MARASHI

PLAN YOUR WORK AND WORK ON YOUR PLAN BUT, WHEN YOU FAIL TO PLAN, YOU PLAN TO FAIL

Sunday, August 19, 2012

SWALA YA IDD KITAIFA RUVUMA




Muft wa Tanzania Issa bin Shaaban Simba akiwa katika pozi mbalimbali aliokuwa akihudhuria swala ya IDD iliyoswaliwa kitaifa Mkoani Ruvuma.

SWALA YA IDD MASJID BAKWATA MAKAO MAKUU




Rais Jakaya Kikwete akiwa katika pozi mbalimbali alipokwenda kuswali swala ya Idd katika viwanja vya Bakwata Makao Makuu jijini Dar es Salaam.

SWALA YA IDD MNAZI MMOJA DAR ES SALAAM





Makamu wa Rais Dk Moh'd Gharib Bilal na Mzee Ali Hassan Mwinyi wakiwa katika pozi mbalimbali wakati na baada ya kuswali Idd katika Viwanja vya Mnazi Mmmoja jijini Dar es Salaam.

Friday, August 17, 2012

BREWERIES YAFUTARISHA: NI UPI UHALALI WA FUTARI HIYO, NINI HUKUMU YA MUISLAM ALIYEKUBALI KUFUTARISHWA NA KAMPUNI YA POMBE?




Baadhi ya waislaam na wafanyakazi wa Kampuni ya Bia Tanzania (Breweries) wakiwa katika pozi mbalimba waliposhiriki futari iliyoandaliwa na kampuni hiyo jana.

Thursday, August 16, 2012

MAREKANI YAENDELEZA MAUAJI SOMALIA

MOGADISHU
Ndege za kigaidi zisizo na rubani za Marekani zimeendelea kufanya mauaji ya watu katika nchi ya Waislamu ya Somalia iliyopo Afrika.
Watu wasiopungua saba wameauwa na wengine kumi na saba wamejeruhiwa katika mashambulizi ya jana Jumatano yaliyofanywa na ndege hizo kwenye mji wa JOWHAR nje kidogo ya mji mkuu wa nchi hiyo Mogadishu.
Hadi sasa hakuna taarifa yoyote iliyotolewa kuhusu hasara nyingine zilizosababishwa na mashambulizi hayo ya kinyama.
Mbali na nchini Somalia, Marekani imekuwa ikitumia ndege zisizotumia rubani kufanya mashambulizi ya kigaidi katika nchi za Afghanistan, Pakistan, Yemen na imewahi kutumia pia ndege hizo nchini Libya.
Marekani inadai kuwa inashambulia wanamgambo wa AL-QAEDA na AS-SHABBAB, lakini wananchi wa kawaida ndio wahanga wakuu wa mashambulizi ya ndege hizo za kigaidi.

MAELFU WAKIMBIA MAKAZI YAO

KINSHASA
MAPIGANO ya miezi mitano sasa kati ya waasi wa kundi la M23 na Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya KONGO yamewalazimisha zaidi ya watu nusu milioni kukimbia makazi yao huko mashariki mwa nchi hiyo.
Ripoti zinasema kuwa raia wengi wa maeneo ya Kivu Kaskazini yenye utajiri mkubwa wa madini wamelazimika kukimbia makazi yao baada ya kujikuta katikati ya machafuko na mapigano ya kundi la M23 na Jeshi la serikali ya Kinshasa.
Maafa hayo yanaendelea kuwapata raia wa kawaida wa KONGO licha ya kuwepo maelfu ya askari wa Umoja wa Mataifa waliopelekwa nchini humo kwa ajili ya kulinda amani.
Mamia ya wakimbizi hao wa KONGO wamevuka mpaka na kuingia nchi jirani za RWANDA, BURUNDI na UGANDA huku Serikali ya KONGO ikitoa shutuma kali kwa nchi ya RWANDA na UGANDA kwa kuwaunga mkono waasi wa kundi la M23.
Waasi wa M23 walijitenga na jeshi la serikali ya Kinshasa wakidai kuwa serikali haijatekeleza vipengele vya makubaliano ya amani yaliyotiwa saini MACHI 23, 2009.

