MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Sunday, July 26, 2009

Kafulila ajitupa jimboni

Salim Said
AFISA Habari wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) David Kafulila ametangaza rasmi nia yake ya kugombea kiti cha ubunge kwenye jimbo la Kigoma Kusini katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Jimbo hilo, ambalo lipo jirani na la Kigoma Kaskazini la mbunge wa Chadema Zitto Kabwe, kwa sasa linashikiliwa na Manju Msambya kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza na Mwananchi ofisini kwake Kinondoni jijini Dar es Salaam jana, Kafulila alisema tayari ameanza harakati mbalimbali za kuhakikisha kuwa anajenga uhusiano mzuri na wananchi wa jimbo hilo pamoja na mtandao mzuri wa Chadema.

“Ya ni kweli nna nia ya kugombea ubunge wa Kigoma Kusini na nimeshaanza maandalizi tangu mwaka juzi kwa kuwasaidia wananchi katika matatizo mbalimbali yanayowakabili,” alisema Kafulila.

Alisema, jimbo la Kigoma Kusini linashikiliwa na Msambya wa CCM, lakini matatizo ya jimbo hilo yamekuwa yakizungumzwa na wabunge wa Chadema zaidi kuliko yeye aliyepewa dhamana na wananchi.

“Sasa utashangaa Msambya badala ya kuwa msemaji mkuu wa matatizo ya wananchi wa Kigoma Kusini badala yake yamekuwa yakifikishwa bungeni na wabunge wa Chadema akiwamo Zitto, Halima Mdee na Muhonga Said,” alisema Kafulila.

Alisema, anaamini kuwa kwa kushughulikia matatizo ya kijamii ya watu wa Kigoma Kusini itawafanya kuwa na imani naye pamoja na chama chake cha Chadema.

Alifafanua, katika juhudi anazofanya kuimarisha mtandao wa Chadema katika jimbo hilo, chama chake kinakusudia kupeleka Operesheni Sangara mwezi ujao.

“Jimbo lile hadi hivi sasa inaonesha kuwa limo katika mikono ya upinzani licha ya kuwa mbunge wake anatoka CCM, kwa sababu vijiji 27 vinashikiliwa na upinzani na vijiji 16 tu ndio vya chama tawala,” alisema.

Mbio za kuelekea uchaguzi mkuu wa 2010 zimeanza huku kila mwanasiasa akijiimarisha katika jimbo lake ili kuhakikisha anapata kuungwa mkono na watu wa jimbo lake.

BoT kuwabana wadanganyifu ugawaji wa mabilioni ya mtikisiko wa uchumi

Salim Said
SERIKALI imeiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kufanya mchanganuo wa kampuni 50 ambazo zitapata uhalali wa kuingia katika orodha ya kampuni zitakazofidiwa na serikali baada ya kupata hasara kubwa kutokana na athari za mtikisiko wa uchumi ulioikumba dunia kuanzia mwaka jana.

Fedha hizo ni kiasi cha sh 21.9 bilioni zilizotengwa na serikali kwa ajili ya kuwanusuru wale wote waliopata hasara kutokana na kuanguka kwa bei ya mazao katika soko la dunia kutokana na athari za mtikisiko wa kiuchumi ulioikumba dunia.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Uchumi Ramadhan Khijja aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba, tayari BoT imeanza mchakato wa kuratibu kampuni hizo, ili kuweza kupata kampuni 50 zilizoathirika sana kwa lengo la kuanza kuzipatia fidia.

“Tayari BoT inafanya mchanganuo wa kuzitambua kampuni 50 ambazo ziliathirika zaidi na mtikisiko huu, kwa kula hasara kutokana na kununua mazao kwa bei kubwa na kuyauza kwa bei ndogo, baada ya bei kushuka katika soko la dunia,” alisema Khijja mara baada ya kufungua Mkutano wa Mwaka wa Shirikisho la Wenyeviwanda Tanzania (CTI).

Alisema, mchanganuo huo yakinifu utaweza kubaini ni kampuni gani iliyoathirika sana na mtikisiko huo na ipi ambayo haikuathirika sana na mtikisiko.

“Baada ya mchanganuo wa BoT tutaweza kujua ni kampuni gani inastahiki kupata fedha hizo na ipi haistahiki ili tusijekuingia katika hasara kwa kutoa fedha kwa kampuni ambazo hazikustahiki,” alisema Khijja.

Khijja alibainisha kuwa, kuna baadhi ya kampuni ambazo zimekula hasara miaka mingi iliyopita lakini tayari kuna kampuni ambazo zimejitokeza na kujifanya kama kwamba zimekula hasara katika mtikisiko wa uchumi wa mwaka jana ili ziweze kufidiwa.

