MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Sunday, May 31, 2009

Hamas: Hatutautambua rasmi Mkataba wa Abbas na Israel

Phalastine

Chama cha Hamas kimetangaza kwamba hakitatambua rasmi mkataba wowote utakaofikiwa kati ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina na utawala haramu wa Israel.

Hayo yamesemwa na Fauzi Barhum, Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas.

Alisisitiza kwamba, kipindi cha urais wa Mahmoud Abbas tayari kimemalizika na kwamba hana mamlaka yoyote ya kutia saini maktaba wowote na utawala haramu wa Israel.

Barhum aliongeza kwamba Abbas pia hana mamlaka yoyote ya kuitisha kura ya maoni kuhusiana na haki za Wapalestina.

Ni vyema kukumbusha hapa kwamba, Hamas iliitaja safari ya hivi karibuni ya Abbas nchini Marekani kuwa isiyo na natija na kuongeza kwamba, Rais Barack Obama wa nchi hiyo hana uwezo wowote wa kuulazimisha utawala wa Kizayuni kuondoa mzingiro wa kidhulma unaoutekelezwa dhidi ya Ukanda wa Gaza wala kuushinikiza usimamishe ujenzi haramu wa vitongoj

Sudani: Tuko tayari kwa tishio lolote dhidi yetu

Sudan

Shirika la habari la Uchina Xinhua limeripoti kuwa Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan imeulaumu vikali utawala haramu wa Israel kutokana na juhudi zake za kuchochea mgogoro na ugomvi kati ya nchi hiyo na jirani yake Chad.

Imesema kuwa utawala huo umekuwa ukiunga mkono uchukozi wa Chad dhidi ya Sudan.

Akizungumzia suala hilo, Ali Yusuf, afisa wa ngazi za juu katika wizara hiyo amesema kuwa njama za Israel kuhusiana na suala hilo ni hatari kubwa kwa usalama na uthabit wa bara la Afrika.

Hata hivyo, amesema kuwa jeshi na vyombo vya usalama vya Sudan viko tayari kukabiliana na aina yoyote ile ya tishio dhidi ya usalama wake.

Uadui wa utawala haramu wa Israel dhidi ya Sudan unatokana na msimamo wa nchi hiyo ya Kiafrika wa kuunga mkono Wapalestina wanaonyanyaswa na utawala huo wa kibaguzi na ambao wanapitia kipindi kigumu cha mateso kutokana na juhudi za kutetea haki zao za kimsingi zilizoporwa na kukanyagwa na utawala huo haramu.

Urithi mweusi wa Bushi

Kipindi cha miaka minane ya utawala wa Rais George W. Bush wa Marekani pamoja na wenzake wa mrengo wa wahafidhina mambo-leo kinaelekea ukingoni katika hali ambayo ulimwengu unaachwa na kumbukumbu chungu ya utawala na siasa zao mbovu katika Ikulu ya White House.

Kwa kuzingatia madhara ya siasa hizo ambazo zimewaletea wanadamu machungu mengi, ulimwengu kamwe hausikitishwi na kuondoka kwao madarakani bali unaridhishwa na jambo hilo ambalo bila shaka litapunguza mivutano na vita katika pembe mbalimbali za dunia.

Tarehe nne Novemba mwaka huu wa 2008, Wamarekani walishiriki katika uchaguzi muhimu ambao uliomwondoa madarakani Rais Bush na kumfungulia Barack Obama mlango wa utawala kupitia uchaguzi huo uliomshirikisha mgombea huyo wa chama cha Democrat na John McCain wa chama tawala cha Republican.

Uchaguzi huo ulifanyika baada ya kupita miezi 20 ya kampeni kali za uchaguzi ambazo ziligharimu mabilioni ya dola za Wamarekani na kushuhudia mijadala mitatu muhimu kati ya wagombea hao.

Mbali na kampeni hizo ambazo zimepelekea kuchaguliwa Barak Obama kuwa rais wa kwanza mweusi na wa 44 katika orodha ya marais wa Marekani, lakini Wamarekani na walimwengu bado wanaathirika na madhara ya siasa mbovu za ubabe, upande mmoja na za umwagaji damu za Rais Bush pamoja na watenda jinai wenzake wa mrengo wa wahafidhina mambo-leo katika Ikulu ya White House.

Bila shaka machungu yanayowasibu walimwengu hivi sasa kutokana na siasa hizo yataendelea kushuhudiwa kwa miaka mingi ijayo.

Katika mazungumzo yake ya hivi karibuni alipokutana na shakhsia kadhaa wa kisiasa na kidini mjini Tehran, Ayatullah Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran alisisitiza kwamba ukweli mchungu unaoshuhudiwa hii leo katika pembe mbalimbali za dunia, vikiwemo vita, majanga ya njaa na ukiukwaji wa haki za binadamuu, yote hayo yanatokana na dhulma ikiwemo ya uchu wa madaraka na tamaa ya watawala.