HRW YAINGILIA KATI WAISLAAM KUKAMATWA ETHIPEA

ADDISABABA
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch (HRW) limeitaka serikali ya Ethiopia kuwaachia huru viongozi 17 wa Kiislamu waliokamatwa katika maandamano ya amani yaliyofanyika nchini humo.
Taarifa iliyotolewa na hilo la Kutetea Haki za Binadamu imesema serikali ya Ethiopia inapaswa kuwaachia huru viongozi hao 17 wa Kiislamu waliotiwa nguvuni wakati askari wa usalama wa Ethiopea walipowakandamiza kinyama wapinzani Waislamu mjini Addis Ababa.
Watu hao walitiwa nguvuni katika maandamano makubwa ya amani yaliyofanywa na Waislamu mwezi jana kupinga uingiliaji usio wa kisheria wa serikali katika masuala ya Waislamu.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesisitiza kuwa mahabusu hao wanakabiliana na hali mbaya na wanashikiliwa bila ya kujulishwa makosa yao au kuwa na wakili.
Waislamu wanaunda zaidi ya asilimia 30 ya jamii ya watu milioni 83 ya Ethiopia.

TRA WAPATA SCANNER MPYA TANGA

TANGA
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Tawi la Tanga imepata mashine mpya ya kisasa yenye uwezo wa kutambua bidhaa zilizohifadhiwa ndani ya makontena (Scarner) na kuiwezesha mamlaka hiyo kufanya kazi zake kwa ufanisi na haraka.
Meneja wa Mamlaka hiyo Mkoani Tanga Nyonge Mahanyu, amesema mashine hiyo itakuwa mkombozi kwa wafanyabiashara wa mkoa huo kwa kuwa itaondosha kero za wafanyabiashara kucheleweshewa shehena zao katika Bandari ya Tanga.
Mahanyu amesema awali wafanyabiashara wa Tanga walikuwa wakilalamikia kucheleweshwa kwa ukaguzi wa mizigo yao bandarini hapo jambo lililokuwa likitishia uhai wa bandari kongwe ya mkoa wa Tanga.
Amesema baada ya ujio wa mashine hiyo utaweka mvuto kwa wafanyabiashara wengi kwa kuwa wataweza kushusha shehena zao kwa wakati na bila ya usumbufu.
Mahanyu amefafanua kuwa mashine hiyo ina uwezo wa kukagua kontena moja kwa dakika tatu tu jambo ambalo litaiwezesha TRA kukagua makontena mengi ndani ya muda mfupi na hivyo kukusanya kodi nyingi tofauti na ilivyo sasa.
Kwa upande wake mtaalamu wa Scana Mhandisi Julias Joseph, amesema mashine hiyo ambayo ina uwezo mkubwa wa kukagua na kutambua shehena zilizomo ndani ya makontena itakuwa kimbilio la wafanyabiashara kushusha bidhaa zao katika bandari ya Tanga.
Kutokuwapo kwa ufanisi katika utoaji wa huduma katika Bandari ya mkoa wa Tanga kumesababisha wafanyabiashara wengi nchini kuikimbia bandari hiyo na kuamua kushushia mizigo yao katika bandari za Mombasa, Zanzibar na Dar es Salaaa.

HATARINI 'KUTOGRADUATE'