“Shilingi 21.9 bilioni ambayo imetengwa na serikali kuwafidia wafanyabiashara ni kwa wale tu ambao wamekula hasara kutokana na mtikisiko wa mwaka jana, ujanja huu tumeugundua na ndio maana serikali imeiagiza BoT kufanya uchanganuzi,” alisema Khijja.


Khiija alisema, wataziomba benki nchini kuowaongezea muda wa kurudisha mikopo baadhi ya kampuni ambazo zimepata hasara katika biashara zao kutokana na kuyumba kwa uchumi wa dunia.

Aidha alisema, serikali imeahidi kuzichukulia dhama baadhi ya kampuni ili kuweza kupata mikopo katika benki mbalimbali nchini lakini itafanya hivyo kwa zile kampuni ambazo hazina historia nzuri katika sura kibenki.

“Benki nyingi zinaingia katika hasara kutokana na kuwakopesha watu ambao hawana historia nzuri, hawajulikani mali zao, mahali wanapoishi, ufanisi wake katika biashara na hata uaminifu wake iwapo je alishawahi kukopa na kurejesha mkopo kwa wakati,” alisema Khijja na kusisitiza:

“Dhamana hii tutaoa kwa watu ambao hawajajenga historia katika benki ili kuweza kujenga wateja wazuri kwa mabenki kwa lengo la kuziondoa katika hatari ya kula hasara, halafu sisi tutasiamamia wale tuliowachukulia dhamana.”


Kwa upande wao baadhi ya wajumbe wa CTI walilaumu ukubwa serikali na gharama za uendeshaji kama ndio kikwazo kikubwa katika maendeleo ya Tanzania, huku wakihimiza miundombinu kuwa ndio njia ya mkato ya kuinua uchumi wa nchi.

Mwenyekiti wa Zamani wa CTI na Waziri Mstaafu katika serikali ya Tanzania Iddi Simba alisema, ukubwa wa serikali bado ni kikwazo katika maendeleo ya Tanzania.

“Kama tunatambua kuwa sekta ya viwanda kuwa ni injini ya uchumi wa nchi, lazima tuangalie kwa makini ukubwa wa serikali na gharama za uendeshaji wake,” alisema Simba na kusisitiza:

“Ukuaji wa uchumi wowote duniani ni matokeo ya uwekezaji, usimamiaji na matumizi sahihi ya rasilamali za nchi. Amani, ulinzi na usalama wan chi hii unaangalia ni namna gani tutapunguza au kuondoa umasikini ambao unazidi kukua siku hadi siku.”


Alisema, serikali ya Tanzania ni kubwa sana na ina matumizi makubwa hivyo kama kweli kuna nia ya kumkomboa mtanzania ni lazima serikali ipunguze ukubwa na matumizi yake.

Naye Mwenyekiti wa CTI Reginald Mengi aliipongeza serikali kwa kutenga sh1.7 trilioni kama fungu maalumu (stimulus package) kwa ajili ya kunusuru uchumi wa nchi baada ya kuyumba kutokana na mtikisiko.

“Fedha hizi ni nzuri na naipongeza serikali, lakini pekee haitoshi bali inataka kuungwa mkono kwa serikali kupunguza kodi ya bidhaa kutoka nje, kuongeza uzalishaji wa ndani kwa kutumia mali ghafi zetu, kutafuta soko la nje kwa bidhaa za ndani na serikali kutoa ruzuku,” alisema Mengi.

Aliitahadharisha serikali, kuwa makini na mafisadi katika matumizi ya fedha hizo ili ziweze kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa bila ya kufujwa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirikisho la Maendeleo ya Viwanda Vidogovidogo (Sido) Mike Laiser alilalamikia mabenki nchini kwa kutoza riba kubwa kwa wakopaji na kuweka riba ndogo kwa mtu anapoweka fedha benki.

“Ukikopa unapigwa riba kati ya asilimia 18 hadi 25 lakini wewe ukiweka fedha benki riba yake ni asilimia mbili hadi nne, hili bado ni tatizo kubwa katika maendeleo ya SMEs,” alisema Laiser.

Mtikisiko wa kiuchumi duniani ulianzia marekani mwaka 2007, baada ya mabenki ya taifa hilo kiongozi duniani kukithiri katika kutoa mikopo ya nyumba na hatimaye kufilisika.

Kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya uchumi wa Marekani na mataifa mengine hatimaye mtikisiko huo ulianza kuenea katika mataifa ya Ulaya, Asia na Afrika.

Tanzania iliathirika na mtikisiko huo katika sector za kilimo, biashara, utalii, ajira, madini, uwekezaji wan je (FDI), viwanda na nishati.