MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Thursday, July 23, 2009

Masha: kuna nini mradi wa vitambulisho vya utaifa

Salim Said na Kizitto Noya
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha amewajia juu vigogo wenzake serikalini kwa kumzuia kusimamia ipasavyo kazi ya Mradi wa Vitambulisho vya Taifa inayotarajiwa kugharimu kiasi cha Sh200 bilioni.

Akitoa majumuisho ya bajeti ya wizara yake bungeni mjini Dodoma jana, Waziri Masha alisema baadhi ya vigogo walimzuia kuhoji dosari aliyoiona katika mchakato wa zabuni ya Mradi wa Vitambulisho vya Taifa, wakati yeye ndiye waziri mwenye dhamana na wizara hiyo.

Mwanzoni mwa mwaka huu, Waziri Masha alidaiwa kumwandikia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwa kuna kigogo mmoja Ikulu (jina tunalihifadhi) alimwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupeleka taarifa ya utekelezaji wa mradi wa vitambulisho kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri.

Ilidaiwa katika malalamiko ya Masha kwa Waziri Mkuu kuwa hatua hiyo ya kigogo huyo wa Ikulu haikumridhisha (Masha) kwa madai kwamba, hakumhusisha kwa vile yeye ndiye atakayeiwasilisha taarifa hiyo kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri na ndiye atakayewajibika kwa maamuzi yoyote yatakayofanyika wizarani kwake, bila kujali kama maamuzi hayo yalipata baraka (ya kigogo huyo) au la.

Kwa mujibu wa habari ambazo ziliandikwa na vyombo vya habari na kuthibitisha na Waziri Mkuu wakati akijibu maswali ya papo kwa papo bungeni, alikiri kupokea barua ya Waziri Masha, lakini habari hizo zilivuja baada ya nyaraka kunyofolewa katika Wizara ya Mambo ya Ndani.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Masha alimwandikia Waziri Mkuu barua akimlalamikia kwa madai ya kigogo huyo kumwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani kuwasilisha taarifa hiyo kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri bila kumhusisha yeye kama Waziri.

Akiongea bungeni jana, Waziri Masha alisema wabunge wengi wamehoji mradi wa vitambulisho katika hoja tatu ambazo ni kwa nini vinachelewa, kwa nini waziri aliingilia na kwa nini halijapelekwa katika Baraza la Mawaziri.

“Mheshimiwa Naibu Spika, mheshimiwa Anna Komu ameuliza swali zuri hapa kwamba katika mradi wa vitambulisho kuna nini? Na mimi nauliza katika mradi wa vitambulisho kuna nini,” alihoji Masha.

Akizungumza huku akikariri mara kwa mara swali la kuna nini katika mradi wa vitambulisho, Waziri Masha alisema, kuna baadhi ya wabunge walimuona kafanya makosa yeye kumuhoji Katibu Mkuu na kumuandikia Waziri Mkuu kumuelezea dosari aliyoiona katika mchakato.

“Mradi upo katika mchakato, lakini baadhi ya watu hawaridhiki. Mimi niliuliza swali kwa katibu mkuu wangu, nikaambiwa nimeingilia mchakato na sina haki ya kuuliza, lakini bunge lina haki ya kunihoji mimi. Nami nauliza katika mradi huu kuna nini,” alihoji na kuongeza.

“Cha ajabu ni kwamba, mimi niliuliza ili nitakapokuja ulizwa bungeni niweze kujibu, lakini kumuuliza kwangu ilikuwa ni kosa, naambiwa hukutakiwa kuuliza. Kwa nini Bunge liniulize mimi halafu mimi nisiwe na haki ya kuuliza watendaji wangu. Hivi ndani ya mradi wa vitambulisho kuna nini?”

Waziri Masha alihoji zaidi kuwa kuna nini Watanzania na baadhi ya wabunge wasiipe muda serikali kukamilisha mradi huo, badala yake wanamtaka waziri mwenye dhamana asihoji wala kuingilia mchakato wake.

Alifafanua kuwa cha ajabu ni kwamba, kuna hoja inayotaka hata Rais na Baraza la Mawaziri hawatakiwi kupewa taarifa, huku ikisema kuwa Bunge linapaswa kujua.

