MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Wednesday, May 27, 2009

TFDA yateketeza tani 34 za Maziwa hatari kutoka China

Salim Said
HATIMAYE Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imeteketeza tani 34 za maziwa ya unga aina ya Golden Bell-Instant Full Cream kutoka nchini China yenye thamani ya sh150 milioni, ambayo yamechanganywa na Kemikali aina ya ‘Melamine’.

Uteketezaji wa maziwa hayo, ulifanyika jana chini ya uangalizi mkali wa polisi wenye silaha katika Dampo la Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam eneo la Pugu Kinyamwezi.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi kabla ya uteketezaji huo, Kaimu Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula wa TFDA Raymond Wigenge alisema, Maziwa hayo yalikamatwa Septemba mwaka jana lakini yalichelewa kuteketezwa kutokana na taratibu za kimaabara baina ya mmiliki na TFDA.

Alisema, taarifa za kuwepo kwa maziwa yaliyochanganywa kemikali ya ‘Melamine’ walizipata kutoka kwa Mtandao wa Mamlaka za Udhibiti wa Usalama wa Vyakula Duniani (Inforsan) na walipofanya uchunguzi waligundua kuwapo kwa maziwa hayo nchini.

“Hatua ya kwanza baada ya kupata taarifa hiyo tulisitisha uingizaji na pili tulifanya ukaguzi nchini kote na kukamata tani nyingi za maziwa hayo. Tatu tulipeleka ‘sampo’ vigezo katika maabara za Afrika ya Kusini na za TFDA kwa ajili ya vipimo,” alisema Wigenge na kuongeza:

“Tulichukua aina 94 za bidhaa nyengine za maziwa zilizomo ndani ya soko nchini kwa ajili ya vipimo, lakini hatukubaini maziwa yaliyochanganywa ‘melamine’ zaidi ya huyo mtu mmoja ambaye alikuwa anaingiza kihalali.”

Alifafanua kuwa, Mmiliki wa maziwa hayo ambaye ni Kampuni ya Vin Mart Ltd hakuridhika na vipimo hivyo na alitaka kupelekwa vigezo vya maziwa hayo katika maabara za Ubeligiji na Ufaransa, ambako pia matokeo yake yalilingana na ya TFDA na ya Afrika ya Kusini.

“Leo ndio tumeamua kuyateketeza baada ya mmiliki kujiridhisha na vipimo vilivyofanywa katika maabara nne zikiwa ni ya TFDA, Afrika ya Kusini, Ufaransa na Ubeligiji ambako majibu yalilingana,” alisema Wigenge.

Alisema, mmiliki huyo hakuwa na kosa, kwa sababu maziwa hayo yaliingizwa kemikali hiyo kiwandani nchini China, ikiwa ni mbinu ya kuongeza virubitisho vya Protini kutokana na tabia ya wafugaji wa nchi hiyo kuweka maji katika maziwa baada ya kuyakamua.

“Kama mmiliki atataka kudai fidia kutoka kwa kampuni iliyotengeneza maziwa haya, sisi tunaweza kutoa ushirikiano kwa kuthibitisha kuwa tuliyaharibu kwa kuwa yalikuwa na kemikali yenye madhara kwa afya ya binadamu,” alisema Wigenge.

Hata hivyo Wigenge alithibitisha kuwa, mmiliki wa maziwa hayo hana kosa kwa sababu kemikali ya ‘melamine’ ambayo inasababisha ugonjwa wa figo hasa kwa watoto haikuwa kigezo cha kupima ubora wa maziwa hapo awali.

Uteketezaji huo ulifanyika chini ushuhuda wa maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), TFDA, Tume ya Ushindani wa Kibiashara (FCC), polisi, na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke.

Afisa Mkuu wa Forodha kutoka TRA Tmeke Peles Mwaipopo alisema, wao kazi yao ni kushuhudia tu na kuthibitisha kwamba uteketezaji umefanyika na si vyenginevyo.

“Baada ya hapa tutaandika ripoti kwa ajili ya kuiwasilisha kwa wakuu wetu kama kumbukumbu ili siku yoyote mmiliki akilalamika tunatoa ushahidi kuwa kitendo hicho kilifanyika,” alisema Mwaipopo.

Kwa mujibu wa sheria anayekamatwa na bidhaa bandia hupaswa kugharamia hasara yote ya uteketezaji wa bidhaa hiyo ikiwa ni pamoja na usafiri, posho za maofisa na wabebaji.