Kwa msingi huo alisema, katika kila juhudi zinazofanywa kwa lengo la kutatua matatizo yanayoukabili ulimwengu, nara za uadilifu na mapambano dhidi ya dhulma zinapasa kuchukuliwa kuwa muhimili na nguzo muhimu.

Alisema kuwa mazungumzo na kubadilishana mawazo ni jambo zuri na la dharura na kusisitiza kuwa, jambo hilo lina nafasi muhimu katika kuleta maelewano kati ya mataifa na serikali mbalimbali. Ameongeza kwamba licha ya hayo, lakini jambo hilo pekee halitoshi kufutilia mbali sifa mbaya za madola ya kibabe na dhalimu ulimwengu wala kutatua masaibu yanayoikumba jamii ya mwanadamu, bali mambo mengine yanapasa kutiliwa maanani kuhusiana na suala hilo.

Ayatullah Khamenei aliongeza kwamba, uonevu na dhulma ndicho chanzo cha historia ya masaibu na matatizo yanayoikumba jamii ya mwanadamu. Huku akiashiria mauaji ya kinyama ambayo yamekuwa yakifanywa na Marekani pamoja pamoja na nchi nyingine za Magharibi dhidi ya watu wa Iraq, Afghanistan na Palestina, Ayatullah Khamanei aliuliza swali hili kuwa je, mauaji hayo yanatokea kutokana na kutokuwepo maelewano na kutofahamiana vyema pande mbili hizi au yanatokana na tamaa, ubabe na dhulma ya madola makubwa? Hata kama migogoro inayoendelea nchini Afghnaistan, Iraq, Palestina na mzozo wa nyuklia wa Korea Kaskazini na ule unaogharimu fedha nyingi wa Iran, mpango uliofeli eti wa Mashariki ya Kati Kuu na mivutano iliyopo kati ya Marekani na China na vilevile Russia inaweza kuchukuliwa kuwa miongoni mwa mifano ya wazi ya kufeli kwa siasa mbovu za Marekani ulimwenguni, lakini rais huyo anayeondoka madarakani anakabiliwa na matatizo mengine chungu nzima ndani ya Marekani yenyewe.


Mfano wa wazi zaidi wa matatizo hayo yanayowakabili Wamarekani hivi sasa kutokana na siasa mbovu za rais wao, ni mgogoro wa kifedha unaoendelea hivi sasa nchini humo.

Si tu kwamba mgogoro huo umewakumba Wamarekani peke yao bali na ulimwengu mzima kwa ujumla, kutokana na kuwa mifumo ya kiuchumi ya nchi nyingi ulimwenguni inafungamana na mfumo wa kifedha na kiuchumi wa Marekani. Uchumi wa nchi hiyo ndio mkubwa zaidi duniani.

Kufeli kwa siasa za Bush ndani na nje ya mipaka ya nchi hiyo hakujafumbiwa macho na Wamarekani bali siasa hizo mbovu na za kupenda vita, na hasa kuhusiana na Iraq na Afghanistan, zimekabiliwa na radiamali kali ya Wamarekani wa kawaida na vilevile wasomi na wanafikra wa masuala ya kisiasa wa nchi hiyo.

Katika maafikiano yasiyo ya kawaida ya kimitazamo, mara hii wasomi wengi wa Marekani wamekubaliana kwamba urithi wa pekee ulioachwa na Bush na wahafidhina wenzake mambo-leo, ambao wameeneza siasa za uchokozi, uharibifu, vita na umwagaji damu kote ulimwenguni unaoana kikamilifu na maana ya ibara 'urithi mweusi.'

Huku akisema kuwa mshindi wa uchaguzi wa Marekani hatapata fursa nzuri ya kutulia na kupumzika, Chas Freeman, mkuu wa kamati ya Marekani inayoshughulikia masuala ya Mashariki ya Kati anaamini kuwa, ili kubadili sura mbaya na nyeusi ya Marekani iliyoharibika duniani kutokana na siasa mbovu za Rais Bush, rais wa baadaye wa Marekani atahitaji kufanya jitihada maradufu ili kupunguza chuki na hasira iliyoenea duniani dhidi ya nchi hiyo kutokana na siasa mbovu za Bush.

