MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Monday, May 25, 2009

DC akiri vyama vya upinzani kuimarika

Salim Said

MKUU wa Wilaya ya Makete mkoani Iringa, Hawa Ng’humbi amewataka viongozi wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kujipanga vizuri, ili kuhakikisha wanapata ushindi mkubwa katika chaguzi za serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu, kwa kuwa upinzani umekuwa mkubwa sasa.

Akizungumza mara baada ya kutawazwa kuwa Mlezi Mkuu wa Jumuiya hiyo, kata ya Mabibo jijini Dar es Salaam jana, Ng’humbi alisema matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu ndiyo utakaotoa taswira ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 nchini kote.

“Tujipange vizuri katika uchaguzi za serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka, ili kujenga mazingira ya CCM kutwaa tena dola mwakani katika uchaguzi mkuu na pia kuzuia jimbo la Ubungo lisichukuliwe na upinzani” alisema Ng’humbi.

Ng’humbi ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro kabla ya kuhamishiwa Makete, alisema upinzani kwa sasa ni mkubwa na kila chama cha upinzani kinajaribu kujiimarisha ili kuhakikisha kwamba kinashika dola.

“Ndugu zangu mimi ni mchapa kazi mzuri, nitahakikisha kwamba tunashirikiana katika kuhakikisha tunashinda uchaguzi wa serikali za mitaa mwishoni mwa mwaka huu katika kata yetu na taifa kwa ujumla,” aliahidi Ng’humbi.

Kwa upande wake Mwenyekiti mpya wa jumuiya hiyo kata ya Mabibo Bononi Mlowe aliwataka, wanajumuiya kutokubali kurubuniwa kwa fedha na kuchaguwa wafadhili badala ya viongozi.

Alisema, watanzania wamekuwa wakichagua viongozi kwa miaka mingi lakini viongozi hao hawawajali wapiga kura wao na badala yake wanaamua kutajirisha matumbo yao.

Alisema katika awamu yake, atahakikisha kuwa anawashawishi viongozi wa jumuiya hiyo kutafuta kazi nyingine kwa ajili ya kupata fedha na kuifanya kazi ya uongozi kuwa huduma badala ya biashara.

“Wakipata kazi nyingine ya kutafutia fedha watakuwa waaminifu katika mali za chama na ada za watoto wetu, hii itatusaidia kunyanyua maendeleo na kuimarisha Chama chetu,” alisema Mlowe.

Katibu Mkuu Bakwata ashushwa madaraka

Mwandishi Wetu

MUFTI wa Tanzania sheikh Issa Shaban Simba ametengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislaam Tanzania (Bakwata) ustadhi Ally Juma Mzee na kumteua sheikh Suleiman Said kukaimu nafasi hiyo.

Mabadiliko hayo yamefanyika kimya kimya bila ya kutangazwa kabla ya Mufti Simba kusafiri kuelekea nchini Uturuki, ambako ameenda kufanya uchunguzi wa kawaida wa afya yake.

Habari ambazo Mwananchi imezipata zinasema kwamba, Mufti amechukua hatua hiyo kutokana na tuhuma za ubadhirifu wa mali za Bakwata zinazomkabili aliyekuwa Kaibu Mkuu wake ustadhi Mzee.

Utenguzi huo unafanyika wakati uchaguzi mkuu wa baraza hilo unaendelea kufanyika katika ngazi mbalimbali kuanzia Msikiti hadi taifa.

Kabla ya Mufti kufanya utenguzi huo Masheikh na waumini mkoani Arusha, walishampinga ustadhi Mzee, kuendelea kuongoza baraza hilo kwa madai kuwa hana sifa.

Kaimu Sheikh wa Wilaya ya Arusha, Mahmoud Salum, alisema katika tamko lao mara baada ya kikao kilichofanyika katika Msikiti wa Ngarenaro Arusha kuwa, kwa kauli moja wanaunga mkono mapendekezo na uamuzi wa Halmashauri ya Ulamaa Mkoa wa Arusha kumfukuza ustadhi Mzee.

''Tuhuma zilizomkabili ustadhi Mzee ni nzito, hivyo haturidhishwi na utendaji wake na pia kupewa jukumu kubwa la Katibu Mkuu wa Bakwata kwani, hana sifa stahiki,'' alisema Sheikh Salum.