“Cha ajabu kuna hoja bungeni kwamba, hata rais na baraza lake la mawaziri hawapaswi kupata taarifa za mchakato huu, lakini Bunge linapaswa kupewa taarifa, hivi kuna nini kwenye mradi huu,” alihoji Waziri Masha.

Alisema suala la mradi wa vitambulisho lipo katika mchakato na kwamba, anawaomba wabunge wampe muda kukamilisha mchakato wa zabuni ya mradi huo.

“Tumeshapokea taarifa ya PPRA (Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi), sasa tunasubiri taarifa ya Mwanasheria Mkuu wa serikali ili suala hilo lifikishwe kwa Baraza la Mawaziri. Napenda kuona kabla ya kumalizika kwa Bunge huu mradi unaanza,” alisema.

Awali Waziri Masha alilalamika kuwa asibebeshwe lawama kwa kuchelewa vitambulisho hivyo kwa kuwa suala hilo lilianza kabla hajazaliwa mwaka 1968 huku mama yake akiwa na umri wa miaka 19 tu.

Alisema, sheria ya vitambulisho hivyo ilitungwa mwaka 1986 na mwaka 1995 tenda ya kwanza ikatangazwa ambayo hata hivyo haikufanikiwa.

Alisema, mnamo mwaka 2004 upembuzi yakinifu ulifanyika na Febuari mwaka 2007 ikakubali ushauri na kuiteua kampuni ya Gotham kuwa mshauri mwelekezi wa mradi huo.

“Hapo ndipo Masha alipofahamu mradi wa vitambulisho. Kwa hiyo hata mimi nauliza kuna nini ndani ya mradi huu,” alilalamika Masha.

Alisema hadi sasa mamlaka ya kusimamia na kuratibu utoaji wa vitambulisho hivyo (NIDA) imezinduliwa, watendaji watajiriwa na kamati ya uongozi kuteuliwa na kasha kuanza kazi.

“Pia wizara imekamilisha hatua ya kwanza ya kumpata mkandarasi ambaye ataweka mfumo wa kutunza taarifa za watu watakaopewa vitambulisho,” alisema.

Kwa mujibu wa Masha, miradi hiyo inaenda sambamba na maandalizi ya utoaji zabuni ya vitambulisho hivyo yanayoendelea sasa.

“Naomba kuwathibitishia Watanzania kupitia Bunge lako tukufu kwamba, mradi wa vitambulisho utakamilika kwa kufuata sheria na utaratibu, bila mizengwe, kwa uwazi unaostahili na bila upendeleo,”alisisitiza.

Baada ya Waziri Masha kumaliza kutoa hoja alisimama mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo, (CCM) na kusema kwa jazba kuwa wanachokitaka kwa Waziri ni lini vitambulisho hivyo vitapatikana.

“Kama waziri mwenyewe hajui kinachoendelea katika wizara yake ina maana hakuna kinachoendelea, halafu anatuambia mchakato unaendelea, mchakato gani huo,” alihoji Shelukindo.

Masha alijibu, kwa kusema, “Mheshimiwa Naibu Spika narudia tena kuhoji katika mradi wa vitambulisho kuna nini? Waraka wa Baraza la Mawaziri ni siri.”

“Kuna nini katika mradi wa vitambulisho kinachawanfanya baadhi ya wabunge wasitake sisi kupata ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Nauliza tena kuna nini,” alihoji Waziri Masha kwa sauti ya chini kabisa.

Alisema, Masha ni yule yule hajabadilika, amaamini kuwa anaweza, lakini na aliuliza tena kuna nini katika mradi wa vitambulisho.

Jambo hili lilisababisha Naibu Spika Anne Makinda kusimama na kutoa ufafanuzi akisema: “Mheshimiwa waziri na mheshimiwa mbunge hapa tunasikilizwa na wananchi nchi nzima, wanachotaka kujua ni je, vitambulisho watavipata au hawatavipata? Hilo ndilo wanalohitaji na sio kuna nini”.