ZANZIBAR
Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kimesema wanafunzi wote wanaomaliza masomo yao na ambao hawatakamilisha malipo ya ada hadi Agosti 22 mwaka huu hawataruhusiwa kufanya mitihani yao ya muhula wa pili kwa mwaka 2011/2012.
SUZA inatarajia kuanza mitihani yake ya muhula wa pili ya kufunga mwaka wasomo kuanzia Agosti 22 mwaka huu chuoni hapo.
Onyo hilo limetolewa na Makamu Mkuu wa SUZA Professa Idriss Ahmad Rai mbele ya waandishi wa habari muda mfupi baada ya kikao cha pamoja kati ya uongozi wa chuo na serikali ya wanafunzi kwenye Makao Makuu ya chuo hicho Vuga, mjini Unguja.
Profesa Rai amesema onyo hilo halitawahusu wanafunzi wa mwaka wa kwanza na wa pili ambao wameruhusiwa kufanya mitihani baada ya kujaza mkataba maalum baina ya mwanafunzi binafsi na chuo.
Profesa Rai amesema mkataba huo utawalazimisha wanafunzi hao kulipa malimbikizo ya ada wanayodaiwa kabla ya kuanza muhula mpya wa masomo unaotarajiwa kuanza Oktoba mwaka huu na kwamba watakaoshindwa kulipa hawataruhusiwa kuanza masomo katika muhula huo.
Hata hivyo amesema wanafunzi watakaoshindwa kuanza mitihani Agosti 22 mwaka watapewa nafasi ya kufanya mitihani wakati wa mitihani ya marejeo (supplementary examination) lakini kwa upande wao utakuwa ndio mtihani wa kawaida iwapo watakamilisha malipo ya madeni yao.
Professa Rai amesema SUZA imeamua kufanya uwamuzi huo mzito kutokana na wanafunzi wengi kushindwa kulipa ada zao na hivi sasa wanawadai kiasi cha shilingi 270 milioni.
Amesema lengo la chuo siyo kuwakomoa wanafunzi lakini ni njia ya kuhakikisha wanapata fedha ambazo ni muhimu katika kukiendeleza chuo hicho pamoja na ruzuku inayotolewa na Serikali.
Ameongeza kuwa wanaelewa ugumu wa maisha unaowakabili wanafunzi wengi hasa katika kipindi hiki cha mwezi wa Ramadhani na kuelekea sikukuu ya IDD-EL-FITRI lakini alidai hakuna njia ya mkato ya kupata mapato ya kuendesha chuo hicho.

NGALAWA AWAASA WAISLAAM


TANGA
MKUU wa Mkoa wa Tanga Chiku Ngallawa, amewataka Waislamu katika kipindi hiki cha kuelekea mwisho wa mfungo wa Ramadhani kuhakikisha mafunzo wanayoyapata kutoka kwa Mashekh wao wanayaendeleza hata baada ya mfungo wa mwezi mtukufu.
Ngallawa ameyasema hayo katika futari iliyoandaliwa na Bank ya CRDB tawi la Tanga.
Ngallawa amesema tabia ya upendo na kuoneana huruma katika jamii iliyojengeka miongoni mwa waislaam kipindi hiki cha Ramadhani ni dalili za kuyapokea mafunzo mbalimbali yanayotolewa na Masheikh.
Kwa upande wake Meneja wa huduma kwa wateja wa CRDB Makao Makuu, Godwin Semunyu, amesema kwa kuzingatia utukufu wa mwezi wa Ramadhani ndio mana wamekuwa na utaratibu wa kufuturisha lengo likiwa ni kuleta umoja na mshikamano katika jamii.
Semunyu amesema CRDB itaendelea kuwa karibu na Waislamu hasa katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na kutoa misaada kadiri ya uwezo wake kwa kuwkufanya hivyo ni faida kubwa kwa jamii na beki hiyo.