Aidha, Bakwata Mkoa huo ilitoa onyo kali Mei 21 mwaka huu kwa ustadhi Mzee, ambaye sasa ni katibu wa Bakwata mkoa kwa madai anawarubuni waumini ili kuibua upya mgogoro wa kidini ambao walishaupatia ufumbuzi.

Aidha Mwananchi imebaini kuwa ustadhi Mzee anakabiliwa na tuhuma za kutumia mapato ya msikiti huo na kusababisha hasara kwa baraza.

Pamoja na uamuzi huo mzito wa Mufti bado baadhi wa maafisa wa ngazi za juu wa Bakwata hawajaridhika na wanasema licha ya Mufti kutengua uteuzi wa ustadhi Mzee na kumteua kuwa Katibu wa Mkoa wa Arusha wa baraza hilo, ni kwamba bado hajatatua tatizo.

“Tatizo la mwenzetu ni kubwa kwa sababu anakabiliwa na tuhuma za ufisadi lakini Mufti analichukulia suala kijujuu jambo ambalo ni hatari na linaweza kuligawa Bakwata,” alisema Afisa mmoja na kuongeza:

“Kwa nini waumini ambao unawaongoza wakukatae? Lazima kutakuwa na matatizo tu unachaguliwa kuwa katibu wa Mkoa wa Bakwata halafu unafukuza viongozi na kuchagua unaoona watafanyakazi kukulinda unapofanya maovu yako. Hata ukatibu wa msikiti unautaka wewe.”

“Mufti ni bora akaunda tume huru kwanza kuchunguza tuhuma za ustadhi mzee na siyo kulichukulia suala hili zito juu juu,” alisema.

Uchunguzi unaonesha kuwa Msikiti Mkuu wa mkoa wa Arusha una vitega uchumi vingi vikiwamo milango mingi ya maduka ambayo inakodishwa kwa wafanyabiashara na kuliingizia mapato Baraza.

“Sio siri bwana, mwenzetu anakabiliwa pia na tuhuma za kuuza viwanja vya Wakfu vya Bakwata, lazima watu wakukatae kwa hali hiyo,” alisema Afisa mwengine na kusisitiza:

“Mufti bado hajatatua tatizo kwa sababu ustadhi Mzee anakabiliwa na tuhuma za ufisadi Arusha na waumini wa mkoa huo wameshamkataa, halafu unamrudisha tena kuwa katibu wa mkoa, haingii akilini.”

FemAct dola imetekwa na mafisadi

Salim Sai
MTANDAO wa asasi za kiraia nchini, FemaAct, jana umeeleza kuwa dola ya Tanzania imetekwa na kundi la mafisadi.

Tamko hilo, lilosainiwa na viongozi kutoka asasi 14 za kiraia na lililowakilisha asasi 50 wanachama wa mtandao huo, lilisomwa na msemaji wa FemAct, Buberwa Kaiza mbele ya waandishi wa habari kwenye makao makuu ya Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) yaliyo Mabibo jijini Dar es Salaam.

Kaiza, ambaye anatoka taasisi ya Fordia, alisema wameamua kutoa tamko hilo kali kwa kuwa wameguswa na kuchukizwa na mwenendo wa kushughulikia matukio ya ufisadi na ukwapuaji wa mali za umma nchini, ambao unaendelea kushamiri nchini.

“Kushamiri kwa ufisadi kunabainisha jambo moja kubwa na lenye kutia shaka. Ni kwamba dola ya Tanzania tayari imetekwa na mafisadi,” alisema Bubelwa.

“Tumetathmini kwa muda mrefu na kubaini kuwa kushamiri kwa ufisadi nchini kunasababishwa na kutekwa kwa dola, sera ya uchumi wa soko holela, kutokuwepo kwa misingi endelevu ya utawala bora, ulafi wa madaraka na ubinafsi wa viongozi.”

Pia alisema kitendo cha wananchi kutodai uwajibikaji; kuendelea kutumika kwa baadhi ya sheria za kikoloni; katiba iliyopitwa na wakati na serikali kulea kundi la ‘wateule’ wasioguswa na sheria, ni ushahidi tosha wa kutekwa nyara kwa dola ya Tanzania na mafisadi wachache.