Waziri Masha baada ya hapo alisimama na kujibu kwa ufupi kuwa, vitambulisho hivyo vitapatikana ndani ya mwaka huu wa fedha.

“Mheshimiwa Naibu Spika, vitambulisho vitapatikana ndani ya mwaka huu wa fedha,” aliahidi.

Hata hivyo, kambi ya upinzani ilieleza wasiwasi kuhusu kukamilika kwa mradi huo, ikisema serikali imekuwa ikiahidi bila kutekeleza.

Msemaji wa kambi hiyo katika wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Ibrahin Muhammed Sanya alisema serikali imekuwa ikitoa ahadi zisizotekelezeka kuhusu suala la uraia wa nchi mbili na vitambulisho vya Uraia.

“Katika hotuba zetu za kambi miaka 2006/2007, 2007/2008 na 2008/2009, tumekuwa tukizungumzia suala la uraia wa nchi mbili, Na katika majibu ya Serikali mara zote ni kwamba mchakato unaendelea huku muda ukiyoyoma. Je, mchakato huo utamalizika lini? alihoji Sanya.

Akinukuu majibu ya serikali ya mwaka 2006 kuhusu vitambulisho vya uraia, Sanya alihoji: “Toka mwaka huo hadi sasa 2009, bado mchakato unaendelea tu. Kila siku tunaambiwa hadithi mpya kuhusiana na vitambulisho hivyo. Fedha za walipakodi zinazidi kuwaneemesha baadhi ya watu katika kadhia nzima ya vitambulisho vya uraia. Je Serikali inawatendea haki Watanzania?”

RAAWU yaingilia katia uhamishwaji watumishi NECTA

Salim Said
KATIBU Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu (RAAWU), Adelgunda Mgaya amesema uhamishaji wa wafanyakazi 70 wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta) uliofanywa na Wizara ya Elimu hivi karibuni umegubikwa na mizengwe mingi.

Hivi karibuni, wafanyakazi 70 wa Necta waliwahamishwa kutoka katika vituo vyao vya kazi na kupangiwa katika vituo vipya kwenye mikoa mbalimbali nchini.

Akizungumza na Mwananchi Ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, Mgaya alisema uhamisho huo uligubikwa na mizengwe pamoja na ukiukwaji mkubwa wa kanuni na taratibu za uhamisho wa watumishi wa umma.

Alisema, wafanyakazi hao walitakiwa kusaini barua za uhamisho wao chini ya ulinzi mkali wa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) wenye silaha, askari wa usalama wa raia na askari wa kmpuni binafsi ya ulinzi.

“Kwa kweli uhamisho ule haukuwa wa kawaida kwa sababu uligubikwa na mizengwe. Katika mazingira ya kawaida haiwezekani kumtaka mfanyakazi asaini barua ya uhamisho chini ya ulinzi mkali wa FFU tena wenye silaha,” alisema Mgaya.

“Hata wewe niambie kampuni yako ya Mwananchi inakuhamisha kikazi labda kwenda tawi la Mwanza, unakuja unasainishwa barua ya uhamisho chini ya ulinzi wa FFU wenye silaha, halafu unaambiwa ukishasaini barua uondoke hata ndani huruhusiwi kuingia, utakuwa umetendewa haki,” alihoji Mgaya.

Alisema, hivyo ndivyo walivyafanyiwa wafanyakazi 70 wa Necta, kwamba mara baada ya kusaini barua zao walitakiwa kuondoka na hawakuruhusuiwa hata kuingia ndani ya ofisi kuchukua vitu vyao.

“Unajua unapokaa katika ofisi kwa muda mrefu, huwa unaweka vitu vyako vingi, leo unamuhamisha mfanyakazi bila kumruhusu kuingia ndani na kuhamisha vitu vyake, je utakuwa umefuata taratibu za uhamisho,” alihoji.

Mgaya alisema, kwa sasa hana mengi ya kusema kwa sababu anafanya mawasiliano na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa mazungumzo zaidi kuhusiana na ukiukwaji wa kanuni katika uhamisho huo.

