MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Monday, July 27, 2009

Profesa Ngugi kunguruma UDS

Salim Said
PROFESA Ngugi wa Thiong’o kutoka Kenya anatarajiwa kuhutubia Kongamano la sita la Usomaji kwa Wote katika nchi za Afrika litakalofanyika katika chuo kikuu cha Dar es Salaam kuanzia Agosti 10 hadi 14 mwaka huu.
Kongamano hilo, linafanyika chini ya ushirikiano wa Chama cha Usomaji wa Kimataifa, Kamati ya Kimataifa ya Afrika, Chama cha Usomaji Tanzania na Mradi wa Vitabu vya Watoto Tanzania (CBP).

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya kongamano hilo Profesa Mugyabuso Mulokozi alisema, kongamano hilo litawashirikisha wadau na kuwakutanisha wadau mbalimbali wa elimu kutoka ndani na nje ya nchi.

“Katika kongamano hili Profesa Ngugi atakuwa mgeni rasmi na washiriki kutoka nchi mbalimbali watakutana kubadilishana maarifa, uzoefu, taarifa, na kupanga mikakati mbalimbali ya kuboresha masuala ya usomaji na ikiwa ni pamoja na kuzitafutia ufumbuzi changamoto za usomaji,” alisema Profesa Mulokozi.

Alisema, kauli mbiu ya mwaka huu ni ‘Usomaji wa Vitabu kwa ajili ya Kuleta Maegeuzi na Maendeleo ya Kijamii na Kiuchumi.

“Kongamano hili litawakutanisha wakereketwa wa usomaji wakiwamo walimu, wakufunzi, watafiti, wahadhiri, wakutubi, waandishi, wachapaji, wauza vitabu, viongozi, watunga sera na wasomaji mbalimbali kutoka Afrika na kwenmgineko,” alisema Profesa Mulokozi,.

Alisema, zaidi ya washiriki 200 watawasilisha maandiko yao katika kongamano hilo, na kwamba washiriki 200 kutoka nje ya nchi watashiriki na 300 kutoka Tanzania.

Alisema katika kongamano hilo kutakuwa na zawadi kwa washindi wa tatu wa shindano la uandishi wa fasihi katika bara la Afrika pamoja na uzinduzi wa kitabu cha prfesa Ngugi kijulikancho kwa jina la ‘Re-Membering Afrika’.

Kongamano hili ni la sita ambapo yaliyopita yalifanyika katika nchi za Afrika ya Kusini 1999, Nigeria 2001, Uganda 2003, Swaziland 2005 na Ghanna mwaka 2007.

Wadau wapinga mfuko wa jimbo

Salim Said
WADAU wa masuala ya kisiasa na uchumi nchini wameipinga vikali nia ya serikali kuanzisha Mfuko wa Kuhudumia Jimbo kwa sababu mfuko huo utakuwa na harufu mbaya ya ufisadi.

Wakati wadau wakiupinga uanzishwaji wa mfuko huo, serikali inakusudia kukusanya maoni ya wananchi kuhusu uanzishwaji wa mfuko huo wiki ijayo.

Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam jana wadau hao walisema, mfuko huo una harufu ya ufisadi ndani yake.

Profesa Ibrahim Lipumba alisema, hauungi mkono mfuko huo kwa sababu una harufu ya ufisadi na upendeleo kwa wabunge wenye majimbo.

“Mimi siuungi mkono kwanza una harufu ya mbaya ya ufisadi lakini pia wabunge wenye majimbo watakuwa na upendeleo katika matumizi ya fedha hizo,” alisema profesa Lipumba.

Alisema, hakuna haja ya kuanzishwa kwa mfuko huo kwa sababu kuna halmashauri za Wilaya ambazo zinatosha kutumika kusimamia fedha za maendeleo ya wananchi.

“Serikali inaweza kupitishia fedha hizo katika halmashauri na kugaiwa katika kikao cha Baraza la Madiwani ambacho mbunge ni mjumbe wa kikao hicho ataweza kushiriki katika njia hiyo na si kumkabidhi fedha,” alisema Profesa Lipumba.

Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dk. Benson Bana alisema, hakubaliani kabisa na nia ya serikali kuanzisha mfuko huo kwa sababu tayari kuna mifuko mingi ya maendeleo katika ngazi za Halmashauri.

“Mfuko huu unatoka wapi na kwa nini uwe wa jimbo, kwa sababu ngazi za maendeleo katika halmashauri si jimbo tu na kwa nini usiwe wa ngazi nyingine. Kwa kweli mfuko huu unazua maswali mingi kuliko majibu,”alisema Dk Bana.

Dk Banna alihoji, sababu ya serikali kutaka kuanzisha mfuko huo hivi sasa na kwa nini haukuanzishwa katika miaka 10 iliyopita.

“Mfuko huu kwa mazingira ya Tanzania na ukata tuliwonao lazima utazua na kuongeza mitafaruku na migongano majimboni kutokana na upendeleo wa wabunge,” alisema Dk. Bana.

Alisema, hakuna haja ya kumuongezea Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kazi ya kufanya ukaguzi katika mifuko isiyo na idadi.

“Halmashauri zinatosha kabisa kusimamia fedha, kama serikali ina fedha inataka kuzipeleka kwa wananchi izipitishie katika halmashauri tu na hakuna haja ya kuongeza idadi ya mifuko,” alisema Dk. Banna na kuhoji:

“Tuna mfumo uliokamilika katika ngazi ya halmashauri wa kusimamia fedha za serikali kwa ajili ya maendeleo ya wananchi, kwa nini tusiutumie au tunataka kuwapa mdomo wabunge waliopo madarakani.”

Shabiby: Aataka EWURA, TRA kudhibiti bei za mafuta

Salim Said
MBUNGE wa Gairo (CCM) Ahmed Mabkhut Shabiby amezitaka Mamlaka za Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na ya Mapato Tanzania (TRA) kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuhakikisha wanadhibiti upandaji wa ovyo wa bei za mafuta katika majiji nchini.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu jana, Shabiby alihoji kwa nini bei ya mafuta katika jiji la Dar es Salaam iko juu na mikoani iko chini.

Alisema, upandaji wa mara kwa mara wa bei za mafuta kwenye majiji makubwa nchini hususan Dar es Salaam unatia shaka na kutishia amani kwa watumiaji.

Akizungumza huku akitolea mifano baadhi ya makampuni ya mafuta nchini, alisema Dar es Salaam ndiyo sehemu ambayo mafuta hushuka kutoka nje ya nchi, lakini bei yake iko juu kuliko mikoani ambako husafirishwa baada ya kushushwa jijini hapa.

“Hivi hizi bei elekezi za EWRA zinafanya kazi kweli, kwa sababu Dar es Salaam ambako mafuta hayo hushushwa yanauzwa kati ya 1500 na kuendelea, lakini Dodoma mfano yanauzwa sh 1450, napata wasiwasi na ushirikiano wa TRA na EWRA katika kazi zao,” alisema Shabiby.

Alisema, kama kuna ushirikiano kati ya mamlaka hizo, wangekaa na kuangalia kwa makini faida na gharama ya kila lita moja ya mafuta na kuweza kupanga bei ambayo itakuwa inakidhi mahitaji ya watumiaji na isiyobadilika ovyo ovyo.

“Kinachofanyika katika kupanga bei hapa ni kwamba hawaangalii gharama bali huangalia wingi wa magari (mahitaji) katika mji. Kama magari ni mingi bei itakuwa juu na kama ni kidogo bei itakuwa chini, hivi si sahihi hata kidogo,” alisema Shabiby.

Alitolea mifano katika nchi jirani ya Kenya ambapo sehemu zenye bandari ambapo mizigo hushukia bei ya mafuta huwa chini kwa sababu mamlaka za mapato na za udhibiti wa huduma za mafuta zinafanya kazi kwa na ushirikiano mkubwa.