MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Thursday, June 25, 2009

Kampeni uchaguzi Bakwata zapamba moto

Salim Said
KAMPENI za uchaguzi wa Baraza Kuu la Waislaam Tanzania (Bakwata) katika ngazi ya Wilaya zinaendelea, huku ishara za kutokea kwa vurugu za hapa na pale zikianza kuonekana mapema.


Baadhi ya wagombea wamewashutumu wengine kuwa, wanatoa vitisho kwa lengo la kudhoofisha nguvu zao katika kampeni hizo ambazo zinatarajiwa kuishia mwishoni mwa mwezi huu.

Akizungumza na Mwananchi jijini Dar es Salaam jana, mgombea mwenyekiti wa Bakwata Wilaya ya Temeke sheikh Ali Mtulya alidai, amekuwa akitumiwa ujumbe wa vitisho kupitia simu yake ya mkononi mara kwa mara.

Alisema, wanaomtumia ujumbe huo hawajui na kila anapojaribu kupiga namba zinazotumiwa kutuma ujumbe huo, huwa hazipatikani.

“Haya hayaashirii mema katika uchaguzi huu, nimekuwa nikitumiwa meseji za vitisho na matusi kupitia simu yangu ya mkononi na kila nikijaribu kupiga simu hizo hazipatikani,” alisema sheikh Mtulya.

Sheikh Mtulya, ambaye anatetea nafasi yake ya Mwenyekiti wa Wilaya hiyo, alimshutumu sheikh Mkuu wa Bakwata Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum kuwa, amekusudia kuandaa watu kwa ajili ya kumng’oa.

Alidai, katika hotuba ya uzinduzi wa msikiti wa Bakwata Wilaya hiyo sheikh Salum alisema kuwa, atahakikisha sheikh Mtulya haingii madarakani.

“Sheikh wa Mkoa katika hotuba yake ya uzinduzi wa msikiti wa Bakwata Wilaya ya Temeke alisema kwamba, atahakikisha mimi sirudi madarakani na ataandaa watu wake kuhakikisha anatimiza azma hiyo,” alisema Sheikh Mtulya na kuongeza:

“Yeye kama sheikh wa mkoa alitakiwa kutoa hotuba nzuri ya kuhamasisha amani na utulivu katika uchaguzi wetu, badala ya kuharibu. Eti kwa sababu mimi sikumpigia kura alipogombea usheikh wa mkoa na ni kweli sikumpigia.”

Alisema, kutoka na kauli hiyo wanaandaa tamko la kulaani kauli ya sheikh Salum na baadaye wataliwasilisha Bakwata Makao Makuu.

Kwa upande wake sheikh Salum ambaye ni sheikh wa mkoa wa Dar es Salam alikiri kusema maneno hayo, lakini alidai kuwa alizungumza maneno hayo kwa utani tu na wala hayakuwa na ukweli wowote.

“Mimi yule ni shemegi yangu ametuolea, kwa hiyo mimi nilisema kama kumtania tu, kwa sababu mtu akitaka kufanya ubaya kwa mwengine hasemi bali hufanya kimya kimya,” alisema Sheikh Salum.

Alisema, kama wao wameyachukulia kweli ni upuuzi, kwa kuwa kama anataka kumfanyia ubaya hana haja ya kuandaa vijana bali angesubiri majina ya wagombea yatakapofikishwa ofisini kwake na kuliondoa jina lake.

“Lakini mimi sina ubaya na mtu yoyote, wote nimewasamehe,” alisema sheikh Salum.

Alisema, kama kuna watu wamejitokeza kupambana na sheikh Mtulya kwa kuchukua fomu wanatumia haki yao ya kidemokrasia na hawakuandaliwa na yeye.

“Kama kuna vijana wamechukua fomu, wanatumia demokrasia yao, lakini sijawandaa mimi. Na kama wanaandika tamko la kulaani ili waliwasilishe Bakwata makao makuu ni upuuzi tu,” alibeza sheikh Salum.

Kwa upande wake Afisa Habari wa Bakwata ustadh Issa Mkalinga, alithibitisha kupata malalamiko hayo kutoka kwa Sheikh Mtulia na kwamba uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika Juni 28 kwenye shule ya Sekondari ya Thaqafa Tandika jijini hapa.

Alisema, tayari wamemaliza chaguzi katika ngazi ya Msikiti na Kata kwa kiwango kikubwa nchini na kwamba sasa wanaingia katika ngazi ya Wilaya halafu Mkoa na kumalizia na Taifa.

Chadema kumpokea Lwakatare Bukoba Mjini leo

Salim Said
ALIYEKUWA Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Tanzania Bara Wilfred Lwakatare, ametangaza rasmi kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na leo anatarajiwa kupokelewa rasmi na wanachama wa chama hicho mjini Bukoba.