Kwa mujibu wa Freeman, rais wa baadaye wa Marekani anapasa kufungua ukurasa mpya katika siasa za nje za Marekani kwa ajili ya kuwakinaisha walimwengu kwamba serikali mpya ya nchi hiyo inaheshimu sheria za kimataifa na kwamba iko tayari kurekebisha siasa nyeusi na mbovu zilizotekelezwa na Bush kuhusiana na kashfa za jela za Abu Ghuraib na Guantanamo na vilevile kurekebisha siasa hizo zilizotumika na serikali inayoondoka madarakani kwa shabaha ya kumwaga damu za watu wasio na hatia katika nchi za Iraq na Afghanistan.

Katika ripoti ya hivi karibuni kwenye mtandao wake, harakati inayopinga vita ya Anti-War iliashiria rekodi mbovu ya siasa za uingiliaji na uchokozi za serikali ya Bush dhidi ya nchi nyingine na kusema kuwa rais huyo ndiye aliyetengwa na kuchukiwa zaidi katika historia ya marais wa Marekani. Laurence Wool, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sheria cha Massachusetts nchini Marekani pia anasema kuwa Bush na serikali yake wanapasa kufikishwa mbele ya vyombo vya mahakama kuhusiana na jinai walizofanya na kuchukuliwa hatua za kisheria hata kama itakuwa na maana ya kupewa adhabu ya kifo kama watapatikana kuwa na hatia.

Francis Fukoyama, mwananadharia wa Marekani na ambaye hivi karibuni alijitenga na mrengo wa Wazayuni na Wakristo wenye misimamo ya kupindukia nchini humo pia hivi karibuni aliandika kitabu ambapo alisema kuwa, udiplomasia wa kikaoboy wa Marekani ulikuwa unaelekea ukingoni na kuituhumu serikali ya Bush kwamba imetumia vibaya madaraka.

Joseph Nay, mkuu wa zamani wa Halmashauri ya Habari za Kitaifa ya Marekani vilevile hivi karibuni aliwalinganisha marais wa Marekani na kusema kuwa Bush ndiye rais mbaya na anayechukiwa zaidi katika historia ya marais wa Marekani katika kipindi cha karne mmoja iliyopita. Amesema, katika kipindi cha utawala wake, serikali ya Bush imekuwa ikitajwa ulimwenguni kuwa serikali inayochukiwa ziadi na mataifa.

Paul Findlay, mbunge wa zamani wa Marekani katika Congress ya nchi hiyo kwa tiketi ya chama cha Republican aliandika makala ya kielimu katika gazeti la Lebanon la Daily Star ambapo alisema kwamba, serikali ya Bush ilifanya makosa makubwa na ya kipumbavu ambayo yamehatarisha usalama wa Marekani.

Seneta Joe Biden, Makamu wa Rais wa baadaye katika serikali ya Obama alisema katika mjadala wake wa televisheni wa hivi karibuni na Sara Palin ambaye alikuwa mgombea mwenza wa John McCain kwamba, hali mbaya inayotawala hivi sasa nchini Marekani inatokana na siasa mbovu za Bush.

Akizungumza hivi karibuni na televisheni ya CNN, Nancy Pelosi Spika wa Congress ya Marekani alimwita Bush kuwa msindwa mkuu na halisi wa siasa zake na kuongeza kuwa amepoteza shakhsia na itibari yake mbele ya Wamarekani, yakiwemo masuala yanayohusiana na uchumi, vita na nishati.

Katika kampeni zake za uchaguzi kabla ya kushindwa na mwenzake, Barrack Obama katika kinyang'anyiro cha kuwania urais wa Marekani, Seneta Hillary Clinton aliashiria kufeli kwa siasa za Bush katika kipindi cha miaka minane ya utawala wake nchini Marekani na kusema kuwa hatua za lazima zilipasa kuchukuliwa ili kukomesha siasa zake za kikaoboy na hivyo kupunguza madhara ya siasa hizo kwa taifa la Marekani.

Bush ambaye alijiita kuwa Kaoboy alipoingia madarakani nchini Marekani, amepitisha miaka hiyo mieusi kwa kutekeleza siasa hatari za umwagaji damu katika maeneo mengi ya dunia. Ubovu wa siasa hizo ulianza kuonekana wazi pale alipoanza kupinga wazi, na kwa mshangao wa wengi katika upeo wa kimataifa, juhudi za kimataifa za kulinda mazingira na kukabiliana na uchafuzi wa hali ya hewa duniani.

Kwa kisingizio cha kulinda viwanda vya Marekani, Bush alipinga vikali na akakataa kutia saini mkataba wa kulinda mazingira wa Kyoto Japan. Kwa mujibu wa wataalamu wa mambo, hatua hiyo imeongeza matatizo ya mazingira pamoja na kiwango cha joto duniani. Kipindi hiki cheusi cha utawala wa Bush ambacho kinamalizika kwa mgogoro wa fedha na uchumi, kinaelekea ukingoni katika hali ambayo walimwengu wanatamani kimalizike haraka ili waweze kupumzika kutokana na matatizo pamoja na mikasa kilichoandamana nayo.