“Barua zile zilisainiwa na Katibu Mkuu wizarani hivyo nafanya mawasiliano naye ili tukutane anieleze kwa nini amekiuka taratibu za uhamisho, je ni kwa makusudi au alikuwa hajui,” alihoji Mgaya na kuongeza:

“Kama kutakuwa na maridhiano basi tutasema na kama hakutakuwa na maridhiano pia tutaeleza hatua gani tutachukua zaidi kutetea haki za wanachama wetu.”

Pamoja na hayo, Mgaya alisema Wizara haikuwashirikisha wao kama watetezi wa haki za wafanyakazi hao kabla ya kuwahamisha, jambo ambalo limesababisha hata kuathirika kwa Tawi la RRAWU katika ofisi za Necta.

“Kisheria kwa sababu wafanyakazi waliohamishwa wengi ni viongozi wa tawi letu pale, wizara ilitakiwa kutushirikisha ili tutafute mtu mwengine wa kumuweka badala yake lakini haikufanya hivyo,” alisema Mgaya na kuongeza:

“Jambo ambalo limedhoofisha nguvu ya tawi letu kwani ni kiongozi mmoja tu aliyebaki waliobakia wote wameingia katika uhamisho bila ya kuwa na mbadala wake.”

Kwa muda baadhi ya watendaji wa Necta wamekuwa wakilalamikiwa kutokana na kuvuja kwa mitihani ya taifa, ambapo suala la wafanyakazi kukaa katika kituo kimoja cha kazi kwa miaka mingi ikitajwa kuwa miongoni mwa sababu za kuvuja kwa mitihani hiyo.

Watu wenye ulemavu wataka misaada

Salim Said
SHIRIKISHO la Vyama vya Walemavu Tanzania (Shivyawata), limezitaka taasisi mbalimbali nchini kulitupia macho shirika hilo, kwa kuwapatia misaada badala ya kuthamini taasisi na sekta nyingine pekee.


Wito huo ulitolewa jana na Katibu Mkuu wa Shivyawata Felician Mkude alipotoa shukurani kwa baadhi ya taasisi chache zilizolipatia misaada mbalimba shirika hilo.

“Pamoja na kuzishukuru baadhi ya taasisi zilizotupatia misaada, lakini pia tunaziomba taasisi nyengine kutupia macho masuala ya watu wenye ulemavu, kwani nalo ni kundi tete lililosahaulika na linalohitaji kuwezeshwa ili kujiendesha,” alisema Mkude na kuongeza:

“Shivyawata inatoa wito kwa mashirika mbalimbali, makampuni binafsi, wizara na Idara za serikali, taasisi za dini, wafanyabiashara na watu binafsi wa ndani na nje ya nchi kuchangia kwa hali na mali, maendeleo na ustawi wa watu wenye ulemavu nchini.”

Mkude alisema, mtu mwenye ulemavu anaweza iwapo jamii itamuwezesha kwa kumuunga mkono katika juhdi zake za kutafuta maendeleo.

Alisema, Shivyawata linazipongeza taasisi zote za ndani na nje zilizojitokeza kuwasaidia kwa njia moja au nyengine, hususan mashirika ya Iternational Sustainable Cities (ISC) la Kanada, Magdala Foundation (MF) ya Madrid Hispania, na kampuni ya MMI Steel ya jijini Dar es Salaam.

Alisema, ISC iliwezesha wajasiriamali wenye ulemavu mkoani Dar es Salaam (Uwawada) kwa kuwatunishia mfuko wao wa kuweka na kukopa ambao kwa sasa umefikia miaka miwili.


Aidha MF iliwawezesha wanawake 50 wenye ulemavu kupitia Saccoss hiyo kwa kutoa fedha ambazo zitatumika kuwakopesha sh250,000 kwa awamu mbili tofauti.

“Halikadhalika kampuni ya MMI Steel, imetoa msaada wa vifaa vya kusikia kwa ajili ya watoto viziwi vyenye thamani ya milioni 15, ambavyo wamevikabidhi kwa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA),” alisema Mkude na kusisitiza:

“Vifaa hivi vitawasaidia vijana hao katika kuendeleza elimu yao hususan kwa watoto wenye ulemavu nchini.”