya Washington kwa utawala haramu wa Israel pamoja na kupuuza haki za Wapalestina imekuwa moja ya nguzo muhimu za serikali ya Bush katika kipindi cha miaka minane iliyopita. Hii ni katika hali ambayo mzingiro wa kidhulma wa chakula, madawa na misaada ya dharura kwa Wapalestina umeimarishwa zaidi dhidi ya Wapalestina wanaoishi katika Ukanda wa Gaza. Mifano hii ni moja ya ukweli mchungu unaotawala hii leo ulimwenguni, mifano ambayo matokeo yake yanapasa kuwa funzo kwa watu wanaofuata kibubusa siasa za Marekani. Hatima ya Parviz Musharraf wa Pakistan ni mfano mzuri wa ukweli huo.

Siasa za Bush zilipata pigo jingine kubwa kwa kufichuliwa njama za serikali yake za kuzusha mgogoro wa kifedha na kiuchumi duniani. Mara hii mfumo wa kiuchumi wa Marekani umepata pigo kubwa na hata kumpelekea Bush mwenyewe kuomba msaada kutoka kwa jamii ya kimataifa ili kuiokoa nchi hiyo katika siku za mwisho za serikali yake. Kwa bahati mbaya, madhara ya mgogoro huo wa kiuchumi yamezipata pia nchi masikini ambazo zinalazimika kulipa gharama ya mgogoro huo wa Marekani.

Hata hivyo, inatarajiwa kuwa mgogoro huo wa kiuchumi na kifedha utakuwa na matokeo mazuri kwa Bush, wahafidhina mambo-leo na rais wa baadaye wa Marekani kwa kuwakumbusha kwamba wanapasa kuondoa vichwani mwao fikra kwamba wao ndio viongozi wa ulimwengu. Wakati huohuo wanapasa kutambua kwamba siasa za mabavu na kujichukulia maamuzi ya upande mmoja hazitawafikisha popote na kwamba wanawajibika kukubali na kutambua rasmi ukweli wa kuwepo nguvu za nchi nyingine duniani na hasa zile za nchi za Kiislamu.

Kwa vyovyote vile kipindi cha miaka minane ya utawala wa wahafidhina mambo-leo nchini Marekani kimemalizika na kuanza kipindi kilichojaa changamoto muhimu kwa watawala wa baadaye wa chama cha Democrat. Ulimwengu unasubiri kuona iwapo watawala hao watabadili siasa mbovu za uchokozi, ubabe na ujuba zilizotekelezwa na wenzao Warepublican au wataamua kuendelea na siasa hizo na hivyo kuvuruga zaidi amani na utulivu wa ulimwengu.

Mahakama yatetea uamuzi wa mjane kurudishwa kwenye nyumba alimofukuzwa

Ellen Manyangu na Salim Said

MAHAKAMA ya Ardhi Wilaya ya Kinondoni imetupilia mbali ombi la wakili wa mlalamikaji katika shauri la kutaka mahakama hiyo ifute agizo la mjane Shamsa Nassor wa Kiluvya kurudishwa katika nyumba alimohamishwa.

Mwenyekiti Joseph Kaare alitoa uamuzi huo jana alipokuwa akisoma hukumu ya maombi hayo yaliyowasilishwa na mlalamikaji Abdalah Malik kupitia wakili wake kutoka kampuni ya uwakili ya Rutabingwa.

Maombi hayo yaliwasilishwa mahakamani hapo yakiambatanishwa na nakala mbalimbali za hukumu zilizotolewa na mahakama za ngazi tofauti kuhusu kesi hiyo.

Nakala hizo, ambazo ni kutoka katika ngazi ya Mahakama ya mwanzo Magomeni, mahakama ya Wilaya Kinondoni na Mahakama Kuu ya Tanzania (High Court).

Kaare alithibitisha kuwa, nakala za hukumu za kesi ziliwasilishwa mahakamani hapo na wakili Rutabingwa hazihusiani na kesi ya ardhi aliyopeleka Shamsa Nassor.

Alisema, nyumba na eneo ambalo Rutabingwa aliwasilisha nyaraka zake ni la marehemu Zuwena Salum (mama mkwe wa Shamsa) ambayo msimamizi wake ni Mohammed Markbel na sio ya marehemu mume wa mjane huyo Salum Aklan.

“Amri yangu ya kumrudisha nyumbani mwake Shamsa, ambayo Rutabingwa alinitaka kuitengua haihusiani na mali zote za Zuwena wala maamuzi yoyote ya mahakama,” alisema Kaare katika hukumu ya kukataa ombi hilo na kusisitiza:

“Amri yangu ilikuwa ya kumrudisha mlalamikaji katika nyumba ya marehemu mume wake Salum Aklan, ambayo Shamsa na Alhaj Mohammed walichaguliwa kusimamia eneo na mali hiyo na mahakama ya mwanzo Kinondoni, ambapo namba ya kesi ilikuwa 55 ya mwaka 2008.”

Katika hukumu yake ambayo nakala imepatikana Kaare alisema, kwa maamuzi hayo nyumba iliyokuwa na mgogoro anayoishi mlalamikaji (Shamsa) ni ya marehemu mume wake Salum Aklan na maamuzi hayo hayajawahi kutofautishwa na maamuzi mingine yoyote.

Kwa upande wake Wakili wa Malik alikataa kuzungumza na mwandishi wa Mwananchi kwa madai kuwa hana muda.

“Sina muda wa kuzungumza na wewe kama unataka njoo ofisini,” alisema Rutabingwa ambaye pia Mwananchi ilimshuhudia akizungumza na waandishi wa baadhi ya vyombo vya habari nje ya mahakama hiyo ya Ardhi.

Baada ya hapo, Mwandishi wa habari hii alimpigia simu Malik ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Maji ya Cool Blue, Tembo Blox na Safari Kargo ili kuzungumzia kutupiliwa mbali kwa ombi lake.

“Sitaki kuzungumza katika simu, nifate ofisini, kwanza ulishindwa kunifata ofisini ukaandika uongo mtupu,” alisema Malik na kukata simu.

Hata hivyo baada ya dakika 10, Malik aliamua kumpigia simu mwandishi na kumueleza kwamba yeye hana kesi na Shamsa na kudai kuwa, mwenye kesi ni Shamsa na msimamizi wa mirathi ambaye hakumtaja jina lake.

“Usiniandike mimi sina kesi na Shamsa mwenye kesi na Shamsa ni msimamizi wa mirathi,” alijitetea Malik na kukata simu bila ya kumruhusu mwandishi kuzungumza.

Hata hivyo alipoulizwa Mohammed Markbel ambaye ni msimamizi wa mirathi ya marehemu Zuwena iwapo ana kesi na Shamsa au la, alikanusha kwa madai kuwa kesi zote zilishatolewa hukumu mahakamani.

“Mimi sina kesi na Shamsa ila tatizo lilikuwa baada ya kuteuliwa mimi kuwa msimamizi wa mirathi ya Zuwena Salum, Shamsa alikataa lakini alishindwa kwa sababu nilichaguliwa na watu watatu na yeye pekee ndiye alikataa,” alisema Markbel.