Tuesday, August 14, 2012

MABAKI YA NDEGE ZA JESHI LA UGANDA YAPATIKANA KENYA

Mabaki ya Helikopta mbili za Uganda ambazo ziliripotiwa kutoweka siku ya Jumapili zimepatikana mashambani nchini kenya. Kanali Cyrus Oguna ambae ni msemaji wa jeshi la Kenya amesema hatma ya watu 14 waliokuwemo ndani ya chombo hicho haijulikani.
Ndege hizo mbili zilikuwa ni sehemu ya vifaa vilivyokuwa vikipelekwa nchini Somalia kuongezea nguvu kikosi cha umoja wa Afrika kilichoko huko.
Helikopta ya tatu ambayo pia ilikuwa katika msafari huo ilitua kwa ghafla katika eneo la mlima Kenya siku ya Jumapili.
Kanali Oguna amesema wote waliokuwa katika helikopta hiyo ya tatu waliokolewa.
Ni helikopta moja peke yake ndio faulu kutua vizuri na kuongeza mafuta katika mji wa Garissa ulioiko kaskzzini mwa Kenya.
Helikopta hizo nne ambazo zimetengezezwa Urusi ziliondoka siku ya Jumapili Uganda zikelekea Somalia kabla ya kukumbwa na mkasa huo.
Masalia ya helikopta hizo mbili ambazo awali ziliripotiwa kutoweka zilionekana juu ya mlima Kenya na maafisa wa Shirika la Wanyama pori, limeripoti gazeti la Daily Nation la Kenya.
Msemaji wa jeshi Kanali Oguna ameimbia BBC kwamba kikosi cha jeshi la Kenya linaelekea katika eneo hilo la Mlima Kenya , ambao ndio mlima wapili kwa urefu ,afrika.
Afisa huyo amefafanua kwamba moja ya helikopta hizo imeharibika kabisa ilhali ya pili imeharibika kiasi.
Helikpta hizo zilikuwa zinaelekea nchini Somalia kuongezea nguvu vikosi vya Umoja wa Afrika ambavyo vinajitayarisha kuvamia mji wa Kismayo na kuwafurusha wapiganaji wa Al Shabaab toka mji huo ambyo ndio ngome yao kuu.
CHANZO: www.bbcswahili.com

UNAIKUMBUKA HIII?

WIZZI MTUPPPPPPPPPPPPPPPP

TUNATAKA MATUTA


Wanafunzi wa Shule za Msingi Ndugumbi na Mwalimu Nyerere, Magomeni, Kinondoni jijini Dar es Salaam, wakiandamana katika Barabara ya Kawawa, kushinikiza Wakala wa Barabara wa Serikali (TANROADS), kuweka matuta barabarani,baada ya wenzao wawili kugongwa.

BREAKIING NEWSSSS

MABOMU YA MACHOZI YANAENDELEA KUPIGWA KIGAMBONI BAADA YA WACHIMBA KOKOTO KUFANYA VURUGU NA KUFUNGA BARABARA

HALI sasa si shwari eneo la Mji Mwema, Kigamboni, Dar es Salaam, baada ya wachimba kokoto kufanya vurugu kwa kufunga barabara kwa mawe na kuwasha matairi barabaran wakipinga kitendo cha Serikali kuwazuia kuchimba kokoto.
Mkazi mmoja wa Mji Mwema aliye karibu na makazi ya Rais msitaafu wa wa Zanzibar Alhaji Aboud Jumbe, amesema hali ni mbaya kiasi cha asilimia kubwa ya wakazi wa eneo hilo kujifungia majumbani wakihofia vurugu hizo.

"Ndugu mwandishi wa habari, hali hivi sasa ni mbaya mno, mawasiliano ya usafiri yamekatika kwani wachimba kokoto waliozuiwa kufanya kazi yao, wameandamana huku wengine wakijaza kokoto na mawe barabarani na wengine wakichoma matairi, tunaogopa hivyo tumejifungia majumbani" alisema mama huyo.

Alisema mabomu ya machozi yanaendelea kupigwa na FFU ili kuwatawanya vijana hao, lakini inaelekea ni wabishi.

Blogu yako ya Kamanda wa Matukio itaendelea kuwapatia taarifa juu ya sakata hilo kwa kadri itakavyokuwa inazipata.
CHANZO: mwaikenda.blogspot.com

