MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Friday, July 24, 2009

Chadema: suluhu ya muungano ni serikali tatu

Salim Said
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema migogoro na malumbano kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar itaendelea iwapo nchi haitafuata mfumo wa serikali tatu au serikali moja.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mjadala kuhusu mambo ya Muungano huku pande zote mbili zikishutumiana mara kwa mara kama ndio chanzo cha migogoro hiyo.

Malumbano makubwa kuhusu muungano baina ya pande mbili hizo, yamezuka miezi ya karibuni baada ya kuzuka kwa tetesi kwamba kuna uwezekano wa kuwapo kwa mafuta na gesi asilia katika visiwa vya Zanzibar.

Akizungumza na Mwananchi Ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema Victor Kimesera alisema, mvutano kati ya pande mbili za muungano hautoisha iwapo mfumo wa serikali hautabadilika.

“Suluhu ya mivutano hii isiyoisha kati ya pande mbili za muungano ni kuwapo kwa serikali tatu au serikali moja tu nchini na sio serikali mbili,” alisema Kimesera.

Alisema, uwepo wa serikali mbili yaani ya Zanzibar na Muungano kunasababisha malumbano na mivutano ya mara kwa mara kati ya pande mbili za muungano huo.

“Chaguo na msimamo wa Chadema kikatiba hasa, ni kuwepo kwa serikali tatu au serikali moja nah ii ndio dawa kubwa ya malumbano na mivutano baina ya pande mbili za muungano,” alisema Kimesera.

Juzi Waziri Mkuu Mizengo Pinda alionya uwezekano wa Muungano huo kuvunjika endapo malumbano kuhusu gesi asilia na mafuta yataendelea.

Alisema baada ya muungano huo kuvunjika lazima upande mmoja wa muungano utapata shida.

Hivi karibuni Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ilitoa msimamo rasmi wa kutaka suala la mafuta na gesi asilia liondolewe katika orodha ya mambo ya Muungano.