MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Tuesday, July 21, 2009

Lwakatare amejimaliza kisiasa; Dk. Bana

Salim Said
KWA miaka mingi watanzania wamekuwa wakishuhudia wanachama na viongozi kutoka vyama vya upinzani wakihamia chama tawala cha Mapinduzi (CCM), lakini upepo wa kisiasa umeanza kubadilika kwa viongozi upinzani kutoka chama kimoja cha upinzani kwenda kingine cha upinzani.

Kwa mara ya kwanza watanzania wameshudia kiongozi mmoja wa ngazi za juu kutoka chama cha upinzani akikihama chama chake na kuhamia chama kingine cha upinzani.

Si mwengine huyu bali ni aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Tanzania Bara Wilfred Lwakatare, ambaye amajiunga rasmi na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), sababu kubwa ikiwa ni kukosa nafasi yake baada ya mabadiliko ya uongozi yaliyofanyika ndani ya chama hicho Machi mwaka huu.

Kwa mujibu wa Lwakatare, ameamua kuhama CUF kutokana na tabia ya majungu, roho mbaya, unafiki, fitna na mtima nyongo walizonazo baadhi ya wanachama na viongozi wa chama hicho na kumsababishia kuukosa nafasi yake.

“Jina langu liliachwa katika kutetea nafasi yangu ya unaibu Katibu Mkuu wa chama kwa sababu ya viongozi wa CUF kusikiliza na kuamini majungu na fitna kutoka kwa baadhi ya viongozi, kwamba mimi ni mbadhirifu wa fedha za chama,” anasema Lwakatare.

Lakini kuhama kwa Lwakatare ndani ya chama chake cha CUF kunachukuliwaje na wananchi, wasomi na wanasiasa?

Baadhi ya wadau wa masuala ya kisiasa wanaona kwamba nguvu ya upinzani imeanza kupoteza mwelekeo wa kisiasa.

Kwa mtazamo wa chama cha NCCR-Mageuzi wanaona kuwa, Lwakatare kwenda Chadema, ni hujuma na ufisadi wa kisiasa ambapo chama hicho kinatumia ubaguzi kuiba viongozi wa vyama vingine vya upinzani kwa lengo la kuudhoofisha.

Dk. Benson Bana, ni Mkuu wa Kitengo cha Sayansi ya Siasa cha Chuo kikuu cha Dar es Salaam, anasema kwa alivyomsikiliza Mwenyekiti wa CUF taifa Profesa Ibrahim Lipumba, sababu za kumuacha Lwakatare hajazitaja na kwamba kuna sababu nyingine za kumuacha kigogo huyo Naibu Katibu Mkuu huyo wa zamani.

“Kumuacha mtu kwa sababu eti akiwa Naibu Katibu Mkuu anakosa muda wa kuimarisha chama si kweli. Ni tofauti akiingia kiongozi jimboni kwake kama Naibu Katibu Mkuu na akiingia kama mwanachama wa kawaida. Mbona tuna Mawaziri wa CCM, lakini wanafanya kazi ya kuimarisha chama vizuri tu,” anasema Dk. Bana.

Dk. Bana anakiri kuwa, Chadema ni chama namba moja cha upinzani kwa upande wa Tanzania bara, lakini pia anikiri kuwa haina nguvu kubwa kuliko CUF katika Wilaya ya Bukoba.

“Chadema ni chama chenye nguvu sana Tanzania bara kwa sababu kina wanachama wengi na hata wabunge wake ni imara sana,” anasema Dk. Bana.

Anafafanua kwamba, Lwakatare amebeba hatari ya kisiasa (Political risk) mgongoni mwake kwa kuwa ni vigumu sana kile ambacho kilimfanya ahame CUF kukipata ndani ya Chadema.

“Kwanza Lwakatare si mwanasiasa makini, huwezi kumlinganisha na maalim Seif Sharif au Juma Duni hawa wana akili sana na pia ni hazina katika siasa za Tanzania. Ni kweli CUF imeathirika lakini hata hivyo pengo aliloliacha si kubwa sana kama anavyodhani mwenyewe,” anasema Dk. Bana.

Anasema, Chadema haiwezi kumuondoa Zitto Kabwe na kumuweka Lwakatare na kwa kugombea ubunge kupitia Chadema hawezi kushinda kwa sababu tayari kura zake ameshazigawa, waumini wake lazima watagawika kwani wapo watakaomfuata na wapo watakaobakia CUF.

“Si dhani kama anaweza kupata nafasi ya juu kama aliyokuwanayo CUF ingawa pia sijui aliahidiwa nini mpaka akashawishika kuhama chama chake na kuingia Chadema,” anasema Dk. Bana.

Dk. Bana anasema, Lwakatare anakabiliwa na upinzani mkubwa wa mbunge wa Bukoba Mjini Hamisi Kagasheki, ambaye tayari amejiimarisha vya kutosha jimboni humo.

“Kagasheki ana nguvu sana Bukoba, amejimarisha vya kutosha, amesaidia kuboresha hospitali, ameimarisha shule za sekondari na ameafanikiwa kuanzisha kituo chake cha redio, jambo ambalo limemrahisishia kuwafikia watu wengi na kwa muda mfupi, ili kuwauzia sera zake,” anaeleza hali ngumu inayomkabili Lwakatare.

Anasema, kwa miaka mitano aliyokaa madarakani mbunge Kagasheki, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi amefanikiwa kuwafanya wananchi wa Bukoba Mjini kutokuwa na usongo naye na anaingia katika uchaguzi 2010 akiwa anajiamini.