MAREKANI YAVURUGA MAMBO MASHARIKI YA KATI

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema Marekani ina nafasi haribifu kuhusiana na matukio ya Mashariki ya Kati.
Kuhusu mpango wa Marekani wa kutaka kuanzisha eneo lisiloruhusiwa kupaa ndege huko Syria, Ramin Mehmanparast Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ameongeza kuwa Marekani imeazimia kufanya uharibifu na mauaji huko Syria kama ilivyofanya huko Iraq, Afghanistan, Libya na katika nchi nyinginezo.
Amesema Marekani inajaribu kila inaloweza  kusababisha mauaji mengi miongoni mwa raia na umma wa Kiislamu katika eneo la Mashariki ya Kati. Ramin Mehmanparast amesema Marekani inafanya kila iwezalo ili kunufaika zaidi sambamba na waitifaki wake. 
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema hivi sasa kunafanywa njama kwa ajili ya kuandaa utangulizi wa kuzusha mapigano ya kijeshi huko Syria kupitia kutangazwa eneo lisiloruhusiwa kupaa ndege na kwamba hiyo ni tahadhari kwa nchi zote za eneo  kwamba fitna kubwa inafanywa ili kuzigombanisha nchi za Kiislamu katika eneo hili na kwamba Marekani na Uzayuni  zinafanya kila linalowezekana kwa malengo yao ya kisiasa  yakuzusha mapigano na kusababisha vifo vya raia wasio nan hatia na kusababisha hasara kubwa katika eneo hili kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni.

JAPAN YAKUMBWA NA TETEMEKO LA ARDHI

Mtetemeko wa ardhi wenye ukubwa wa 7.3 kwa kipimo cha rishta umeyatikisha maeneo ya kaskazini na kaskazini mashariki mwa Japan kama ilivyoripotiwa na kituo cha metorolojia cha nchi hiyo. 
Mtetemeko huo wa ardhi umetokea alfajiri ya leo na kitovu cha zilzala hiyo kilikuwa katika pwani ya Hokkaido katika bahari ya Okhotsk. 
Juni 18 mwaka huu pia mtetemeko wa ardhi uliokuwa na ukubwa wa 6.4 kwa kipimo cha rishta ulitokea katika bahari ya Pasifiki, umbali wa kilomita 28 kusini mashariki mwa mji wa Ofunato huko Japan. Hakuna taarifa zozote zilizotolewa hadi sasa kuhusu watu waliopoteza maisha yao na wala maafa yaliyosababishwa na zilzala hiyo ya leo. 
CHANZO REDIO NYUMBANI

MSOMALI AHUKUMIWA MAISHA JELA

Raia mmoja wa Somalia ambaye anayedaiwa kuwa alikuwa mzungumzaji wa maharamia katika kupokea vikomboleo kwa ajili maharamia wa Somalia walioteka nyara meli moja ya Marekani mwaka uliopita na kuwauwa mateka wanne raia wa Marekani amehukumiwa vifungo 12 vya maisha na mahakama ya Marekani. 
Mohamed Shibin alipatwa na hatia mwezi Aprili mwaka huu kwa makosa 15 yakiwemo uharamia, kuteka nyara na kula njama. Mahakma hiyo ya Marekani imesema kuwa Shibin alilipwa kati ya dola elfu 30 hadi 50 kwa kazi yake ya kuwa mzungumzaji wa maharamia kwa ajili ya kupatiwa kikomboleo. 
CHANZO: REDIONYUMBANI