Marekani yaitoa hofu Tanzania

Salim Said

MAREKANI imesisitiza kuwa itatekeleza ahadi yake ya kuipatia Tanzania fedha kwa ajili ya miradi ya changamoto za Milenia (MCC) licha ya uchumi wake kutikisika.

Hayo yalielezwa juzi na rais Jakaya Kikwete alipokuwa akifungua harambee ya kuchangisha fedha za Mfuko wa Elimu mkoa wa Rukwa, iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Jambo la faraja kwetu ni kuwa miradi ya MCC haijaathirika na matatizo ya mtikisiko wa uchumi wa dunia nchini Marekani, wala mabadiliko ya serikali ya nchi hiyo,” alisema Rais Kikwete na kusisitiza:

“Marekani imenihakikishia kuwa fedha ya miradi hiyo bado ipo, imetengwa na iko salama. Vilevile serikali ya rais Barrack Obama, inaunga mkono mpango wa MCC na miradi yake hapa nchini, na ile yote iliyoamuliwa na rais mstaafu George Bush.”

Aidha alifafanua, fedha za barabara za ndani ya mkoa wa Rukwa zipo kupitia misaada ya Benki ya Dunia, kwa ajili ya ukarabati wa barabara ya kilomita 230 kutoka Sumbawanga hadi Mpanda.

Alizitaja barabara nyingine kuwa ni pamoja na ile ya Chala-Katongoro kilomita 87, Kilyamatunda-Muze kilomita 148 na upanuzi wa bandari ya Kusanga katika ziwa Tanganyika unaofanywa na mamlaka ya bandari.

“Nataka kuwahakikishia kuwa ni dhamira ya serikali kuchukua hatua za dhati kukabiliana ya barabara yanayoukabili mkoa wa Rukwa,” alisema rais Kikwete.

Kuhusu maendeleo ya elimu Rais Kikwete, alisema hivi sasa kata zote 2,556 nchini zina sekondari yake na kwamba nyingine zina sekondari zaidi ya moja.

“Matkeo yake ni kuongezeka kwa vijana wa kike na kiume wanaoingia sekondari kutoka 180,239 mwaka 2005 hadi 432,000 mwaka 2008,” alisema rais.

Hata hivyo alisema, maendeleo makubwa nay a haraka katika sekta ya elimu nchini yana changamoto za kupata walimu bora, maabara, vitabu na nyumba za walimu.

“Tumejipanga vyema kukabiliana na changamoto zote hizo. Nyongeza kubwa ya bajeti ya elimu ni ushahidi tosha wa kutambua wajibu wetu,” alithibitisha.

Serikali kupunguza gharama za mawasiliano

Salim Said

SERIKALI inafikiria kuangalia upya mfumo wake wa gharama za kodi kwa vyombo vya mawasiliano, ili kuwianisha gharama za mawasiliano kwa nchi zote tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha, uamuzi huo unakuja kutokana na gharama za mawasiliano nchini kuwa juu kuliko nchi nyingine.

Hatua hiyo ni katika juhudi za serikali ya Tanzania kutaka kupunguza gharama za mawasiliano nchini ili kuwianisha gharama zake za mawasiliano na zile za nchi tano za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Hayo yalisemwa jana na Waziri wa Mawasiliano Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, mara baada ya kufungua siku ya pili ya mkutano wa kuwianisha kanuni na sera za mawasiliano ya posta na simu, kwa nchi za Afrika Mashariki, uliomalizika jana, jijini Dar es Salaam.

Profesa Msolla alisema, gharama za mawasiliano nchini ziko juu zaidi kuliko nchi zote za Afrika Mashariki na Kati na kwamba tatizo ni mfumo wa kodi wa Tanzania kwa vyombo vya mawasiliano.

“Gharama za mawasiliano tanzania ziko juu kuliko nchi nyingine kwa sababu ya mfumo wa gharama za kodi kwa vyombo vya mawasiliano,” alisema Msolla.

Hata hivyo alisema, serikali ina mpango wa kuangalia upya mfumo huo wa kodi kwa ajili ya kuwianisha viwango vya gharama za mawasiliano miongoni mwa nchi zote tano za Jumuiya ya Afrika ya ashariki.

“Serikali inaandaa utaratibu wa kuangalia upya mfumo wake wa kodi hasa kwa vyombo vya mawasiliano ili viwango vya gharama za bidhaa hii viweze kufanana miongoni mwa nchi washiriki wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki,” alithibitisha Msolla.

Alisisitiza kuwa mawasiliano ni moja ya bidhaa katika soko la pamoja la Afrika ya Mashariki kwa hiyo lazima gharama zilingane kwa watumiaji wote wa mijini na vijijini.

Aidha alifafanua kuwa mkutano wa 16 wa wadhibiti na watoa huduma ya mawasiliano wa ukanda wa Afrika ya Mashariki pia ulijadili ujenzi wa mundombinu ya uhakika ya mawasiliano ili bidhaa hiyo iweze kuwafikia watu wote wa mijini na vijijini.

Aidha priofesa Msolla alisema, katika kufanikisha shirikisho la Afrika ya Mashariki lazima maudhui ya vyombo vya mawasiliano na lugha zifanane ili kulinda utamaduni wa watu wake.

“Sisi tuna lugha zetu na mila na utamaduni wetu, kwa hiyo maudhui ya vyombo vyetu vya mawasiliano lazima yange katika kulinda na kuendeleza utamaduni wetu,” alisema Msolla na kusisitiza:

“Tusiwe tunaiga na kufuata mila na tamaduni za watu, tunacho Kiswahili chetu basi tukitumie kwa manufaa ya watu wetu.”

Kwa upande wake Mshauri wa Sheria wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano ya Rwanda, Lamin Jabir alisema, serikali ya nchi yake inajitahidi kutoa ruzuku kwa watoa huduma za mawasiliano ili kuwapa nafuu watumiaji.

“Serikali yetu inajitahidi kutoa ruzuku kwa watoa huduma ya mawasiliano ili mtumiaji aweze kumudu kwa urahisi,” alisema Jabir na kusisitiza:

“Lakini pia sera, sheria na kanuni zetu ni nzuri kabisa kwa watumiaji na watoa huduma.”

Mamlaka zakutana kujadili sera,kanuni

Salim Said

MAMLAKA za Mawasiliano za nchi tano za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, zimekutana na watoa huduma za mawasiliano jijini Dar es Salaam kuoanisha sera, sheria na kanuni za mawasiliano katika nchi hizo.

Mamlaka hizo zilikutana jana katika semina iliyojali umuhimu wa kuharakisha uundaji wa Shirikisho la Afrika Mashariki.
Tayari baadhi ya asasi za shirikisho hilo zimekwishaundwa.

Akizungumza katika ufunguzi wa semina hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wa Tanzania, Dk. Naomi Katunzi, alisema katika mjadala wa kuunda soko la pamoja baina ya nchi hizo, suala la mawasiliano lilijitokeza.