Mahakama ya Ardhi K,ndoni yamwokoa mjane Kiluvya

Salim Said na Ellen Manyangu

SIKU moja baada ya mjane Shamsa Nassor kuhamishwa nyumbani mwake kikatili, Kiluvya jijini Dar es Salaam, Mahakama ya Ardhi Wilaya ya Kinondoni imeamrisha mama huyo arudishwe nyumbani mwake.

Aidha, Kampuni ya Namic Auction Mart ilipewa kazi ya kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo chini ya usimamizi mkali wa Polisi kutoka Wilaya ya kipolisi Kimara.

Amri hiyo, nakala tunayo, ilitolewa jana na kusainiwa na Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi Kinondini Joseph Kaale na kukabidhiwa kwa kampuni ya Namic kwa ajili ya utekelezaji.

“Mahakama imeamrisha kwamba muombaji katika ombi hili arudishwe nyumbani mwake ambamo alitolewa bila ya sababu za msingi, haraka iwezekanavyo” alisema Kaale katika nakala ya amri hiyo.

Safari ya kwenda kumrudisha nyumbani mwake mjane huyo, ilianzia Kinondoni kupitia kituo cha polisi Mbezi, ofisi ya serikali ya Mtaa Kiluvya na Mjumbe wa Shina la eneo hilo.

Ilichukua takriban masaa mawili hadi juhudi za Mkurugenzi Mtendaji wa Namic Michael Mwenda kufanikiwa kuopata asakari wawili kwa ajili ya kulinda amani na usalama wakati wa urudishwaji wa mjane huyo.

Aidha baada ya kufika eneo la tukio, askari wa Kampuni ya Ulinzi ya General na mwakilishi wa Abdallah Malik aliyejitambulisha kwa jina la Abdu Mkata waligoma kufungua lango la kuingilia licha ya askari waliotumwa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kimara (OCD) N. Ndaki.

“Mimi sipo tayari kufungua nipo tayari hata kufa, kufungwa au kukamatwa na polisi. Subirini niwasiliane na Malik au turudini kwa OCD” alisema Mkata.

“Usikubali, usikubali bora tukalale ndani kuliko kumwachia huyu mama aingie humu ndani kwa kuwa Malik hatatuelewa,” alisistiza kumueleza Mkuu wa General Guard Haroub Mbelwa.

Hata hivyo, Mwenda aliamua kuwasiliana na OCD na kumueleza kwamba amri iliyotumika kumtoa mama huyo haikufuata utaratibu na kwamba amri kumrudisha ni halali na kwa hiyo atakaekaidi atashitakiwa.

Baada ya majibizano marefu kati ya askari hao na Viongozi wa Namic hatimae waliachia ngazi bila ya kutoa funguo na wao kuamua kurudi kituo cha polisi Mbezi kwa ajili ya kumuona OCD kwa majadiliano zaidi.

Baada ya wao kuondoka uamuzi wa kuvunja kufuli na minyororo katika milango ya kuingia ndani ya eneo na nyumba ya mjane huyo ulipitishwa na kufanywa na viongozi wa Namic.

Kwa upande wake Shamsa alilishukuru sana gazeti la Mwananchi kwa kuandika habari hiyo pamoja na mahakama ya ardhi kwa kumpatia amri ya kurudishwa ndani ya nyumba yake.

“Nimefurahi sana, pia natoa shukurani zangu kwa gazeti la Mwananchi maana leo (jana) tangu asubuhi napokea simu za pole kutoka na habari hiyo. Lakini nawaomba muendele kufuatilia, serikali nayo ifuatilie ili ijue ukweli wa kesi,” alisema Shamsa na kuongeza:

“Lakini hofu yangu ni usalama na amani yangu kwa kuwa tukio hili limenitisha sana na chochote kinaweza kikanitokea kutokana na vitisho nilivyopewa na shemeji yangu Malik.”

Hadi Mwenanchi inaondoka eneo la tukio jana majira ya saa 11:05 OCD Ndaki alipiga simu na kumtaka Shamsa kuripoti Polisi Kimara kwa taratibu zaidi za kipolisi.

Shamsa alihamishwa nyumbani mwake kwa nguvu juzi na kampuni ya Yono Auction Mart, kitendo ambacho kilimsababishia hasara na majeraha mwilini.

Mjane ahamishwa 'kinyama Kiluvya

Salim Said
KAMPUNI ya Yono Auction Mart imeihamisha kwa nguvu familia ya Shamsa Nassor katika nyumba yake iliyopo Kiluvya Mtaa wa Gogoni, Kinondoni jijini Dar es Salaam na kasababisha hasara ya mali na kujeruhi.

Nymba hiyo ambayo ni mali ya marehemu mume wa Shamsa aitwae Salim Aklan, ilivamiwa jana na kampuni hiyo kwa madai kuwa wamepewa amri na mahakama ya mwanzo Magomeni ya kuwahamisha huku kukiwa hakuna notisi.