Kipindi hicho mbali na kuandamana na mikasa mikubwa ikiwemo ya fedha na uchumi pamoja na uharibifu wa mazingira, kimekuwa na machungu mengine mengi ambayo yalisababishwa na siasa mbovu za Bush, vikiwemo vita vya Afghanistan ambavyo vilitekelezwa dhidi ya makundi ya Taliban na al-Qaida kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. Ni wazi kuwa vita hivyo havikuwa na natija nyingine isipokuwa kuwafaidi magaidi na kuwaletea machungu zaidi wananchi wa Afghanistan.

Hii leo, licha ya kuwepo kwa wingi askari-jeshi wa Shirika la Kujihami la Nchi za Magharibi Nato, katika ardhi ya Afghanistan na kwa uongozi wa Marekani, matatizo ya Waafghani yamekithiri na ulanguzi wa madawa ya kulevya umeongezeka maradufu. Si tu kwamba wafuasi wa makundi ya Taliban na al-Qaida wanajiimarisha zaidi, bali kwa mshangao na aibu kubwa, watawala wa kisiasa na kijeshi wa Marekani hivi sasa wanadai kwamba makundi hayo yanayochukuliwa kuwa ni ya kigaidi hayawezi kutokomezwa kwa njia za kijeshi bali, yanapaswa kushirikishwa katika mazungumzo ya amani na pia katika uendeshaji wa serikali kwa kupewa nyadhifa muhimu za wizara katika serikali hiyo!

Matamshi ya hivi karibuni ya Robert Gates, Waziri wa Ulinzi na vilevile, Condoleezza Rice, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani juu ya ulazima wa kushirikishwa serikalini makundi ya Taliban na al-Qaida na ushauri wao kwa serikali ya Hamid Karzai kuwa anapasa kuanzisha mazungumzo na makundi hayo ya kigaidi, ni ishara na tathmini kwamba njia za kijeshi dhidi ya makundi hayo hazina tena athari na kwamba njia bora ni kufanywa mazungumzo na magaidi. Kufeli kwa nadharia ya Marekani ya kutekeleza vita kwa ajili ya kuzuia mashambulio, nadharia ambayo ilitumiwa na serikali ya Bush kwa lengo la kuanzisha vita dhidi ya Iraq na kupitia propaganda chafu na kubwa za mtambo wa propaganda wa vyombo vya habari vya Marekani, hii leo ni jambo ambalo liko wazi kwa kila mtu kulishuhudia duniani.

Hadi leo Wamarekani wameshindwa kuthibitisha madai yao kwamba Iraq ilikuwa na mpango wa kutengeneza silaha za maangamizi ya umati za nyuklia na kemikali na vilevile kwamba ilikuwa na uhusiano wa moja kwa moja na mtandao wa al-Qaida, visingizio viwili vilivyotumiwa na serikali ya Bush kuanzisha hujuma kali ya kijeshi dhidi ya nchi hiyo. Kisingizio kingine kilichotolewa dhidi ya serikali ya Dikteta Saddam Hussein ni kuwa ilihusika kwa njia moja au nyingine katika mashambulio ya Septemba 11 katika miji ya New York na Washington.

Hii leo Wamarekani wameshindwa kabisa kurudisha amani na utulivu nchini Iraq na ili kuondokana na jinamizi linalowaandama kutokana na siasa zao bovu katika nchi hiyo, wanajaribu kuepuka mashinikizo yanayotolewa dhidi yao kimataifa na ndani ya Marekani yenyewe kuhusiana na jambo hilo kwa kujaribu kuwatupia wengine lawama za machafuko yanayoendelea nchini humo.

Wanajaribu kupunguza mashinikizo hayo kwa kudai kwamba nchi jirani ndizo zinazochochea machafuko katika ardhi ya Iraq au kuwashinikiza viongozi wa Iraq watie saini mkataba wa amani na serikali ya Washington ili jambo hilo liwape mwanya wa kupumua, wakidhani kwamba kuendelea kubaki kwao nchini Iraq kwa muda zaidi huenda kukawapa fursa ya kutatua matatizo ya usalama ya nchi hiyo na wakati huohuo kuwapa fursa ya kupora utajiri wa Iraq na kutekeleza malengo yao mengine haramu nchini humo.