“Kwa hiyo leo tupo hapa kwa ajili ya ‘kuoanisha sera, sheria na kanuni za mawasiliano miongoni mwa nchi washiriki,” alisema Dk. Katunzi na kuongeza:

“Mawasiliano na biashara ni vitu vinavyotegemeana kwa karibu, huwezi kufanya biashara na kufanikiwa bila ya kuwa na mawasiliano mazuri yanayohusisha wafanyabiashara, walaji na wadhibiti,” alisema.

Hata hivyo shirikisho hilo, linaonekana kuwa na kikwazo ambapo nchi za Kenya na Uganda zinagombania kisiwa cha utalii cha Migingo.

Katibu mkuu huyo alisema, Tanzania itakuwa kitovu cha mawasiliano kupitia Mkonga wake wa taifa wa mawasiliano na kwamba nchi hizo jirani zitaomba kuunganishwa katika mkonga huo kupitia Tanzania.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Profesa John Nkoma, alisema mkutano huo pia unawakutanisha wadhibiti na watoa huduma za mawasiliano kutoka nchi hizo.

Alisema, moja ya lengo la semina hiyo ni kujadiliana nao kuhusu namna ya kupunguza gharama za mawasiliano kwa watumiaji.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya Kanuni, Posta na Mwasiliano) Charles Njoroge wa Kenya, alisema jumuiya yake imekuwa vikikutana mara kwa mara, kujaribu kuweka utaratibu na mfumo wa mawasiliano unaofanana baina ya nchi husika.

“Tutajitahidi kuwasiliana na watoa huduma ili kuhakikisha kuwa gharama za mawasiliano katika Jumuiya ya Afrika ya Mashariki zinakuwa rahisi zaidi,” alisema Njoroge ambaye pia Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano ya Kenya.

Thursday, May 28, 2009

Mahakama ya Ardhi K'ndoni yamwokoa mjane Kiluvya

Salim Said na Ellen Manyangu

SIKU moja baada ya mjane Shamsa Nassor kuhamishwa nyumbani mwake kikatili, Kiluvya jijini Dar es Salaam, Mahakama ya Ardhi Wilaya ya Kinondoni imeamrisha mama huyo arudishwe nyumbani mwake.

Aidha, Kampuni ya Namic Auction Mart ilipewa kazi ya kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo chini ya usimamizi mkali wa Polisi kutoka Wilaya ya kipolisi Kimara.

Amri hiyo, nakala tunayo, ilitolewa jana na kusainiwa na Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi Kinondini Joseph Kaale na kukabidhiwa kwa kampuni ya Namic kwa ajili ya utekelezaji.

“Mahakama imeamrisha kwamba muombaji katika ombi hili arudishwe nyumbani mwake ambamo alitolewa bila ya sababu za msingi, haraka iwezekanavyo” alisema Kaale katika nakala ya amri hiyo.

Safari ya kwenda kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo, ilianzia Kinondoni kupitia kituo cha polisi Mbezi, ofisi ya serikali ya Mtaa Kiluvya na Mjumbe wa Shina la eneo hilo.

Ilichukua takriban masaa mawili hadi juhudi za Mkurugenzi Mtendaji wa Namic Michael Mwenda kufanikiwa kuopata asakari wawili kwa ajili ya kulinda amani na usalama wakati wa urudishwaji wa mjane huyo.

Aidha baada ya kufika eneo la tukio, askari wa Kampuni ya Ulinzi ya General na mwakilishi wa Abdallah Malik aliyejitambulisha kwa jina la Abdu Mkata waligoma kufungua lango la kuingilia licha ya askari waliotumwa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kimara (OCD) N. Ndaki.

“Mimi sipo tayari kufungua nipo tayari hata kufa, kufungwa au kukamatwa na polisi. Subirini niwasiliane na Malik au turudini kwa OCD” alisema Mkata.

“Usikubali, usikubali bora tukalale ndani kuliko kumwachia huyu mama aingie humu ndani kwa kuwa Malik hatatuelewa,” alisistiza kumueleza Mkuu wa General Guard Haroub Mbelwa.

Hata hivyo, Mwenda aliamua kuwasiliana na OCD na kumueleza kwamba amri iliyotumika kumtoa mama huyo haikufuata utaratibu na kwamba amri kumrudisha ni halali na kwa hiyo atakaekaidi atashitakiwa.

Baada ya majibizano marefu kati ya askari hao na Viongozi wa Namic hatimae waliachia ngazi bila ya kutoa funguo na wao kuamua kurudi kituo cha polisi Mbezi kwa ajili ya kumuona OCD kwa majadiliano zaidi.

Baada ya wao kuondoka uamuzi wa kuvunja kufuli na minyororo katika milango ya kuingia ndani ya eneo na nyumba ya mjane huyo ulipitishwa na kufanywa na viongozi wa Namic.

Kwa upande wake Shamsa alilishukuru sana gazeti la Mwananchi kwa kuandika habari hiyo pamoja na mahakama ya ardhi kwa kumpatia amri ya kurudishwa ndani ya nyumba yake.

“Nimefurahi sana, pia natoa shukurani zangu kwa gazeti la Mwananchi maana leo (jana) tangu asubuhi napokea simu za pole kutoka na habari hiyo. Lakini nawaomba muendele kufuatilia, serikali nayo ifuatilie ili ijue ukweli wa kesi,” alisema Shamsa na kuongeza:

“Lakini hofu yangu ni usalama na amani yangu kwa kuwa tukio hili limenitisha sana na chochote kinaweza kikanitokea kutokana na vitisho nilivyopewa na shemeji yangu Malik.”

Hadi Mwenanchi inaondoka eneo la tukio jana majira ya saa 11:05 OCD Ndaki alipiga simu na kumtaka Shamsa kuripoti Polisi Kimara kwa taratibu zaidi za kipolisi.

Shamsa alihamishwa nyumbani mwake kwa nguvu juzi na kampuni ya Yono Auction Mart, kitendo ambacho kilimsababishia hasara na majeraha mwilini.

Wednesday, May 27, 2009

TFDA yateketeza tani 34 za Maziwa hatari kutoka China

Salim Said
HATIMAYE Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imeteketeza tani 34 za maziwa ya unga aina ya Golden Bell-Instant Full Cream kutoka nchini China yenye thamani ya sh150 milioni, ambayo yamechanganywa na Kemikali aina ya ‘Melamine’.

Uteketezaji wa maziwa hayo, ulifanyika jana chini ya uangalizi mkali wa polisi wenye silaha katika Dampo la Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam eneo la Pugu Kinyamwezi.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi kabla ya uteketezaji huo, Kaimu Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula wa TFDA Raymond Wigenge alisema, Maziwa hayo yalikamatwa Septemba mwaka jana lakini yalichelewa kuteketezwa kutokana na taratibu za kimaabara baina ya mmiliki na TFDA.

Alisema, taarifa za kuwepo kwa maziwa yaliyochanganywa kemikali ya ‘Melamine’ walizipata kutoka kwa Mtandao wa Mamlaka za Udhibiti wa Usalama wa Vyakula Duniani (Inforsan) na walipofanya uchunguzi waligundua kuwapo kwa maziwa hayo nchini.

