MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Monday, June 29, 2009

Makamu mwenyekiti ZEC ajiuzulu

Salim Said
MAKAMU Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji Omar Othman Makungu amejiuzulu wadhifa wake katika Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).

Jaji Makungu alikuwa Kamishna wa ZEC tangu Januari mwaka 2008 baada ya kuteuliwa kushika nafasi hiyo na Rais Amani Abeid Karume.

Taarifa ambazo Mwananchi na kuthibitishwa na mwenyewe Jaji Makungu zinasema, amechukua uamuzi huo akihofia kuzidiwa na kazi katika uchaguzi mkuu wa 2010 kwa kuhudumu katika tume mbili tofauti.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kutoka visiwani Zanzibar jana, Jaji Makungu alithibitisha kujiuzulu kwake wadhifa huo hivi karibuni kwa kuhofiwa kuzidiwa na kazi katika kipindi uchaguzi.

“Ni kweli nimejiuzulu,” alithibitisha na kuongeza kuwa:

“Nimejiuzulu kwa sababu tunaelekea katika uchaguzi mkuu kwa hivyo sitaweza kutumika kwenye tume ya taifa ya uchaguzi na tume ya uchaguzi ya Zanzibar kwa wakati mmoja.”

Alisema, kwa vile anafanya kazi katika tume zote mbili za uchaguzi anaweza kuzidiwa na majukumu na hivyo ni bora tu kubakia katika upande mmoja wa NEC.

Januari mwaka 2008 Rais wa Zanzibar Amani Abeidi Karume alimchagua Jaji Makungu kuwa miongoni mwa makamishna wa ZEC baada ya kuunda upya tume ya uchaguzi ya Zanzibar.

Rais Karume alimtangaza Khatib Mwinyichande kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo pamoja na makamishna sita, wakiwemo wawili kutoka chama cha Wananchi (CUF).

Makamishna walioteuliwa kuhudumia ZEC kwa miaka mitano ni aliyekuwa Meneja Mkuu wa Shirika la Biashara Zanzibar (ZSTC), Abdulrahman Rashid na aliyewahi kuwa Waziri wa Afya na Utibabu Zanzibar, Said Bakar Jecha.

Wengine ni Mwanabaraka Maalim Ahmed, Jaji wa Mahakama Kuu na Makamu Mwenyekiti NEC Omar Othman Makungu.

Wajumbe walioteuliwa kutoka CUF, ni wakili maarufu wa Zanzibar, Nassor Khamis na Ayoub Bakar Hamad aliyekuwa Katibu wa Uchaguzi wa CUF.