JUMIKI YATOA UFAFANUZI

Ali Issa-Maelezo Zanziba
Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu (JUMIKI) imepinga uvumi uliosambazwa nchini kuwa leo kutakuwa na maandamano ya Jumuiya hiyo na kudai kuwa propaganda hizo zinaendeshwa na baadhi ya watendaji katika jeshi la polisi na usalama wa taifa ambao hawaitakii mema Jumuiya yao.
Hayo yamesemwa na Amiri wa Jumuiya hiyo Sheikh Farid Ahmed wakati alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Habari Maelezo Zanzķbar kuhusiana na tuhuma ambazo wamezitoa kwa Jeshi la Polisi dhidi ya Jumuiya yao.
Amedai kuwa Jumuiya haijapanga maandamano kwani ni taasisi inayofanya kazi zake kisheria nakwamba hata ikitokezea kufanya maandamano basi watafuata taratibu zote za kisheria ikiwa ni pamoja na kulitaarifu rasmi Jeshi la Polisi.
Aidha amedai kuwa kuna mkakati wa muda mrefu wa kutaka kuwabatiza viongozi wakuu wa jumuiya hiyo kesi za ugaidi hususan Amir Mkuu wa jumuiya ya Maimamu Zanzibar Sheikh Farid Hadi Ahmed ili kuzima vuguvugu la kudai Zanzibar huru.
Shekh Faridi amedai kuwa inasemekana kuna mahusiano makubwa baina ya watendaji ndani ya Jeshi la polisi pamoja na baadhi ya wageni wanaosadikiwa kuwa ni raia wa Marekani juu ya kuutekeleza mkakati huo baada ya kuwa tayari umeshakamilika.
Amedai kuwa kuna ukiukwaji mkubwa wa haki za kirai ambao umekuwa ukifanywa na Jeshi la Polisi Zanzibar kwa kuwanyima haki ya kufanya mihadhara yao ndani ya Misikiti  ambapo Juni 17 mwaka huu wananchi mbalimbali walijeruhiwa kwa mabomu katika vijiji vya Donge,Mkwajuni na Mahonda.
Ameliomba Jeshi la Polisi kufanya kazi zake za kulinda usalama wa wananchi na mali zao na kuacha kufanya kinyume chake kwani huko ni kuchochea chuki kati ya Jeshi hilo na raia.
Amesisitiza haja ya wazanzibari kuungana na kuachana na Itikadi zao za kivyama katika kudai hadhi ya Rais na mamlaka ya Nchi ya Zanzibar ndani na nje ya Zanzibar pale tume ya mabadiliko ya Katiba itakapoanza kazi zake.
Kwa upande wake Naibu Naibu Amir Jumuiya Ya Uamsho Na Mihadhara Ya Kiisilam Sheikh, Azan Khalid Hamdan amewaomba wanahabari nao kuwa makini katika taaluma yao kwa kufanya usawa wa taarifa ambazo wamekuwa wakizitoa.
Hivi karibuni Jumuiya hiyo ilitangaza rasmi kushiriki kikamilifu katika zoezi zima la kutoa maoni yao katika mchakato wa kupata Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kubadili msimamo wao wa awali wa kuisusia Tume hiyo.

KUFUATIA AJALI YA MV SKAGIT MELI 3 ZAFUTIWA USAJILI ZNZ

Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar imezifutia rasmi hati ya kufanya kazi Meli ya Mv.Kalama, Mv.Seagul na Mv.Sepideh kutokana na meli hizo kutokukidhi hali ya usalama wa abiria katika meli hizo.
Aidha meli hizo zimepewa muda wa mwezi mmoja kuanzia leo kuhakikisha zimeondoka katika maeneo ya Zanzibar kabla ya hatua zaidi kuchukuliwa dhidi ya wamiliki wa Meli hizo.
Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mamlaka ya Usafiri wa Baharini Zanzibar Abdullah Husein Kombo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Afisini kwake kuhusu hali ya usafiri wa baharini na usalama Zanzibar.
Amesema Mamlaka hiyo imefanya tathmini na uhakiki wa kutosha na kujiridhisha kuwa Meli hizo hazifai kufanya kazi katika maeneo ya Zanzibar jambo ambalo limepelekea kuchukua hatua za kufuta hati za kufanyia kazi meli hizo.
Amefahamisha kuwa sababu kuu zilizopelekea Mamlaka kufanya maamuzi hayo ni pamoja na uchakavu,umri wa meli hizo kuwa mrefu na kupata matatizo mara kwa mara katika safari zao.
Kombo amefahamisha kuwa Sheria ya Mamlaka ya Usafiri na Bandari Zanzibar ya mwaka 2006 kifungu cha 17.1 inampa mamlaka Msajili wa Meli kuifuta meli yoyote ambayo itakuwa haikidhi usalama wa abiria.
Kufuatia sheria hiyo Kombo amesema watawataka wamiliki wa Meli hizo kuzirudisha hati za kufanyia kazi meli hizo ili waende kutafuta sehemu nyengine za usajili kinyume na maeneo ya Zanzibar.
Akizungumzia Meli ya Mv.Serengeti Kombo amesema wamelazimika kuiagiza meli hiyo kupunguza idadi ya abiria kutoka watu 800 hadi 350 na tani za mizigo kutoka 100 hadi 50  hadi pale ambapo watajiridhisha kutokana na hali ya meli hiyo ilivyo.
Aidha amegusia kuwa Kampuni ya Bakhresa italeta Meli kubwa ya abiria itakayofanya kazi zake Zanzibar ambapo pia Serikali ya Mapinduzi nayo iko mbioni kuhakikisha wanaleta meli inayokidhi mahitaji ya wananchi wa Zanzibar.