“Hatua ya kwanza baada ya kupata taarifa hiyo tulisitisha uingizaji na pili tulifanya ukaguzi nchini kote na kukamata tani nyingi za maziwa hayo. Tatu tulipeleka ‘sampo’ vigezo katika maabara za Afrika ya Kusini na za TFDA kwa ajili ya vipimo,” alisema Wigenge na kuongeza:

“Tulichukua aina 94 za bidhaa nyengine za maziwa zilizomo ndani ya soko nchini kwa ajili ya vipimo, lakini hatukubaini maziwa yaliyochanganywa ‘melamine’ zaidi ya huyo mtu mmoja ambaye alikuwa anaingiza kihalali.”

Alifafanua kuwa, Mmiliki wa maziwa hayo ambaye ni Kampuni ya Vin Mart Ltd hakuridhika na vipimo hivyo na alitaka kupelekwa vigezo vya maziwa hayo katika maabara za Ubeligiji na Ufaransa, ambako pia matokeo yake yalilingana na ya TFDA na ya Afrika ya Kusini.

“Leo ndio tumeamua kuyateketeza baada ya mmiliki kujiridhisha na vipimo vilivyofanywa katika maabara nne zikiwa ni ya TFDA, Afrika ya Kusini, Ufaransa na Ubeligiji ambako majibu yalilingana,” alisema Wigenge.

Alisema, mmiliki huyo hakuwa na kosa, kwa sababu maziwa hayo yaliingizwa kemikali hiyo kiwandani nchini China, ikiwa ni mbinu ya kuongeza virubitisho vya Protini kutokana na tabia ya wafugaji wa nchi hiyo kuweka maji katika maziwa baada ya kuyakamua.

“Kama mmiliki atataka kudai fidia kutoka kwa kampuni iliyotengeneza maziwa haya, sisi tunaweza kutoa ushirikiano kwa kuthibitisha kuwa tuliyaharibu kwa kuwa yalikuwa na kemikali yenye madhara kwa afya ya binadamu,” alisema Wigenge.

Hata hivyo Wigenge alithibitisha kuwa, mmiliki wa maziwa hayo hana kosa kwa sababu kemikali ya ‘melamine’ ambayo inasababisha ugonjwa wa figo hasa kwa watoto haikuwa kigezo cha kupima ubora wa maziwa hapo awali.

Uteketezaji huo ulifanyika chini ushuhuda wa maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), TFDA, Tume ya Ushindani wa Kibiashara (FCC), polisi, na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke.

Afisa Mkuu wa Forodha kutoka TRA Tmeke Peles Mwaipopo alisema, wao kazi yao ni kushuhudia tu na kuthibitisha kwamba uteketezaji umefanyika na si vyenginevyo.

“Baada ya hapa tutaandika ripoti kwa ajili ya kuiwasilisha kwa wakuu wetu kama kumbukumbu ili siku yoyote mmiliki akilalamika tunatoa ushahidi kuwa kitendo hicho kilifanyika,” alisema Mwaipopo.

Kwa mujibu wa sheria anayekamatwa na bidhaa bandia hupaswa kugharamia hasara yote ya uteketezaji wa bidhaa hiyo ikiwa ni pamoja na usafiri, posho za maofisa na wabebaji.

Mahakama ya Ardhi K,ndoni yamwokoa mjane Kiluvya

Salim Said na Ellen Manyangu

SIKU moja baada ya mjane Shamsa Nassor kuhamishwa nyumbani mwake kikatili, Kiluvya jijini Dar es Salaam, Mahakama ya Ardhi Wilaya ya Kinondoni imeamrisha mama huyo arudishwe nyumbani mwake.

Aidha, Kampuni ya Namic Auction Mart ilipewa kazi ya kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo chini ya usimamizi mkali wa Polisi kutoka Wilaya ya kipolisi Kimara.

Amri hiyo, nakala tunayo, ilitolewa jana na kusainiwa na Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi Kinondini Joseph Kaale na kukabidhiwa kwa kampuni ya Namic kwa ajili ya utekelezaji.

“Mahakama imeamrisha kwamba muombaji katika ombi hili arudishwe nyumbani mwake ambamo alitolewa bila ya sababu za msingi, haraka iwezekanavyo” alisema Kaale katika nakala ya amri hiyo.

Safari ya kwenda kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo, ilianzia Kinondoni kupitia kituo cha polisi Mbezi, ofisi ya serikali ya Mtaa Kiluvya na Mjumbe wa Shina la eneo hilo.

Ilichukua takriban masaa mawili hadi juhudi za Mkurugenzi Mtendaji wa Namic Michael Mwenda kufanikiwa kuopata asakari wawili kwa ajili ya kulinda amani na usalama wakati wa urudishwaji wa mjane huyo.

Aidha baada ya kufika eneo la tukio, askari wa Kampuni ya Ulinzi ya General na mwakilishi wa Abdallah Malik aliyejitambulisha kwa jina la Abdu Mkata waligoma kufungua lango la kuingilia licha ya askari waliotumwa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kimara (OCD) N. Ndaki.

“Mimi sipo tayari kufungua nipo tayari hata kufa, kufungwa au kukamatwa na polisi. Subirini niwasiliane na Malik au turudini kwa OCD” alisema Mkata.

“Usikubali, usikubali bora tukalale ndani kuliko kumwachia huyu mama aingie humu ndani kwa kuwa Malik hatatuelewa,” alisistiza kumueleza Mkuu wa General Guard Haroub Mbelwa.

Hata hivyo, Mwenda aliamua kuwasiliana na OCD na kumueleza kwamba amri iliyotumika kumtoa mama huyo haikufuata utaratibu na kwamba amri kumrudisha ni halali na kwa hiyo atakaekaidi atashitakiwa.

Baada ya majibizano marefu kati ya askari hao na Viongozi wa Namic hatimae waliachia ngazi bila ya kutoa funguo na wao kuamua kurudi kituo cha polisi Mbezi kwa ajili ya kumuona OCD kwa majadiliano zaidi.

Baada ya wao kuondoka uamuzi wa kuvunja kufuli na minyororo katika milango ya kuingia ndani ya eneo na nyumba ya mjane huyo ulipitishwa na kufanywa na viongozi wa Namic.

Kwa upande wake Shamsa alilishukuru sana gazeti la Mwananchi kwa kuandika habari hiyo pamoja na mahakama ya ardhi kwa kumpatia amri ya kurudishwa ndani ya nyumba yake.

“Nimefurahi sana, pia natoa shukurani zangu kwa gazeti la Mwananchi maana leo (jana) tangu asubuhi napokea simu za pole kutoka na habari hiyo. Lakini nawaomba muendele kufuatilia, serikali nayo ifuatilie ili ijue ukweli wa kesi,” alisema Shamsa na kuongeza:

“Lakini hofu yangu ni usalama na amani yangu kwa kuwa tukio hili limenitisha sana na chochote kinaweza kikanitokea kutokana na vitisho nilivyopewa na shemeji yangu Malik.”

