MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Tuesday, June 9, 2009

Tani 3.8 za dawa zilizopita muda wa matumizi zateketezwa Dar

Salim Said

MAMLAKA ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), imeteketeza tani 3.8 za dawa za Viuavijasumu (antibiotics) jamii ya ‘Pencillin’, Unga wa Sindano ya Benzathine Pencillin kutoka China, zenye thamani ya 62.6 milioni baada ya kusadikiwa kutokidhi viwango vya ubora.

Dawa hizo zilikamatwa katika maduka mbalimbali ya dawa na makazi ya mfanyabiashara mmoja wa kichina, anayefahamika kwa jina la Du Juu Zhe yaliyopo Kariakoo Jijini Dar es Salaam, kufuatia msako mkali uliofanywa na maofisa wa TFDA na Jeshi la Polisi, Machi 22 mwaka huu, baada ya kumtilia shaka.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TFDA Magreth Ndomondo, Afisa Uhusiano wa Mamlaka hyo, Gaudensia Simwanza, alisema walimuhisi Zhe kuwa anatunza dawa katika jengo lisilo na usajili wa TFDA kwa ajili ya utunzaji wa dawa, jambo ambalo ni kinyume na Sheria Nambari 1 ya Chakula, Dawa na Vipodozi ya 2003.

“Muhusika anatambuliwa na TFDA kama muingizaji wa dawa husika nchini kutoka kiwanda kilichosajiliwa cha China, lakini katika msako huu tulikamata boksi 54 zilizoisha muda wake,” alisema Simwanza.

Alisema, dawa hizo toleo nambari 0602630 na 0602631, ambazo muda wake wa matumizi ulikwishapita tangu Febuari mwaka huu, zilikuwa zimesajiliwa na TFDA kwa nambari TAN 05,208J0H SH1, ambapo katika kila katuni ilikuwa na chupa 600.

“Kutokana na mazingira ya uhifadhi wa dawa hizo kutokidhi viwango, TFDA ilifuatilia jinsi dawa hizo zilivyosambazwa na kufanikiwa kuzuiya jumla ya boksi 173 zenye uzito wa tani 3.8 na thamani ya 62,640,000,” alisema Simwanza na kuongeza:

“Tulisitisha usambazaji na matumizi yake hadi hapo tutakapojiridhisha na ubora wa dawa hizo, lakini baada ya kufanya uchunguzi wa kimaabara kwa matoleo yote mawili, tulibaini kuwa hazikutimiza viwango na hivyo tukahikisha dawa hizo zinaondoka sokoni haraka ili ziteketezwe.”

Alisema, baada ya uamuzi huo walifanya utaratibu wa kuziteketeza dawa hizo na jana wakaamua kuziteketeza katika Dampo la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam lililopo Puga Kinyamwezi.

“Leo (jana) tunateketeza dawa hizi baada ya kuhakikisha kuwa utaratibu umefuatwa ikiwa ni pamoja na vipimo na mmiliki kujiridhisha,” alisema Simwanza.

Uteketezwaji wa dawa hizo ulifanyika chini ya ulinzi mkali wa polisi wenye silaha, mgambo wa Manispaa ya Temeke, TFDA na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Mei 26 mwaka huu, TFDA iliteketeza tani 34 za maziwa ya unga aina ya Golden Bell-Instant Full Cream kutoka China yaliyokuwa na thamani ya sh150 milioni, ambayo yalichanganywa na Kemikali aina ya ‘Melamine’ ambayo ni hatari kwa afya ya binadamu.

Kwa mujibu wa Sheria nambari moja ya Chakula, Dawa na Vipodozi ya mwaka 2003, mmiliki anapaswa kugharamia gharama zote za uteketezaji wa bidhaa zitakazogundulika kuwa chini ya ubora.


Ally Mzee 'bye bye' Bakwata

Salim Said

MUFTI wa Tanzania sheikh Issa Shaban Simba, amemfukuza kazi Katibu wa Baraza Kuu la Waislaam Tanzania (Bakwata) Mkoa wa Arusha sheikh Ally Juma Mzee kufuatia tuhuma mbalimbali za ubadhirifu wa mali zinazomkabili.

Sheikh Mzee alitenguliwa katika nafasi ya Ukatibu Mkuu wa Bakwata taifa Mei mwaka huu na kuteuliwa kuwa Katibu wa baraza hilo Mkoa wa Arusha kabla ya kufukuzwa kazi.

Mabadiliko hayo ya uongozi Mkoa wa Arusha yamefanyika wakati Mufti Simba akiwa nchini Uturuki kwa ajili ya uchunguzi wa kawaida wa afya yake.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Bakwata sheikh Suleiman Lolila, aliwaarifu waislaam nchini kote kuhusu mabadiliko ya uongozi wa Bakwata Mkoa wa Arusha.

“Tunapenda kuwaarifu waislaam nchini kote mabadiliko ya uongozi wa Bakwata mkoani Arusha, ambapo Katibu wa baraza mkoa huo, sheikh Ally Juma Mzee amefukuzwa kazi na nafasi yake inachukuliwa na ustadh Abdulkarim Jonjo,” alisema sheikh Lolila na kuongeza:

“Tunawaomba waislaam nchini kote watoe ushirikiano wa hali na mali kwa Jonjo, ili tuweze kufanikisha kusogeza mbele uislaam.”

Kwa mujibu wa sheikh Lolila, sheikh Mzee kwa sasa anabakia kuwa muumini wa kawaida wa dini ya kiislaam, badala ya kushika nafasi yoyote ya uongozi wa baraza.

Aidha, sheikh Lolila alisema Mufti Simba bado yuko Ankara Uturukia katika hospitali Bingwa akiendelea na uchunguzi wa afya yake na kwamba anaendelea vizuri.

“Na hivi karibuni anakusudia kukutana na viongozi wa serikali ya nchi hiyo pamoja na viongozi mbalimbali wa taasisi za kiislaam za Uturuki, kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali ya maendeleo ya waislaam wa Tanzania likiwamo la elimu,” alisema sheikh Lolila.

Kabla ya sheikh Mzee kufukuzwa kazi Masheikh na waumini mkoani Arusha, walishampinga Mzee, kuendelea kuongoza baraza hilo kwa madai kuwa hana sifa.

Kaimu Sheikh wa Wilaya ya Arusha, Mahmoud Salum, alisema katika tamko lao mara baada ya kikao kilichofanyika katika Msikiti wa Ngarenaro Arusha kuwa, kwa kauli moja wanaunga mkono mapendekezo na uamuzi wa Halmashauri ya Ulamaa Mkoa wa Arusha kumfukuza ustadhi Mzee.

''Tuhuma zilizomkabili ustadhi Mzee ni nzito, hivyo haturidhishwi na utendaji wake na pia kupewa jukumu kubwa la Katibu Mkuu wa Bakwata kwani, hana sifa stahiki,'' alisema Sheikh Salum.

Aidha Mwananchi imebaini kuwa ustadhi Mzee anakabiliwa na tuhuma za kutumia mapato ya msikiti huo na kusababisha hasara kwa baraza.