“Ushahidi mwingine wa dola kutekwa na mafisadi ni serikali na bunge kutumikia maslahi ya watu wachache; kutawala kwa rushwa kubwa; kulegalega kwa dola katika kuwachukulia hatua za haraka za kinidhamu na kisheria watuhumiwa wa ufisadi; kucheleweshwa kwa kesi za wakubwa za tuhuma za ufisadi na sheria kutumikia wachache,” alisema Bubelwa.

Bubelwa alifafanua kuwa kushamiri kwa ufisadi na sera za uchumi wa soko holela nchini kumesababisha madhara makubwa kwa Watanzania masikini.

Alisema madhara hayo pia yanasababishwa na hali ya serikali kukosa msimamo thabiti katika kutetea maslahi ya taifa.

Alisema madhara mengine ni kuyumba kwa uchumi wa taifa; utumishi wa umma kugeuzwa daraja la kujipatia utajiri; mgawanyo mbovu wa mapato ambao umesababisha pengo kubwa la kipato; kuongezeka kwa ufukara; kuporomoka kwa ubora wa huduma za jamii na ukosefu wa ajira.

Awali Bubelwa alianisha baadhi ya kashfa za ufisadi zilizotikisa nchi kuwa ni pamoja na ujenzi wa jengo la minara pacha ya Benki Kuu (BoT), wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), mikataba ya madini ya Buzwagi, Kiwira, Kagoda, Tangold, Meremeta ununuzi wa vifaa vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kufilisika kwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), ununuzi wa rada na ndege ya Rais.

HRLC Yalaani kupigwa Trafiki

Salim Said

KITUO cha Msaada wa Sheria na Haki za Binadamu nchini (HRLC) kimelani vikali kitendo cha askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kumsambulia kwa kumpiga askari wa usalama barabarani, Sajenti Thomas Mayapila akiwa kazini.

Askari hao wa JWTZ walifanya kitendo hicho, mapema wiki hii baada ya kushuka katika gari lao na kumshambulia Mayapila wakidai kuwa, aliwachelewesha kuvuka katika makutano ya barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma Ubungo jijini Dar es Salaam, walipokuwa katika msafara wao kuelekea Mbagala.

Akizungumza na Mwananchi Jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa kituo hicho, Francis Kiwanga alisema, wanalaani vikali kitendo hicho kwa kuwa ni kinyume na sheria, haki za binadamu na uraia.

“Tunalani vikali kitendo cha askari wa JWTZ kumsambulia kwa kumpiga askari wa usalama barabarani akiwa kazini, kwa sababu ni kinyume cha sheria, haki za binadamu na haki za uraia,” alisema Kiwanga.

Kiwanga aliitaka serikali kuchukua hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa wote waliohusika katika kitendo hicho kibaya haraka iwezekanavyo, ili iwe fundisho kwa wengine wenye kiburi cha namna hiyo.

“Tunaiomba serikali ichukuwe kwa haraka sana hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa wote waliohusika katika kumshambulia askari mwenzao, ili iwe fundisho kwa wengine,” alisema Kiwanga.

Alifafanua kuwa, askari wa JWTZ nchini wanajiona kuwa wako juu ya sheria na kwamba wanaweza kufanya lolote na kwa wakati wowote, jambo ambalo si kweli hata kidogo.

Alisema, kiburi cha askari wa JWTZ kinatokana na elimu ndogo ya uraia na ya haki za binadamu waliyonayo.

“Tunawaomba wakuu wa vikosi vya JWTZ watengeneze mazingara ya kuwapatia mafunzo ya elimu ya uraia na haki za binadamu askari wao kwa sababu inaoneka elimu yao ni ndogo sana,” alisema.

Alisema, kupitia utaratibu huo wataweza kupunguza kiburi cha wanajeshi na kuwafanya wananchi wa Tanzania kusalimika na kiburi hicho.

Matukio ya askari wa JWTZ kuwashambilia askari wa usalama barabarani na raia wa kawaida yamekuwa yakitokea mara kwa mara nchini, jambo ambalo limekuwa likisababisha madhara makubwa kwa wanaoshambuliwa.