Hadi Mwenanchi inaondoka eneo la tukio jana majira ya saa 11:05 OCD Ndaki alipiga simu na kumtaka Shamsa kuripoti Polisi Kimara kwa taratibu zaidi za kipolisi.

Shamsa alihamishwa nyumbani mwake kwa nguvu juzi na kampuni ya Yono Auction Mart, kitendo ambacho kilimsababishia hasara na majeraha mwilini.

Mjane ahamishwa 'kinyama Kiluvya

Salim Said
KAMPUNI ya Yono Auction Mart imeihamisha kwa nguvu familia ya Shamsa Nassor katika nyumba yake iliyopo Kiluvya Mtaa wa Gogoni, Kinondoni jijini Dar es Salaam na kasababisha hasara ya mali na kujeruhi.

Nymba hiyo ambayo ni mali ya marehemu mume wa Shamsa aitwae Salim Aklan, ilivamiwa jana na kampuni hiyo kwa madai kuwa wamepewa amri na mahakama ya mwanzo Magomeni ya kuwahamisha huku kukiwa hakuna notisi.

Akizungumza na Mwananchi mara baada ya tukio hilo lililotokea mapema asubuhi ya jana Shamsa alisema, kundi la watu zaidi ya 30 walivamia nyumba yake na kumtoa kwa nguvu yeye na watoto wake na kumsababishia hasara ya mali na majeraha ya mwili.

“Walikuja na mjumbe wa shina, wakaniambia kuwa wametumwa na mahakama, nikawaomba kabla ya kuanza kunitoa tukae chini kwanza kwa sababu wao wana nyaraka na mimi ninazo, halafu sina notisi, ndipo waliponisukuma na kuanza kuvunja vitu na kuviburuza nje,” alisimulia Shamsa huku akibubujikwa na machozi na kuongeza:

“Nilipoona hivyo nikachukua gari ili niende polisi kituo cha Kiluvya Gogoni kutoa taarifa na wakati gari liko katika mwendo wakaniwekea mtungi uliokuwa na bustani kwenye tairi na gari ilikakosa mwelekeo na kugonga mti na baadae kupinduka huku ndani nikiwa na mwanangu wa msichana.”

Alisema kutokana na ajali hiyo, wamepata majeraha yeye na mwanawe ambapo baadae alipiga simu kituo cha polisi Ostabey ambapo askari wa usalama barabarani walifika katika eneo hilo kupima ajali hiyo.

“Dhabu zangu zote zenye thamani ya 15 milioni sizioni, wameniibia saa ya aina ya Rado, fedha taslimu 5.9 milioni, wamenivunjia vitu vya jikoni, vitu vya samani na vitabu na madaftari ya shule ya watoto wangu,” alilalamika Shamsa.

Shamsa alidai kuwa, tukio hilo lilishinikizwa na shemgi yake aitwae Abdallah Malik kwa madi kuwa anataka kurithi mali hiyo kwa nguvu.

Alipoulizwa Malik kuhusiana na tukio hilo alijibu kwa jeuri na kutoa vitisho kwa mwandishi.

“Ahaa! Kama ni mwandishi andika unachojua na ukiandika vibaya likikuripukia utajijua, maana mimi nitakuchukulia hatua na wala sitokuachia,” alisema Malik na kuongeza:

“Andika tu wewe kama huyo unayemsikiliza (Shamsa) ni Bibi yako lakini litakalokufika utajua mwenyewe eneo hili lipo chini ya mahakama. Askari asiingie mtu humu, sawa.”

Mara baada ya kumalizika kazi ya kumuhamisha mama huyo, Malik alileta askari wa Kampuni ya Ulinzi ya General (General Guard) na kuwapa kazi hiyo licha ya kudai kuwa eneo hilo lipo chini ya mahakama ya Mwanzo ya Magomeni jijini Dar es Salaam.

Mkaguzi Mkuu wa Kampuni hiyo, Peter Yohana alithibitisha kuletwa hapo na Malik kwa kazi moja tu ya kuhakikisha kuwa haingii mtu ndani ya eneo hilo hata mama huyo aliyehamishwa au mtoto wake.

“Sisi tumeletwa leo (jana) asubuhi na Malik na ametutaka asiingie mtu na hata wewe kama si mwandishi usingeingia humu. Ametuthibitishia kuwa eneo hili lipo chini ya mahakama na vitu vya yule mama vyote vipo nje ya geti kule,” alisema Yohana.

Kwa upande wake mjumbe wa shina la Gogoni Kiluvya mama Mramba alisema yeye hakuwa na taarifa ya kazi hiyo na alikwenda kugongewa asubuhi wakati akichoma vitumbua vyake ili kuwasindikiza wafanyakazi wa Yono.

“Mimi nilipoona vuru nikakimbia polisi na nilipofika sijakuta hata askari mmoja nikaamua kwenda kuendelea kuchoma vitumbua vyangu kwa kuwa ndio kazi ninayoitegemea na biashara ni asubuhi,” alisema mama Mramba.

Hata hivyo Polisi Wilaya ya kipolisi Kimara ilisema haina taarifa za hamishahamisha hiyo na kwamba kitaratibu shughuli kama hizo hutakiwa kusimamiwa na polisi kwa ajili ya amani na uslama.

“Mimi sina taarifa ya tukio hilo wala sina taarifa ya amri ya mahakama kuhusu kuhamishwa kwa watu hao lakini wewe nenda mahakamani ili ujue kama ‘order’ amri ya mahakama ilitoka au la,” alisema Mkuu wa kituo cha polisi Mbezi J.K Ndaki.

Monday, May 25, 2009

DC akiri vyama vya upinzani kuimarika

Salim Said

MKUU wa Wilaya ya Makete mkoani Iringa, Hawa Ng’humbi amewataka viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kujipanga vizuri, ili kuhakikisha wanapata ushindi mkubwa katika chaguzi za serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu, kwa kuwa upinzani umekuwa mkubwa sasa.

Akizungumza mara baada ya kutawazwa kuwa Mlezi Mkuu wa Jumuiya hiyo, kata ya Mabibo jijini Dar es Salaam jana, Ng’humbi alisema matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu ndiyo utakaotoa taswira ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 nchini kote.

“Tujipange vizuri katika uchaguzi za serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka, ili kujenga mazingira ya CCM kutwaa tena dola mwakani katika uchaguzi mkuu na pia kuzuia jimbo la Ubungo lisichukuliwe na upinzani” alisema Ng’humbi.

Ng’humbi ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro kabla ya kuhamishiwa Makete, alisema upinzani kwa sasa ni mkubwa na kila chama cha upinzani kinajaribu kujiimarisha ili kuhakikisha kwamba kinashika dola.

“Ndugu zangu mimi ni mchapa kazi mzuri, nitahakikisha kwamba tunashirikiana katika kuhakikisha tunashinda uchaguzi wa serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu katika kata yetu na taifa kwa ujumla,” aliahidi Ng’humbi.

Kwa upande wake Mwenyekiti mpya wa jumuiya hiyo kata ya Mabibo Bononi Mlowe aliwataka, wanajumuiya kutokubali kurubuniwa kwa fedha na kuchaguwa wafadhili badala ya viongozi.