Ni wazi kuwa hii leo siasa za upande mmoja za Marekani zimefeli kabisa na wala serikali ya Marekani haiwezi kudai kwamba Iraq ni nchi yenye uthabiti na iliyosimama kwenye misingi ya demokrasia ya kuagizwa kutoka nje. Hatua ya watawala wa nchi hiyo ya kuomba msaada wa mashirika na jumuiya za kimataifa ziingilie kati baada ya kushindwa siasa zake za upande mmoja, ni dalili ya wazi inayothibitisha kwamba jumuiya hizo sio ubao wa sataranji unaotumiwa daima na watawala wa Marekani kama muhuri wa kupitisha na kuunga mkono siasa zao za kibabe na kijuba duniani.

Mfano mwingine wa wazi wa watawala wa Marekani kutumia nguvu zao za kijeshi kama wenzo wa kufikia malengo yao haramu duniani ni mashinikizo yao dhidi ya Ethiopia kwa lengo la kupelekwa askari jeshi wake katika ardhi ya Somalia mwaka 2006. Jambo hilo kwa hakika halijakuwa na natija nyingine isipokuwa mauaji, wizi, uporaji na utumiaji mabavu dhidi ya raia wasio na hatia. Mkono mbovu wa watawala hao wapenda vita pia unaonekana wazi katika mauaji na machafuko yanayoendelea hivi sasa katika mpaka wa Pakistan na jirani yake Afghanistan, nchi ambayo imekuwa ikihesabiwa kuwa mshirika wa kwanza wa Washington katika vita vinavyodaiwa kuwa ni vya kupambana na ugaidi wa kimataifa.

Hii ni katika hali ambayo mzozo ambao unachukuliwa kuwa mkubwa zaidi katika Mashariki ya Kati, yaani suala la Palestina, ni nembo ya faili jeusi la serikali mbalimbali za Marekani na hasa utawala wa miaka minane wa Bush. Faili hilo limefumbiwa macho na kunyamaziwa kimya na Wamarekani kana kwamba halina umuhimu wowote kwao.

Miaka minane ya Bush imepita bila ya kutekelezwa ahadi za uongo za utawala huo za kusaidia kuunda serikali ya taifa huru la Palestina. Badala yake utawala huo umekuwa ukiunga mkono waziwazi jinai zinazotekelezwa na utawala haramu wa Israel dhidi ya Wapalestina wasio na hatia wala ulinzi. Kwa masikitiko makubwa, uungaji mkono na himaya ya serikali ya Washington kwa jinai za utawala huo zimeupelekea kumea pembe na kupata kiburi zaidi cha kuendelea kutekeleza jinai zake hizo dhidi ya watoto, wanawake, wazee na vijana wa Kipalestina huku ulimwengu mzima ukiwa umenyamaza kimya na kutochukua hatua yoyote ya maana kwa ajili ya kukabiliana na jinai za utawala huo.

Kufanywa mazungumzo yasiyo na natija, uungaji mkono mkubwa na usio na masharti wa serikali ya Washington kwa utawala haramu wa Israel pamoja na kupuuza haki za Wapalestina imekuwa moja ya nguzo muhimu za serikali ya Bush katika kipindi cha miaka minane iliyopita. Hii ni katika hali ambayo mzingiro wa kidhulma wa chakula, madawa na misaada ya dharura kwa Wapalestina umeimarishwa zaidi dhidi ya Wapalestina wanaoishi katika Ukanda wa Gaza. Mifano hii ni moja ya ukweli mchungu unaotawala hii leo ulimwenguni, mifano ambayo matokeo yake yanapasa kuwa funzo kwa watu wanaofuata kibubusa siasa za Marekani. Hatima ya Parviz Musharraf wa Pakistan ni mfano mzuri wa ukweli huo.

Siasa za Bush zilipata pigo jingine kubwa kwa kufichuliwa njama za serikali yake za kuzusha mgogoro wa kifedha na kiuchumi duniani. Mara hii mfumo wa kiuchumi wa Marekani umepata pigo kubwa na hata kumpelekea Bush mwenyewe kuomba msaada kutoka kwa jamii ya kimataifa ili kuiokoa nchi hiyo katika siku za mwisho za serikali yake. Kwa bahati mbaya, madhara ya mgogoro huo wa kiuchumi yamezipata pia nchi masikini ambazo zinalazimika kulipa gharama ya mgogoro huo wa Marekani.

Hata hivyo, inatarajiwa kuwa mgogoro huo wa kiuchumi na kifedha utakuwa na matokeo mazuri kwa Bush, wahafidhina mambo-leo na rais wa baadaye wa Marekani kwa kuwakumbusha kwamba wanapasa kuondoa vichwani mwao fikra kwamba wao ndio viongozi wa ulimwengu. Wakati huohuo wanapasa kutambua kwamba siasa za mabavu na kujichukulia maamuzi ya upande mmoja hazitawafikisha popote na kwamba wanawajibika kukubali na kutambua rasmi ukweli wa kuwepo nguvu za nchi nyingine duniani na hasa zile za nchi za Kiislamu.