Dk. Bana ambaye pia ni mwenyeji wa Bukoba anasema, Lwakatare ana mambo mingi ya kujifunza kwa sababu wananchi wake hawamchagui mtu kama yeye, bali wanaangalia sera, ilani, msimamo na itikadi ya chama cha mgombea wao.

“Watu wa Bukoba wanaelewa vizuri siasa, naweza kuwafananisha na wazanzibari hasa wa kisiwa cha Pemba, wao si bendera kwamba wanafuata upepo tu. Si dhani kama Lwakatare alifanya utafiti na kujitathmini kabla ya kuchukua uamuzi wa kuhama CUF. Na hata kama angesimama kama mgombea binafsi yeye si Nabii jimboni kwake kwamba anapendwa sana,” ansema.

Dk. Bana ambaye ni mchambuzi wa masuala ya siasa kitaaluma, anaweka hadharani sababu za msingi zilizomfanya Lwakatare kujitoa katika chama cha CUF.

“Unajua Naibu Katibu Mkuu ni nafasi ya mshahara, marupurupu, usafiri na baadhi ya wakati hata nyumba unapewa, lakini wanasiasa wengi wanategemea kazi yao ya siasa kama chanzo cha kujipatia fedha. Hivyo baada ya kuikosa ndio kashindwa kuvumilia,” anasema Dk Bana.

Anasema, jambo baya zaidi kwa Lwakatare ni kuchukua maamuzi haraka tena ndani ya muda mfupi tu tangu kukosa unaibu Katibu Mkuu, jambo ambalo hata mtoto anaanza kuhoji uvumilivu wake na kujua kwamba ametoka katika chama kwa kukosa cheo, mengine yakiwa ni visingizio tu.

“Kimsingi Lwakatare hajatoka ndani ya chama kwa kujenga chama, bali ametoka ndani ya chama kwa maslahi yake binafsi, baada ya kukosa mshahara na marupurupu,” anasema Dk Bana.

Anasema, kwa kawaida mwanasiasa yeyote huingia au kukihama chama kwa mambo manne tu, ambayo ni sera, msimamo wa chama, ilani na Itikadi, “sasa sina uhakika kwamba sera, itikadi, ilani na msimamo wa CUF umebadilika au Chadema wameiba vitu hivyo kutoka CUF na yeye akaona kwamba amepata chama mbadala chenye sera zinazolingana na cha kwake?”

Dk. Bana ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamizi wa chuo kikuu cha Dar es Salaam katika Fani za Sayansi za Siasa, anaelezea madhara ya uamuzi wa mbunge huyo wa zamani wa jimbo la Bukoba Mjini na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni kupitia CUF.

“Hii ni sifa mbaya sana katika jamii kiongozi kuhama chama kwa kukosa madaraka, utahama na kuhamia vyama mara ngapi? Kwa sababu usidhanie kuwa utakuwa kiongozi mkubwa milele katika chama. Jamii inaweza kumtafsiri kuwa ni mlafi wa madaraka na fedha kwa kufanya maamuzi hayo baada ya kukosa madaraka na mshahara,” anasema.

Anaongeza kuwa, wanasiasa makini watamdharau na kumtoa thamani sana kutokana na maamuzi yake, kwa kuwa siasa si ajira bali ni kazi ya kuutumikia umma ili ujijengee jina.

“Ni jambo baya sana kwa kiongozi kuyumbishwa kidogo akaonesha udhaifu wa kuyumbika. Si vizuri hata kidogo, unatakiwa kuwa na msimamo na kusimamia kile unachokiamini siku zote. Lakini anaanza kukosa uvumilivu hata jamii inajua, kwa kweli amejimaliza na kujiharibia kisiasa,” anasema.

Dk. Bana anasema, Lwakatare amejimaliza kwa sababu amesafisha njia na kumtengenezea mpinzani wake CCM ajenda ya kuiuza kwa wananchi wa jimbo hilo katika kampeni za uchaguzi mkuu wa 2010.

CCM watawambia wapigakura, ‘Sisi tunahitaji viongozi makini, wenye msimamo na wavumilivu katika siasa na matatizo, sasa mwangalieni Lwakatare ana uvumilivu, msimamo na umakini gani? Anahangaika tu katika vyama kwa kukosa madaraka’ “hii ni ajenda tayari imeshanunuliwa na Kagasheki mbunge wa Bukoba Mjini CCM,” anasema.

Anasema, Lwakatare amezidi kudhoofisha nguvu ya upinzani kwa sababu, “awali tulikuwa tunaona wapinzani wanahama na kuhamia Chama cha Mapinduzi (CCM), lakini upepo umebadilika na sasa wanaanza kuzunguka humohumo, hii ni ishara mbaya kwa kambi ya upinzani,” anasema Dk. Bana.

Anasema, Upizani wa Tanzania haujui kufaya kazi ya siasa kwa kuwa wameingia katika mtego wa CCM, imefanikiwa kujenga mtandao kuanzia ngazi ya Jamii Msingi (grass root) hadi taifa, na sio kutembea na Helicopter tu wakati wa kampeni za uchaguzi.

“Kutembea na helicopter katika uchaguzi si kuimarisha chama. Nawashauri wapinzani wawe na mpango mkakati wa kuimarisha vyama vyao kama kweli wana nia na utashi wa kisiasa wa kupambana na CCM. Walete mambo ambayo hayajaletwa na CCM,” anasema.

Kwa upande wake, Profesa Lipumba anasema, taarifa za kuhama kwa Lwakatare zimewasikitisha sana kwa sababu hawakutegemea kutokana na ukweli kwamba mtu kukosa cheo ndani ya chama haijawa sababu ya kumfanya ahame.