Alisema, watanzania wamekuwa wakichagua viongozi kwa miaka mingi lakini viongozi hao hawawajali wapiga kura wao na badala yake wanaamua kutajirisha matumbo yao.

Alisema katika awamu yake, atahakikisha kuwa anawashawishi viongozi wa jumuiya hiyo kutafuta kazi nyingine kwa ajili ya kupata fedha na kuifanya kazi ya uongozi kuwa huduma badala ya biashara.

“Wakipata kazi nyingine ya kutafutia fedha watakuwa waaminifu katika mali za chama na ada za watoto wetu, hii itatusaidia kunyanyua maendeleo na kuimarisha Chama chetu,” alisema Mlowe.

Katibu Mkuu Bakwata ashushwa madaraka

Mwandishi Wetu

MUFTI wa Tanzania sheikh Issa Shaban Simba ametengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislaam Tanzania (Bakwata) ustadhi Ally Juma Mzee na kumteua sheikh Suleiman Said kukaimu nafasi hiyo.

Mabadiliko hayo yamefanyika kimya kimya bila ya kutangazwa kabla ya Mufti Simba kusafiri kuelekea nchini Uturuki, ambako ameenda kufanya uchunguzi wa kawaida wa afya yake.

Habari ambazo Mwananchi imezipata zinasema kwamba, Mufti amechukua hatua hiyo kutokana na tuhuma za ubadhirifu wa mali za Bakwata zinazomkabili aliyekuwa Kaibu Mkuu wake ustadhi Mzee.

Utenguzi huo unafanyika wakati uchaguzi mkuu wa baraza hilo unaendelea kufanyika katika ngazi mbalimbali kuanzia Msikiti hadi taifa.

Kabla ya Mufti kufanya utenguzi huo Masheikh na waumini mkoani Arusha, walishampinga ustadhi Mzee, kuendelea kuongoza baraza hilo kwa madai kuwa hana sifa.

Kaimu Sheikh wa Wilaya ya Arusha, Mahmoud Salum, alisema katika tamko lao mara baada ya kikao kilichofanyika katika Msikiti wa Ngarenaro Arusha kuwa, kwa kauli moja wanaunga mkono mapendekezo na uamuzi wa Halmashauri ya Ulamaa Mkoa wa Arusha kumfukuza ustadhi Mzee.

''Tuhuma zilizomkabili ustadhi Mzee ni nzito, hivyo haturidhishwi na utendaji wake na pia kupewa jukumu kubwa la Katibu Mkuu wa Bakwata kwani, hana sifa stahiki,'' alisema Sheikh Salum.

Aidha, Bakwata Mkoa huo ilitoa onyo kali Mei 21 mwaka huu kwa ustadhi Mzee, ambaye sasa ni katibu wa Bakwata mkoa kwa madai anawarubuni waumini ili kuibua upya mgogoro wa kidini ambao walishaupatia ufumbuzi.

Aidha Mwananchi imebaini kuwa ustadhi Mzee anakabiliwa na tuhuma za kutumia mapato ya msikiti huo na kusababisha hasara kwa baraza.

Pamoja na uamuzi huo mzito wa Mufti bado baadhi wa maafisa wa ngazi za juu wa Bakwata hawajaridhika na wanasema licha ya Mufti kutengua uteuzi wa ustadhi Mzee na kumteua kuwa Katibu wa Mkoa wa Arusha wa baraza hilo, ni kwamba bado hajatatua tatizo.

“Tatizo la mwenzetu ni kubwa kwa sababu anakabiliwa na tuhuma za ufisadi lakini Mufti analichukulia suala kijujuu jambo ambalo ni hatari na linaweza kuligawa Bakwata,” alisema Afisa mmoja na kuongeza:

“Kwa nini waumini ambao unawaongoza wakukatae? Lazima kutakuwa na matatizo tu unachaguliwa kuwa katibu wa Mkoa wa Bakwata halafu unafukuza viongozi na kuchagua unaoona watafanyakazi kukulinda unapofanya maovu yako. Hata ukatibu wa msikiti unautaka wewe.”

“Mufti ni bora akaunda tume huru kwanza kuchunguza tuhuma za ustadhi mzee na siyo kulichukulia suala hili zito juu juu,” alisema.

Uchunguzi unaonesha kuwa Msikiti Mkuu wa mkoa wa Arusha una vitega uchumi vingi vikiwamo milango mingi ya maduka ambayo inakodishwa kwa wafanyabiashara na kuliingizia mapato Baraza.

“Sio siri bwana, mwenzetu anakabiliwa pia na tuhuma za kuuza viwanja vya Wakfu vya Bakwata, lazima watu wakukatae kwa hali hiyo,” alisema Afisa mwengine na kusisitiza:

“Mufti bado hajatatua tatizo kwa sababu ustadhi Mzee anakabiliwa na tuhuma za ufisadi Arusha na waumini wa mkoa huo wameshamkataa, halafu unamrudisha tena kuwa katibu wa mkoa, haingii akilini.”

FemAct dola imetekwa na mafisadi

Salim Sai
MTANDAO wa asasi za kiraia nchini, FemaAct, jana umeeleza kuwa dola ya Tanzania imetekwa na kundi la mafisadi.

Tamko hilo, lilosainiwa na viongozi kutoka asasi 14 za kiraia na lililowakilisha asasi 50 wanachama wa mtandao huo, lilisomwa na msemaji wa FemAct, Buberwa Kaiza mbele ya waandishi wa habari kwenye makao makuu ya Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) yaliyo Mabibo jijini Dar es Salaam.

Kaiza, ambaye anatoka taasisi ya Fordia, alisema wameamua kutoa tamko hilo kali kwa kuwa wameguswa na kuchukizwa na mwenendo wa kushughulikia matukio ya ufisadi na ukwapuaji wa mali za umma nchini, ambao unaendelea kushamiri nchini.

“Kushamiri kwa ufisadi kunabainisha jambo moja kubwa na lenye kutia shaka. Ni kwamba dola ya Tanzania tayari imetekwa na mafisadi,” alisema Bubelwa.

“Tumetathmini kwa muda mrefu na kubaini kuwa kushamiri kwa ufisadi nchini kunasababishwa na kutekwa kwa dola, sera ya uchumi wa soko holela, kutokuwepo kwa misingi endelevu ya utawala bora, ulafi wa madaraka na ubinafsi wa viongozi.”

Pia alisema kitendo cha wananchi kutodai uwajibikaji; kuendelea kutumika kwa baadhi ya sheria za kikoloni; katiba iliyopitwa na wakati na serikali kulea kundi la ‘wateule’ wasioguswa na sheria, ni ushahidi tosha wa kutekwa nyara kwa dola ya Tanzania na mafisadi wachache.

“Ushahidi mwingine wa dola kutekwa na mafisadi ni serikali na bunge kutumikia maslahi ya watu wachache; kutawala kwa rushwa kubwa; kulegalega kwa dola katika kuwachukulia hatua za haraka za kinidhamu na kisheria watuhumiwa wa ufisadi; kucheleweshwa kwa kesi za wakubwa za tuhuma za ufisadi na sheria kutumikia wachache,” alisema Bubelwa.