Akizungumza na Mwananchi mara baada ya tukio hilo lililotokea mapema asubuhi ya jana Shamsa alisema, kundi la watu zaidi ya 30 walivamia nyumba yake na kumtoa kwa nguvu yeye na watoto wake na kumsababishia hasara ya mali na majeraha ya mwili.

“Walikuja na mjumbe wa shina, wakaniambia kuwa wametumwa na mahakama, nikawaomba kabla ya kuanza kunitoa tukae chini kwanza kwa sababu wao wana nyaraka na mimi ninazo, halafu sina notisi, ndipo waliponisukuma na kuanza kuvunja vitu na kuviburuza nje,” alisimulia Shamsa huku akibubujikwa na machozi na kuongeza:

“Nilipoona hivyo nikachukua gari ili niende polisi kituo cha Kiluvya Gogoni kutoa taarifa na wakati gari liko katika mwendo wakaniwekea mtungi uliokuwa na bustani kwenye tairi na gari ilikakosa mwelekeo na kugonga mti na baadae kupinduka huku ndani nikiwa na mwanangu wa msichana.”

Alisema kutokana na ajali hiyo, wamepata majeraha yeye na mwanawe ambapo baadae alipiga simu kituo cha polisi Ostabey ambapo askari wa usalama barabarani walifika katika eneo hilo kupima ajali hiyo.

“Dhabu zangu zote zenye thamani ya 15 milioni sizioni, wameniibia saa ya aina ya Rado, fedha taslimu 5.9 milioni, wamenivunjia vitu vya jikoni, vitu vya samani na vitabu na madaftari ya shule ya watoto wangu,” alilalamika Shamsa.

Shamsa alidai kuwa, tukio hilo lilishinikizwa na shemgi yake aitwae Abdallah Malik kwa madi kuwa anataka kurithi mali hiyo kwa nguvu.

Alipoulizwa Malik kuhusiana na tukio hilo alijibu kwa jeuri na kutoa vitisho kwa mwandishi.

“Ahaa! Kama ni mwandishi andika unachojua na ukiandika vibaya likikuripukia utajijua, maana mimi nitakuchukulia hatua na wala sitokuachia,” alisema Malik na kuongeza:

“Andika tu wewe kama huyo unayemsikiliza (Shamsa) ni Bibi yako lakini litakalokufika utajua mwenyewe eneo hili lipo chini ya mahakama. Askari asiingie mtu humu, sawa.”

Mara baada ya kumalizika kazi ya kumuhamisha mama huyo, Malik alileta askari wa Kampuni ya Ulinzi ya General (General Guard) na kuwapa kazi hiyo licha ya kudai kuwa eneo hilo lipo chini ya mahakama ya Mwanzo ya Magomeni jijini Dar es Salaam.

Mkaguzi Mkuu wa Kampuni hiyo, Peter Yohana alithibitisha kuletwa hapo na Malik kwa kazi moja tu ya kuhakikisha kuwa haingii mtu ndani ya eneo hilo hata mama huyo aliyehamishwa au mtoto wake.

“Sisi tumeletwa leo (jana) asubuhi na Malik na ametutaka asiingie mtu na hata wewe kama si mwandishi usingeingia humu. Ametuthibitishia kuwa eneo hili lipo chini ya mahakama na vitu vya yule mama vyote vipo nje ya geti kule,” alisema Yohana.

Kwa upande wake mjumbe wa shina la Gogoni Kiluvya mama Mramba alisema yeye hakuwa na taarifa ya kazi hiyo na alikwenda kugongewa asubuhi wakati akichoma vitumbua vyake ili kuwasindikiza wafanyakazi wa Yono.

“Mimi nilipoona vuru nikakimbia polisi na nilipofika sijakuta hata askari mmoja nikaamua kwenda kuendelea kuchoma vitumbua vyangu kwa kuwa ndio kazi ninayoitegemea na biashara ni asubuhi,” alisema mama Mramba.

Hata hivyo Polisi Wilaya ya kipolisi Kimara ilisema haina taarifa za hamishahamisha hiyo na kwamba kitaratibu shughuli kama hizo hutakiwa kusimamiwa na polisi kwa ajili ya amani na uslama.

“Mimi sina taarifa ya tukio hilo wala sina taarifa ya amri ya mahakama kuhusu kuhamishwa kwa watu hao lakini wewe nenda mahakamani ili ujue kama ‘order’ amri ya mahakama ilitoka au la,” alisema Mkuu wa kituo cha polisi Mbezi J.K Ndaki.