Kwa vyovyote vile kipindi cha miaka minane ya utawala wa wahafidhina mambo-leo nchini Marekani kimemalizika na kuanza kipindi kilichojaa changamoto muhimu kwa watawala wa baadaye wa chama cha Democrat. Ulimwengu unasubiri kuona iwapo watawala hao watabadili siasa mbovu za uchokozi, ubabe na ujuba zilizotekelezwa na wenzao Warepublican au wataamua kuendelea na siasa hizo na hivyo kuvuruga zaidi amani na utulivu wa ulimwengu.

Mahakama yatetea uamuzi wa mjane kurudishwa kwenye nyumba alimofukuzwa

Ellen Manyangu na Salim Said

MAHAKAMA ya Ardhi Wilaya ya Kinondoni imetupilia mbali ombi la wakili wa mlalamikaji katika shauri la kutaka mahakama hiyo ifute agizo la mjane Shamsa Nassor wa Kiluvya kurudishwa katika nyumba alimohamishwa.

Mwenyekiti Joseph Kaare alitoa uamuzi huo jana alipokuwa akisoma hukumu ya maombi hayo yaliyowasilishwa na mlalamikaji Abdalah Malik kupitia wakili wake kutoka kampuni ya uwakili ya Rutabingwa.

Maombi hayo yaliwasilishwa mahakamani hapo yakiambatanishwa na nakala mbalimbali za hukumu zilizotolewa na mahakama za ngazi tofauti kuhusu kesi hiyo.

Nakala hizo, ambazo ni kutoka katika ngazi ya Mahakama ya mwanzo Magomeni, mahakama ya Wilaya Kinondoni na Mahakama Kuu ya Tanzania (High Court).

Kaare alithibitisha kuwa, nakala za hukumu za kesi ziliwasilishwa mahakamani hapo na wakili Rutabingwa hazihusiani na kesi ya ardhi aliyopeleka Shamsa Nassor.

Alisema, nyumba na eneo ambalo Rutabingwa aliwasilisha nyaraka zake ni la marehemu Zuwena Salum (mama mkwe wa Shamsa) ambayo msimamizi wake ni Mohammed Markbel na sio ya marehemu mume wa mjane huyo Salum Aklan.

“Amri yangu ya kumrudisha nyumbani mwake Shamsa, ambayo Rutabingwa alinitaka kuitengua haihusiani na mali zote za Zuwena wala maamuzi yoyote ya mahakama,” alisema Kaare katika hukumu ya kukataa ombi hilo na kusisitiza:

“Amri yangu ilikuwa ya kumrudisha mlalamikaji katika nyumba ya marehemu mume wake Salum Aklan, ambayo Shamsa na Alhaj Mohammed walichaguliwa kusimamia eneo na mali hiyo na mahakama ya mwanzo Kinondoni, ambapo namba ya kesi ilikuwa 55 ya mwaka 2008.”

Katika hukumu yake ambayo nakala imepatikana Kaare alisema, kwa maamuzi hayo nyumba iliyokuwa na mgogoro anayoishi mlalamikaji (Shamsa) ni ya marehemu mume wake Salum Aklan na maamuzi hayo hayajawahi kutofautishwa na maamuzi mingine yoyote.

Kwa upande wake Wakili wa Malik alikataa kuzungumza na mwandishi wa Mwananchi kwa madai kuwa hana muda.

“Sina muda wa kuzungumza na wewe kama unataka njoo ofisini,” alisema Rutabingwa ambaye pia Mwananchi ilimshuhudia akizungumza na waandishi wa baadhi ya vyombo vya habari nje ya mahakama hiyo ya Ardhi.

Baada ya hapo, Mwandishi wa habari hii alimpigia simu Malik ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Maji ya Cool Blue, Tembo Blox na Safari Kargo ili kuzungumzia kutupiliwa mbali kwa ombi lake.

“Sitaki kuzungumza katika simu, nifate ofisini, kwanza ulishindwa kunifata ofisini ukaandika uongo mtupu,” alisema Malik na kukata simu.

Hata hivyo baada ya dakika 10, Malik aliamua kumpigia simu mwandishi na kumueleza kwamba yeye hana kesi na Shamsa na kudai kuwa, mwenye kesi ni Shamsa na msimamizi wa mirathi ambaye hakumtaja jina lake.

“Usiniandike mimi sina kesi na Shamsa mwenye kesi na Shamsa ni msimamizi wa mirathi,” alijitetea Malik na kukata simu bila ya kumruhusu mwandishi kuzungumza.