TUMAINI LILILOPOTEA, LAIBUKA TENA

Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar,Balozi Seif Ali Idd amesema juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutafuta Meli kubwa kwa ajili ya wananchi wake zinaleta matumaini kutokana na Watendaji husika waliopewa agizo hilo kulisimamia kwa nguvu zote katika kulifanikisha.
Amesema Wizara ya Fedha Uchumi na Maendeleo kwa kushirikiana na Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Zanzķbar tayari imeanza mikakati ya kupatikana kwa Meli hiyo ikiwa ni pamoja na kukusanya pesa kutoka vyanzo mbali mbali vikiwemo vile vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Balozi Seif ameyasema hayo leo alipokuwa akitoa hotuba yake ya kuahirisha kikao cha nane cha Baraza la Wawakilishi ambacho kilianza June mwaka huu huko Mbweni nje kidogo ya mji wa Zanzibar.  
Amesema Serikali ya Mapinduzi imejipanga vyema kukabiliana na matatizo yanayowakabili wananchi likiwemo suala la usafiri wa baharini ambapo kupatikana kwa meli hiyo kutaweza kutatua tatizo hilo ambalo limeonekana linaathiri sana uchumi wa wananchi wa Zanzibar.  
Aidha amewahakikishia Wajumbe wa Baraza hilo kuwa ripoti iliyotolewa na Kamati ya kusimamia matumizi ya Serikali PAC, Serikali inaifanyia kazi kwa umakini ili kuweza kutoa maamuzi ya uhakika na sahihi.
Amewataka Wajumbe hao kuendelea kuwa na subra ili suala hilo liweze kukamilika na Serikali haitasita kueleza bayana juu ya maamuzi yake ambayo watayatoa.
Balozi amefahamisha kuwa katika kuwajengea uwezo Akinamama tayari Serikali imetafuta wataalamu wa kufanya uchambuzi yakinifu ili kuanzisha Benki ya Wanawake Zanzibar.
Kuhusu suala la utumiaji wa Madawa ya kulevya Balozi ameeleza kuwa suala hilo linawahusu wananchi wote na kwamba Serikali inawahakikishia usalama wale wote ambao wataweza kutoa taarifa za watu wanaojihusisha na madawa hayo.
Akielezea juu ya umuhimu wa amani ya nchi Balozi amesema kuwa Amani ya nchi ndio rasilimali muhimu ambayo haifai kuchezewa na kwamba kila mwananchi anajukumu la kuienzi .
Amesema Serikali iko makini katika kukabiliana na viashiria vyovyote vya kuhatarisha amani ya nchi na haitochelea kumchukulia hatua mtu yeyote atakayeweza kuchezea na kuhatarisha amani hiyo.
Balozi amewataka wananchi ambao hawajapata nafasi ya kutoa maoni yao juu ya Katiba mpya kujitayarisha kutoa maoni yao pale zoezi hilo litakapoendelea katika maeneo ambayo bado halijafanyika.
Amesema ni vyema wananchi kujitayarisha vyema kwa kuiga wenzao ambao waliweza kuitumia nafasi hiyo vyema katika Mkoa wa Kusini Unguja na Kusini Pemba.
Kikao cha Baraza la Wawakilishi kilichoanza mwezi wa Juni kimeahirishwa leo hadi Octoba 10 mwaka huu baada ya kupitisha makadirio ya matumizi ya fedha kwa Wizara zote za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.