Baada ya kupokelewa leo, kesho Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe atampa kadi chama hicho katika hafla maalumu, itakayofanyika katika Jimbo la Biharamulo Magharibi, kabla ya kuanza kupanda majukwani kumnadi mgombea wa chama hicho katika kinyang'anyiro cha ubunge.

Lwakatare ambaye alishika nafasi ya Naibu Katibu Mkuu Bara kwa zaidi ya miaka 10, alitangaza hayo jana baada ya kupata ushauri kutoka kwa ndugu jamaa na marafiki zake.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu akiwa wilayani Bukoba, Lwakatare alisema:“Mimi ni Chadema kuanzia jana (juzi) saa 1:30 usiku, nyinyi mko nyuma sana kwa sababu taarifa hizi zimefika Ujerumani nyinyi Dar es Salam hamjapata!”

Lwakatare alitangaza kujiondoa CUF kupitia mahojiano yake ya moja kwa moja na Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani juzi saa 1:30 usiku.

Alisema uamuzi huo aliuchukua baada ya kufanya kikao na familia yake, mzazi wake na wanachama wake 284, na kuwaeleza mkasa uliomfika, wanachama 282 walimwambia aende Chadema na kwamba wanachama wawili tu walimtaka aende Chama cha Mapinduzi (CCM).

“Mzazi wangu ameniambia niende Chadema, familia pia imeniambia hivyo hivyo wanachama 282 katika kikao waliniambia ‘nenda chadema’ isipokuwa wawili walioniambia ‘nenda CCM’ kwa hiyo wengi wameshinda,” alisema Lwakatare.


Pamoja na uamuzi huo, Lwakatare aliwataka viongozi wa CUF kujifunza kwa kupitia vitabu yake kuanzia namba moja hadi tatu ambavyo amewatumia ili kurekebisha chama chao kwa kuwa si chama chake.

Alisema bado anaamini kuwa ukombozi wa Watanzania ni vyama vyote kuungana ili kujenga nguvu moja ya mapambano na CCM, na kwamba bila hivyo CCM itaendelea kutawala nchini.

“Licha ya kujiunga na Chadema niko tayari kushirikiana na CUF kwa lengo la kuunganisha nguvu ya upinzani kuing’oa CCM,” alisisitiza Lwakatare.

Naye Mwenyekiti wa CUF taifa Profesa Ibrahim Lipumba alisema amepokea taarifa hizo kwa masikitiko makubwa kwa kuwa Lwakatare alikuwa mjumbe katika Baraza Kuu la Uongozi la chama na mjumbe wa mkutano mkuu wa Taifa.

“Tunasikitika sana kwa sababu alikuwa kiongozi wetu na tulikuwa naye muda mrefu. Tulifanya mabadiliko ili kumpa muda wa kuimarisha chama lakini ameamua kufanya uamuzi huo, tunasikitika sana.

“Licha ya jitihada zangu za kuzungumza naye sana na kumsihi ameamua hivyo, mimi nilidhani tumeshaelewana na kuyamaliza kumbe ilikuwa bado. Lakini kukosa unaibu si sababu ya kuhama chama,” alisema Profesa Lipumba.

Lwakatare aliwahi kuwa mbunge wa Jimbo la Bukoba Mjini na Mwenyekiti wa Kambi ya upinzani Bungeni kupitia tiketi ya CUF na hatimaye sasa ameamu kujiunga na Chadema baada ya kuangushwa Machi mwaka huu katika nafasi yake ya unaibu Katibu Mkuu.

Wakati huohuo, aliyekuwa naibu katika mkuu wa chama cha wananchi CUF Alfred Rwakatare kesho anatarajia kujiunga rasmi na chama cha Demokrasia na maendeleo Chadema na kukabidhiwa kadi ya uanachama na mwenyekiti wa taifa wa chama hicho Freeman Mbowe.

Akizungumza na waandishi wa habari mkurugenzi wa oparesheni na uchaguzi wa Chadema John Mrema alisema kuwa Rwakatare ataingia rasmi Chadema ijumaa na kukabidhi kadi ya uanachama katika mkutano wa hadhara utakaofanyika katika uwanjwa wa Uhuru mjini Bukoba.

Mrema alisema mara baada ya Kukabidhiwa kadi hiyo na kuwa mwanachama rasmi Rwakatare atawasili jumamosi Biharaulo magharibi kwa ajili kusaidia kampeni za kumnadi mgombea wa chadema Dk. Grevas Mbassa pamoja na viopngozi wengine wa Chadema.

Aliwataja viongozi hao kuwa ni pamoja na Dk. slaa, Philimoni Ndesambulo pamoja na Zitto Kabwe ambao baada ya zoezi hilo nao pia wataingia Biharamulo kwa ajili ya kusaidia kampeni za chama chao.