Hata hivyo alipoulizwa Mohammed Markbel ambaye ni msimamizi wa mirathi ya marehemu Zuwena iwapo ana kesi na Shamsa au la, alikanusha kwa madai kuwa kesi zote zilishatolewa hukumu mahakamani.

“Mimi sina kesi na Shamsa ila tatizo lilikuwa baada ya kuteuliwa mimi kuwa msimamizi wa mirathi ya Zuwena Salum, Shamsa alikataa lakini alishindwa kwa sababu nilichaguliwa na watu watatu na yeye pekee ndiye alikataa,” alisema Markbel.

Marekani yaitoa hofu Tanzania

Salim Said

MAREKANI imesisitiza kuwa itatekeleza ahadi yake ya kuipatia Tanzania fedha kwa ajili ya miradi ya changamoto za Milenia (MCC) licha ya uchumi wake kutikisika.

Hayo yalielezwa juzi na rais Jakaya Kikwete alipokuwa akifungua harambee ya kuchangisha fedha za Mfuko wa Elimu mkoa wa Rukwa, iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Jambo la faraja kwetu ni kuwa miradi ya MCC haijaathirika na matatizo ya mtikisiko wa uchumi wa dunia nchini Marekani, wala mabadiliko ya serikali ya nchi hiyo,” alisema Rais Kikwete na kusisitiza:

“Marekani imenihakikishia kuwa fedha ya miradi hiyo bado ipo, imetengwa na iko salama. Vilevile serikali ya rais Barrack Obama, inaunga mkono mpango wa MCC na miradi yake hapa nchini, na ile yote iliyoamuliwa na rais mstaafu George Bush.”

Aidha alifafanua, fedha za barabara za ndani ya mkoa wa Rukwa zipo kupitia misaada ya Benki ya Dunia, kwa ajili ya ukarabati wa barabara ya kilomita 230 kutoka Sumbawanga hadi Mpanda.

Alizitaja barabara nyingine kuwa ni pamoja na ile ya Chala-Katongoro kilomita 87, Kilyamatunda-Muze kilomita 148 na upanuzi wa bandari ya Kusanga katika ziwa Tanganyika unaofanywa na mamlaka ya bandari.

“Nataka kuwahakikishia kuwa ni dhamira ya serikali kuchukua hatua za dhati kukabiliana ya barabara yanayoukabili mkoa wa Rukwa,” alisema rais Kikwete.

Kuhusu maendeleo ya elimu Rais Kikwete, alisema hivi sasa kata zote 2,556 nchini zina sekondari yake na kwamba nyingine zina sekondari zaidi ya moja.

“Matkeo yake ni kuongezeka kwa vijana wa kike na kiume wanaoingia sekondari kutoka 180,239 mwaka 2005 hadi 432,000 mwaka 2008,” alisema rais.

Hata hivyo alisema, maendeleo makubwa nay a haraka katika sekta ya elimu nchini yana changamoto za kupata walimu bora, maabara, vitabu na nyumba za walimu.

“Tumejipanga vyema kukabiliana na changamoto zote hizo. Nyongeza kubwa ya bajeti ya elimu ni ushahidi tosha wa kutambua wajibu wetu,” alithibitisha.

Serikali kupunguza gharama za mawasiliano

Salim Said

SERIKALI inafikiria kuangalia upya mfumo wake wa gharama za kodi kwa vyombo vya mawasiliano, ili kuwianisha gharama za mawasiliano kwa nchi zote tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha, uamuzi huo unakuja kutokana na gharama za mawasiliano nchini kuwa juu kuliko nchi nyingine.

Hatua hiyo ni katika juhudi za serikali ya Tanzania kutaka kupunguza gharama za mawasiliano nchini ili kuwianisha gharama zake za mawasiliano na zile za nchi tano za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Hayo yalisemwa jana na Waziri wa Mawasiliano Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter Msolla, mara baada ya kufungua siku ya pili ya mkutano wa kuwianisha kanuni na sera za mawasiliano ya posta na simu, kwa nchi za Afrika Mashariki, uliomalizika jana, jijini Dar es Salaam.

Profesa Msolla alisema, gharama za mawasiliano nchini ziko juu zaidi kuliko nchi zote za Afrika Mashariki na Kati na kwamba tatizo ni mfumo wa kodi wa Tanzania kwa vyombo vya mawasiliano.

“Gharama za mawasiliano tanzania ziko juu kuliko nchi nyingine kwa sababu ya mfumo wa gharama za kodi kwa vyombo vya mawasiliano,” alisema Msolla.

Hata hivyo alisema, serikali ina mpango wa kuangalia upya mfumo huo wa kodi kwa ajili ya kuwianisha viwango vya gharama za mawasiliano miongoni mwa nchi zote tano za Jumuiya ya Afrika ya ashariki.