Bubelwa alifafanua kuwa kushamiri kwa ufisadi na sera za uchumi wa soko holela nchini kumesababisha madhara makubwa kwa Watanzania masikini.

Alisema madhara hayo pia yanasababishwa na hali ya serikali kukosa msimamo thabiti katika kutetea maslahi ya taifa.

Alisema madhara mengine ni kuyumba kwa uchumi wa taifa; utumishi wa umma kugeuzwa daraja la kujipatia utajiri; mgawanyo mbovu wa mapato ambao umesababisha pengo kubwa la kipato; kuongezeka kwa ufukara; kuporomoka kwa ubora wa huduma za jamii na ukosefu wa ajira.

Awali Bubelwa alianisha baadhi ya kashfa za ufisadi zilizotikisa nchi kuwa ni pamoja na ujenzi wa jengo la minara pacha ya Benki Kuu (BoT), wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), mikataba ya madini ya Buzwagi, Kiwira, Kagoda, Tangold, Meremeta ununuzi wa vifaa vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kufilisika kwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), ununuzi wa rada na ndege ya Rais.

HRLC Yalaani kupigwa Trafiki

Salim Said

KITUO cha Msaada wa Sheria na Haki za Binadamu nchini (HRLC) kimelani vikali kitendo cha askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kumsambulia kwa kumpiga askari wa usalama barabarani, Sajenti Thomas Mayapila akiwa kazini.

Askari hao wa JWTZ walifanya kitendo hicho, mapema wiki hii baada ya kushuka katika gari lao na kumshambulia Mayapila wakidai kuwa, aliwachelewesha kuvuka katika makutano ya barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma Ubungo jijini Dar es Salaam, walipokuwa katika msafara wao kuelekea Mbagala.

Akizungumza na Mwananchi Jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa kituo hicho, Francis Kiwanga alisema, wanalaani vikali kitendo hicho kwa kuwa ni kinyume na sheria, haki za binadamu na uraia.

“Tunalani vikali kitendo cha askari wa JWTZ kumsambulia kwa kumpiga askari wa usalama barabarani akiwa kazini, kwa sababu ni kinyume cha sheria, haki za binadamu na haki za uraia,” alisema Kiwanga.

Kiwanga aliitaka serikali kuchukua hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa wote waliohusika katika kitendo hicho kibaya haraka iwezekanavyo, ili iwe fundisho kwa wengine wenye kiburi cha namna hiyo.

“Tunaiomba serikali ichukuwe kwa haraka sana hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa wote waliohusika katika kumshambulia askari mwenzao, ili iwe fundisho kwa wengine,” alisema Kiwanga.

Alifafanua kuwa, askari wa JWTZ nchini wanajiona kuwa wako juu ya sheria na kwamba wanaweza kufanya lolote na kwa wakati wowote, jambo ambalo si kweli hata kidogo.

Alisema, kiburi cha askari wa JWTZ kinatokana na elimu ndogo ya uraia na ya haki za binadamu waliyonayo.

“Tunawaomba wakuu wa vikosi vya JWTZ watengeneze mazingara ya kuwapatia mafunzo ya elimu ya uraia na haki za binadamu askari wao kwa sababu inaoneka elimu yao ni ndogo sana,” alisema.

Alisema, kupitia utaratibu huo wataweza kupunguza kiburi cha wanajeshi na kuwafanya wananchi wa Tanzania kusalimika na kiburi hicho.

Matukio ya askari wa JWTZ kuwashambilia askari wa usalama barabarani na raia wa kawaida yamekuwa yakitokea mara kwa mara nchini, jambo ambalo limekuwa likisababisha madhara makubwa kwa wanaoshambuliwa.

Thursday, May 21, 2009

Shura ya Maimamu yamwaga misaada kwa waathirika wa mabomu Mbagala


Salim Said
SHURA ya Maimamu, walisimamia na kugawa msaada wa tani moja ya maharage, tani mbili na nusu za Sembe, nguo, chumvi na sabuni vyote vikiwa na thamani ya sh4.2 milioni kwa waathirika.

Ugawaji wa msaada huo kwa watu zaidi ya 500 bila ya kujali tofauti za kiimani, ulifanyika chini usimamizi wa Amiri wa Shura hiyo,Sheikh Mussa Kundecha katika viwanja vya Msikiti wa Taq-wa ulioathirika na milipuko ya mabomu hayo.

Akizunguza muda mfupi kabla ya kuanza kugawa msaada huo, Katibu wa Shura hiyo Sheikh Ponda Issa Ponda alisema, wameamuwa kugawa msaada huo kutokana na malalamiko yanayotolewa na walengwa kwamba haiwafikii.

Shehena ya samaki haramu yawa zigo kwa serikali

Salim Said

SERIKALI imekiri kulemewa na shehena ya tani zaidi ya 290 za samaki zilizokamatwa kwenye meli ya MV Tawariq 1 iliyokuwa ikifanya uvuvi haramu kwenye pwani ya Tanzania.

Imedaiwa kuwa samaki hao wanahifadhiwa kwa gharama ya Dola 80 za Marekani kwa tani moja kila siku na kampuni Bahari Foods Limited ya Dar es Salaam kuanzia Machi 8 mwaka huu.

Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, John Magufuli alisema juzi Dar es Salaam kuwa, gharama hizo ni mzigo kwa serikali ambayo hadi sasa haijui hatima yake.

“Ni kweli serikali inaendelea kuumia,” alisema Magufuli bila kutaja kiwango cha gharama inayolipia shehena hiyo lakini akibainisha kuwa suala hilo lipo chini ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

“Serikali inaheshimu mahakama na wala haiwezi kuingilia kazi yake, kwa hiyo mahakama ndio itakayoamua hatma ya samaki hao,” alisema Magufuli

Alieleza kushangazwa kwake na jinsi kesi hiyo inavyocheleweshwa akitolea mfano wa mahakama katika nchi zingine za Afrika ikiwamo Namibia ambako alisema kuwa hukumu za kesi za aina hiyo hazichukui siku tano

Wednesday, May 20, 2009

Mwenyekiti wa mtaa adaiwa kupandisha nauli za daladala

Salim Said

WAKAZI wa Kimara wisho na Bonyokwa jijini Dar es Salaam, wamemtuhumu Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Kimara Mwisho, Gabriel Kilave, kwa kupandisha nauli ya daladala kutoka Sh 250 bei ya serikali hadi Sh300 ambayo ni bei yake.

Nauli hiyo, inatozwa kwa kila kichwa umbali unaokadiriwa kuwa wa kilometa 3, kutoka Kimara Mwisho hadi wa Bonyokwa.

Mwenyekiti huyo, alisema Msafiri anapaswa kulipa Sh 250 kutoka Kimara Mwisho hadi vyumba vinane ambako kuna umbali wa kilometa 1.5 wakati wanaoendelea na safari hadi Bonyokwa wamekuwa wakilazimishwa kulipa Sh 300 kwa kila safari.