“Serikali inaandaa utaratibu wa kuangalia upya mfumo wake wa kodi hasa kwa vyombo vya mawasiliano ili viwango vya gharama za bidhaa hii viweze kufanana miongoni mwa nchi washiriki wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki,” alithibitisha Msolla.

Alisisitiza kuwa mawasiliano ni moja ya bidhaa katika soko la pamoja la Afrika ya Mashariki kwa hiyo lazima gharama zilingane kwa watumiaji wote wa mijini na vijijini.

Aidha alifafanua kuwa mkutano wa 16 wa wadhibiti na watoa huduma ya mawasiliano wa ukanda wa Afrika ya Mashariki pia ulijadili ujenzi wa mundombinu ya uhakika ya mawasiliano ili bidhaa hiyo iweze kuwafikia watu wote wa mijini na vijijini.

Aidha priofesa Msolla alisema, katika kufanikisha shirikisho la Afrika ya Mashariki lazima maudhui ya vyombo vya mawasiliano na lugha zifanane ili kulinda utamaduni wa watu wake.

“Sisi tuna lugha zetu na mila na utamaduni wetu, kwa hiyo maudhui ya vyombo vyetu vya mawasiliano lazima yange katika kulinda na kuendeleza utamaduni wetu,” alisema Msolla na kusisitiza:

“Tusiwe tunaiga na kufuata mila na tamaduni za watu, tunacho Kiswahili chetu basi tukitumie kwa manufaa ya watu wetu.”

Kwa upande wake Mshauri wa Sheria wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano ya Rwanda, Lamin Jabir alisema, serikali ya nchi yake inajitahidi kutoa ruzuku kwa watoa huduma za mawasiliano ili kuwapa nafuu watumiaji.

“Serikali yetu inajitahidi kutoa ruzuku kwa watoa huduma ya mawasiliano ili mtumiaji aweze kumudu kwa urahisi,” alisema Jabir na kusisitiza:

“Lakini pia sera, sheria na kanuni zetu ni nzuri kabisa kwa watumiaji na watoa huduma.”

Mamlaka zakutana kujadili sera,kanuni

Salim Said

MAMLAKA za Mawasiliano za nchi tano za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, zimekutana na watoa huduma za mawasiliano jijini Dar es Salaam kuoanisha sera, sheria na kanuni za mawasiliano katika nchi hizo.

Mamlaka hizo zilikutana jana katika semina iliyojali umuhimu wa kuharakisha uundaji wa Shirikisho la Afrika Mashariki.
Tayari baadhi ya asasi za shirikisho hilo zimekwishaundwa.

Akizungumza katika ufunguzi wa semina hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wa Tanzania, Dk. Naomi Katunzi, alisema katika mjadala wa kuunda soko la pamoja baina ya nchi hizo, suala la mawasiliano lilijitokeza.

“Kwa hiyo leo tupo hapa kwa ajili ya ‘kuoanisha sera, sheria na kanuni za mawasiliano miongoni mwa nchi washiriki,” alisema Dk. Katunzi na kuongeza:

“Mawasiliano na biashara ni vitu vinavyotegemeana kwa karibu, huwezi kufanya biashara na kufanikiwa bila ya kuwa na mawasiliano mazuri yanayohusisha wafanyabiashara, walaji na wadhibiti,” alisema.

Hata hivyo shirikisho hilo, linaonekana kuwa na kikwazo ambapo nchi za Kenya na Uganda zinagombania kisiwa cha utalii cha Migingo.

Katibu mkuu huyo alisema, Tanzania itakuwa kitovu cha mawasiliano kupitia Mkonga wake wa taifa wa mawasiliano na kwamba nchi hizo jirani zitaomba kuunganishwa katika mkonga huo kupitia Tanzania.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Profesa John Nkoma, alisema mkutano huo pia unawakutanisha wadhibiti na watoa huduma za mawasiliano kutoka nchi hizo.

Alisema, moja ya lengo la semina hiyo ni kujadiliana nao kuhusu namna ya kupunguza gharama za mawasiliano kwa watumiaji.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya Kanuni, Posta na Mwasiliano) Charles Njoroge wa Kenya, alisema jumuiya yake imekuwa vikikutana mara kwa mara, kujaribu kuweka utaratibu na mfumo wa mawasiliano unaofanana baina ya nchi husika.

“Tutajitahidi kuwasiliana na watoa huduma ili kuhakikisha kuwa gharama za mawasiliano katika Jumuiya ya Afrika ya Mashariki zinakuwa rahisi zaidi,” alisema Njoroge ambaye pia Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano ya Kenya.