Wakizungunza na Mwananchi kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi hao walisema, mwenyekiti huyo na watendaji wamepandisha nauli na kwamba kila mwisho wa wiki madereva na wapiga debe wanawalipa kiasi fulani cha fedha.

“Mwenyekiti ameamua kupandisha nauli kinyume na sheria kwani anaestahili kufanya hivyo ni Mamlaka ya Usafirishaji wa Nchi Kavu na majini (Sumatra) pekee na wala si mwenyekiti wa mtaa,” alisema Hashim Juma ambaye ni mkazi wa Kimara.

Juma alisema Mwenyekiti alipandisha nauli kienyeji baada ya kupelekewa malalamiko na madereva wa daladala kuwa barabara hiyo ni mbovu na aliamua kupandisha nauli kienyeji bila kushirikisha mamlaka husika.

“Tunajua hawa madereva walikaa kikao na kuamua kwenda kuonana na uongozi wa serikali ya mtaa kwa sababu walishasema mapema suala la nauli kupanda ni lazima na leo azma hiyo, imetimia tena kwa barua iliyosainiwa na mwenyikiti,” alisema.

Naye Emmanuel Magige alisema, anashangazwa na hatua ya kupandishwa kwa nauli hiyo kiholela kwa kutumia mwamvuli wa serikali ya mtaa.

“Tunashangaa, kama yeye anataka kuwa mtu wa Sumatra si aombe kazi huko? Mbona kazi ya kusimamia hata matengenezo ya hii barabara yamemshinda na kurukia suala la kupandisha nauli kwa kuwakomoa wananchi badala ya kuwatetea?” alisema Magige.

Kilave alikiri kupandishwa kwa nauli hiyo, lakini alikanusha kuandika barua ya kuhalalisha suala hilo.

“Ni kweli tulipandisha nauli, lakini baada ya malalamiko ya makonda na madereva kuwa barabara ni mbovu. Kwanza tulikutana kwa pamoja wenyeviti wa mtaa wa Matangini, Mavurumza na madereva hao na muhutasari wa kikao upo, kabla ya kuamua kupandisha nauli” alisema Mwenyekiti huyo.

Meneja wa Uhusiano kwa Umma wa Sumatra,David Mzirai alisema, kitendo cha wenyeviti hao ni kinyume na sheria na kwamba viwango halali vya nauli ni vile vilivyopitishwa na mamlaka hiyo tu.

Tuesday, May 19, 2009

NIKO TAYARI KUJIUZULU KAMA KUNA UZEMBE WA KULIPUKA KWA MABOMU-MWINYI

Salim Said

WAZIRI wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dk. Hussein Mwinyi amekiri kuwa, atajiuzulu iwapo Baraza la Uchunguzi wa chanzo cha milipuko ya mabomu katika kambi ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Mbagala jijini Dar es Salaam, Aprili 29 mwaka huu, litagundua kuwa milipuko hiyo ilitokea kwa uzembe au ukiukwaji wa taratibu na kanuni za mfumo utendaji.

Hata hivyo Dk. Mwinyi alishusha tuhuma kwa mamlaka zinazoshughulikia ugawaji wa viwanja nchini kwa kugawa viwanja hadi karibu na maeneo ya kambi za JWTZ nchini.

Milipuko ya mabomu Mbagala iligharimu maisha ya watu karibu 30, kujeruhi mamia na kuharibu makazi ya maelfu ya watu na nyumba kadhaa za Ibada ikiwamo misikiti na makanisa.
Dk. Mwinyi aliyasema hayo jana katika mahojiano maalum na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1) kwenye kipindi chake cha ‘Jambo Tanzania’.

“Ikibainika kuwa kuna uzembe wowote wa kimfumo au kiutendaji uliosababisha kutokea kwa milipuko ya mabomu ya Mbagala, Waziri atawajibika,” alisema Dk, Mwinyi na kusisitiza:

“Milipuko ile ilikuwa ajali na wala si uzembe kwa sababu kabla ya Braza la uchunguzi kuanza kazi yake, tulishaangalia majengo yalikuwa mazima kabla ya milipuko, ukaguzi wa mabomu ulikwishafanyika na hata milipuko ilipotokea mlikuwa na watu watano.”

Awali Dk. Mwinyi alikuwa mgumu kukiri utayari wake wa kujiuzulu akisisitiza kuwa milipuko hiyo, ilikuwa ni ajali na kwamba kiongozi hapaswi kujiuzulu kwa matukio ya ajali, bali hujiuzulu kwa uzembe au ukiukwaji wa sheria, taratibu au kanuni za kiutendaji.

“Mimi naamini ile ilikuwa ajali ya kawaida na hakuna uzembe wala ukiukwaji wa taratibu, na kwa maana hiyo waziri hapaswi kujiuzulu kwa matukio ya ajali, kwa sababu kama ni hivyo ajali kila siku zinatokea na hakuna anayejiuzulu kutokana na ukweli kwamba ni vigumu kuzuia ajali,” alisema Dk. Mwinyi.

Alikiri kupata shinikizo la kujiuzulu, lakini alibeza na kusema shinikizo hilo linatoka kwa wanasiasa wa upinzani, ambao wanataka kufanya siasa hata katika sehemu na wakati wa majanga.

Aidha Dk. Minyi alisema, watu wote watano waliokuwamo katika ghala hilo la mabomu, walipoteza maisha na kwamba kuna watu wawili waliokuwapo nje akiwamo mwanajeshi mmoaja na raia mmoja, ambao watatumika kama hadidu za rejea.

Alisema, baraza la uchunguzi lililoundwa ni zuri na kwamba litatoka na chanzo sahihi cha milipuko hiyo na mapendekezo ya kujilinda ili tatizo kama hilo lisitokee tena nchini.

Kuhusu kuendelea au kutoendelea kwa makazi ya watu karibu na kambi za JWTZ dk, Mwinyi alisema, “kwa sababu tatizo kwa sasa lipo katika kambi ya Mbagala na kuna nyumba zilizobomoka, mategemeo ni kutowarudisha tena waliobolewa nyumba zao na tutaangalia mapendekezo ya kamati kuhusu ‘buffer zone’ umbali kutoka kambini na makazi ya watu, halafu tutafanya nchi nzima.”

Hata hivyo Dk. Mwinyi alikataa kutaja tarehe ya mwisho waliyopewa baraza la uchunguzi akisisitiza kuwa, “kwa sababu ni kazi ya kitaalamu tunapaswa kuwapa muda wa kutosha bila ya kuwabana, ili watoke na ripoti nzuri, lakini tuliwapa maelekezo tu kabla ya kuanza kazi kwamba, wafanye kazi haraka iwezekanavyo.”

Aidha Dk Mwinyi alisema, uvamizi wa watu katika makambi ya JWTZ ni kutokana na utendaji wa mamlaka zinashoghulikia ardhi nchini, ambapo alizitaja serikali za halamashauri na wizara ya ardhi.

Miongoni mwa athari za milipuko ya Mbagala ni tisho la baadhi ya watu kupata ulemavu wa kusikia na kuona ambapo hadi sasa zaidi ya watu 1600 wameripotiwa kuwa na matatizo hayo.